42. Hukumu ya mwenye kufa wakati wa kujitetea

Imaam Ahmad bin Hanbal (Rahimahu Allaah) amesema:

“Na ikitokea yeye ndiye akafa wakati yuko anaitetea nafsi yake na mali yake, kunatarajiwa kwake kufa shahidi. Hivyo ndivyo ilivyotajwa katika Hadiyth na mapokezi. Vinaamrisha tu kujitetea na wala haviamrishi yule mshambulizi kuuawa wala kufuatwa. Wala usimalize uhai wake endapo ataanguka chini au akapata majeraha. Hafai vilevile kwake kumuua wala kumsimamishia adhabu iwapo atamkamata. Badala yake anatakiwa kumpeleka mahakamani na awaache wamuhukumu.”

MAELEZO

Hayo ni kutokana na Hadiyth kutoka kwa Abu Hurayrah (Radhiya Allaahu ´anh) ambaye amesema:

“Kuna mtu alikuja kwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akasema: “Ee Mtume wa Allaah! Unaonaje iwapo atakuja mtu anayetaka kuchukua mali yangu?” Akasema: “Usimpe.” Akauliza: “Akinipiga vita?” Akajibu: “Mpige vita.” Akauliza: “Akiniua?” Akajibu: “Basi wewe utakuwa shahidi.” Akauliza: “Nikimuua?” Akajibu: “Basi yeye ataingia Motoni.”[1]

Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema vilevile:

“Atakayeuawa kwa ajili ya kutetea nafsi yake ni shahidi. Atakayeuawa kwa ajili ya kutetea mali yake ni shahidi. Atakayeuawa kwa ajili ya kutetea dini yake ni shahidi.”[2]

Haijuzu kuwaua majeruhi wao, kuwafuata wasaliti wao, kuchukua mali zao wala kuwateka wanawake wao – kwa sababu ni waislamu.

[1] Muslim (140).

[2] Abu Daawuud (4772), at-Tirmidhiy (1421) na an-Nasaa’iy (4094). Swahiyh kwa mujibu wa al-Albaaniy katika ”Swahiyh-ut-Targhiyb wat-Tarhiyb (1411).

  • Mhusika: ´Allaamah Ahmad bin Yahyaa an-Najmiy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Itmaam-ul-Minnah, uk. 149-150
  • Imechapishwa: 01/05/2019