Shirki imegawanyika aina mbili:

1- Shirki kubwa inayomtoa mwenye nayo nje ya Uislamu. Mwenye nayo anadumishwa Motoni milele akifa kabla ya kutubia kwayo. Shirki ni kule kufanya kitu katika aina za ´ibaadah kumfanyia asiyekuwa Allaah kama mfano wa kumuomba asiyekuwa Allaah, kujikurubisha kwa kuchinja na kuweka nadhiri kwa asiyekuwa Allaah katika makaburi, majini na mashaytwaan. Vilevile kuwa na khofu juu ya wafu, majini au mashaytwaan wasimdhuru au wasimfanye akagonjweka. Pia kuwa na matarajio kwa asiyekuwa Allaah katika mambo yasiyoweza yeyote isipokuwa Allaah katika kutatua haja mbalimbali na kuondosha matatizo miongoni mwa mambo yanayofanywa hii leo pambizoni mwa makuba yaliyojengwa juu ya makaburi ya mawalii na waja wema. Amesema (Ta´ala):

وَيَعْبُدُونَ مِن دُونِ اللَّـهِ مَا لَا يَضُرُّهُمْ وَلَا يَنفَعُهُمْ وَيَقُولُونَ هَـٰؤُلَاءِ شُفَعَاؤُنَا عِندَ اللَّـهِ ۚ قُلْ أَتُنَبِّئُونَ اللَّـهَ بِمَا لَا يَعْلَمُ فِي السَّمَاوَاتِ وَلَا فِي الْأَرْضِ ۚ سُبْحَانَهُ وَتَعَالَىٰ عَمَّا يُشْرِكُونَ

“Wanaabudia pasi na Allaah ambavyo haviwadhuru wala haviwanufaishi na wanasema: “Hawa ni waombezi wetu mbele ya Allaah.” Sema: “Je, mnamjulisha Allaah kwa yale asiyoyajua katika mbingu na ardhini?” Utakasifu ni Wake na ametukuka juu kabisa kutokamana na yale yote wanayomshirikisha.”[1]

2- Shirki ndogo isiyomtoa mtu nje ya Uislamu. Lakini hata hivyo inapunguza Tawhiyd na ni njia inayopelekea katika shirki kubwa. Shirki aina hii imegawanyika sampuli mbili:

Ya kwanza: Shirki iliodhahiri mdomoni na kwenye viungo vya mwili. Nayo ni yale matamshi na matendo. Mfano wa matamshi ni kuapa kwa asiyekuwa Allaah. Amesema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Mwenye kuapa kwa asiyekuwa Allaah amekufuru au ameshirikisha.”[2]

Kama kusema:

“Akitaka Allaah na ukataka.”

Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alisema wakati mtu mmoja alipomwambia:

“Akitaka Allaah na ukataka.” Akasema:

“Umenifanya ni mshirika wa Allaah? Sema: “Akitaka Allaah  pekee.”[3]

Kama kusema:

“Lau kama si Allaah na fulani.”

Sahihi ni mtu kusema:

“Akitaka Allaah kisha fulani akataka.”

au kusema:

“Lau kama si Allaah kisha fulani.”

Kwa sababu “kisha” inafidisha mpangilio pamoja na kufanywa matakwa ya mja ni yenye kufuata matakwa ya Allaah. Amesema (Ta´ala):

وَمَا تَشَاءُونَ إِلَّا أَن يَشَاءَ اللَّـهُ رَبُّ الْعَالَمِينَ

”Hamtotaka isipokuwa atake Allaah, Mola wa walimwengu.”[4]

Kuhusu “na” inaonyesha ukusanyaji na ushirikiano. Haipelekei katika mpangilio. Mfano wake ni kama kusema:

“Mimi si wa mwingine isipokuwa ni wa Allaah na wewe.”

na:

“Haya ni kutokana na baraka za Allaah na baraka zako.”

Ama matendo ni kama kuvaa uzi kwa ajili ya kuondosha au kuzuia majanga. Mfano mwingine ni kuvaa hirizi kwa ajili ya kuogopa kijicho na vyenginevyo. Akiamini kuwa hii ni sababu ya kuondosha au kuzuia majanga inakuwa shirki ndogo. Kwa sababu Allaah hakufanya kitu hicho kuwa ni sababu. Ama akiamini kuwa yenyewe kama yenyewe ndio yenye kuondosha au kuzuia majanga inakuwa shirki kubwa. Kwa sababu amemtegemea asiyekuwa Allaah.

[1] 10:18

[2] Ahmad (6072), Abu Daawuud (3251) na at-Tirmidhiy (1539).

[3] Ahmad (1839).

[4] 81:29

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: ´Aqiydat-ut-Tawhiyd, uk. 83-84
  • Imechapishwa: 11/03/2020