Imani inapungua kwa sababu mbalimbali ikiwa ni pamoja na:

1- Mtu kuwa mjinga wa kutomjua Allaah (Ta´ala) na majina na sifa Zake.

2- Mtu kughafilika na kuzipuuza alama za Allaah za kilimwengu na za kidini. Hakika mambo hayo yanasababisha moyo kuwa na maradhi au kufa kabisa kwa vile matamanio na utata vimeshika nafasi juu yake.

3- Kufanya maasi. Imani inashuka kwa kutegemea na sampuli ya maasi, kiwango chake, kuyachukulia wepesi na ile nguvu ya pupa juu yake.

Kuhusiana na sampuli na viwango vyake, imani inashuka zaidi kwa madhambi makubwa kuliko inavyoshuka kwa madhambi madogo. Imani inashuka zaidi kwa kuua nafsi isiyokuwa na hatia kuliko mtu anapochukua mali ya mtu pasi na haki. Imani inashuka zaidi kwa dhambi mbili kuliko inavyoshuka kwa kufanya dhambi moja na kadhalika.

Ama kuhusu kuchukulia wepesi maasi, imani inashuka zaidi ikiwa inatokana na mtu ambaye khofu yake kwa Allaah ni dhaifu kuliko inavyoshuka pindi inatokana na mtu ambaye anamuadhimisha zaidi Allaah na ni mwenye kumuogopa zaidi lakini hata hivyo imetokea amemuasi.

Kuhusu ile nguvu ya pupa juu ya maasi, imani inashuka zaidi ikiwa yanafanywa na mtu ambaye upupiaji wake wa maasi una unyonge kuliko yanapofanywa na mtu ambaye upupiaji wake wa maasi una nguvu zaidi. Ndio maana ikawa jeuri ya fakiri na uzinifu wa mtumzima ni jambo lina dhambi kubwa kuliko jeuri ya mtu ambaye ni tajiri na uzinifu wa kijana. Hadiyth inasema:

“Watu aina tatu Allaah hatowasemeza, hatowatazama siku ya Qiyaamah na wala hatowatakasa na watakuwa na adhabu kali.”[1]

Miongoni mwao akamtaja mzee ambaye ni mzinifu na fakiri mwenye jeuri kutokana na udhaifu wao katika kupupia dhambi hizi.

4- Kuacha utiifu. Imani inashuka kwa kuacha utiifu. Inashuka kwa kutegemea na uzito wa utiifu huo. Kadri ambavyo utiifu utakuwa umesisitizwa zaidi, ndivyo jinsi imani inashuka zaidi kwa kuacha kuufanya. Imani inaweza kutoweka kabisakabisa kwa mfano mtu kuacha kuswali.

Kushuka kwa imani kwa kuacha utiifu kumegawanyika aina mbili:

1- Aina ambayo mtu anaadhibiwa kwayo na ni kule mtu kuacha kitu cha wajibu pasi na udhuru.

2- Aina ambayo mtu haadhibiwi kwayo na ni kule kuacha kitu cha wajibu kwa sababu ya udhuru wa Kishari´ah na kuacha kitu kilichopendekezwa. Mfano wa aina ya kwanza ni kama mwanamke kuacha kuswali wakati yuko katika hedhi na mfano wa aina ya pili ni kama kuacha kuswali swalah ya Dhuhaa.

[1] at-Twabaraaniy katika ”al-Mu´jam al-Kabiyr” (6111). Swahiyh kwa mujibu wa al-Albaaniy katika ”Swahiyh-ul-Jaami´” (3072).

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Fath Rabb-il-Bariyyah, uk. 95-96
  • Imechapishwa: 15/05/2020