40. Shubuha ya nne ya watu wa Tawassul na majibu juu yake

4- Shubuha ya nne: Nayo ndio shubuha yao kubwa. Wanasema kwamba ´Umar (Radhiya Allaahu ´anh) alitawassul kwa ´Abbaas (Radhiya Allaahu ´anh) katika kuomba mvua wakati kulipokuwa ukame wakaomba wanyeshelezewe ambapo ´Umar (Radhiya Allaahu ´anh) alimuomba ´Abbaas (Radhiya Allaahu ´anh), ambaye ni ami yake Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam), awaombee kwa Allaah ateremshe mvua. Alisema:

“Ee Allaah! Hakika sisi tulikuwa tukitawassul Kwako kwa [du´aa ya] Mtume Wako. Tunyweshelezee. Hakika sisi hivi sasa tunatawassul Kwako kwa [du´aa ya] ami wa Mtume Wetu. Tunyweshelezee. Simama, ee ´Abbaas, na uombe! Akasimama ´Abbaas na akawaombea ambapo Allaah akawaitikia.”[1]

Wanatumia hoja hii na kusema hii ni Tawassul na kwamba ´Umar ametawassul kupitia ´Abbaas. Hii ni dalili ya kwamba kufanya mkati na kati ni jambo linalojuzu.

Tunawaambia: Allaah ametakasika kutokamana na mapungufu! ´Umar ametawassul kwa du´aa ya ´Abbaas na wala hakutawassul kwa ´Abbaas mwenyewe. Bali alichofanya ni kutawassul kwa du´aa yake. Amesema:

“Simama na uombe!”

Kuomba du´aa kutoka kwa watu wema ni jambo lililowekwa katika Shari´ah. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alimwambia ´Umar pindi ´Umar (Radhiya Allaahu ´anh) alipotaka kusafiri kwenda ´Umrah ambapo akawa amemuaga, ndipo Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akamwambia:

“Usinisahau, ewe ndugu yangu, kwa zile du´aa zako njema.”[2]

Kwa hivyo kuomba du´aa kutoka kwa watu wema waliohai ni jambo linalokubalika Kishari´ah. Ama maiti haombwi kitu. Lakini mtu mwema na aliye mbele yako inajuzu kwako kumuomba akuombee kwa Allaah au awaombee waislamu.

Vivyo hivyo Mu´aawiyah (Radhiya Allaahu ´anh) alipoomba kunyweshelezwa alimwamrisha Yaziyd (ambaye ni Ibn al-As-wad) al-Jarshiy amuombe Allaah ambapo akawa amemuomba Allaah[3]. Kujengea juu ya hili wanachuoni wa Fiqh wamesema katika “Kitaab-ul-Istisqaa´”:

“Imependekezwa kutawassul kwa waja wema.”[4]

Bi maana kufanya Tawassul kwa du´aa zao. Ingekuwa makusudio ni kutawassul kwa dhati zao, kwa fadhilah zao na nafasi zao, basi Maswahabah wasingelimwacha Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Kwa sababu Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ana nafasi na jaha mbele ya Allaah. Hadhi na jaha yake si yenye kwisha baada ya kufa kwake (´alayhis-Swalaah was-Salaam). Pamoja na hivyo, hawakumuomba Allaah kwa jaha, haki wala kwa matendo ya Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Wakamwacha Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam), ilihali yeye ndiye kiumbe bora kabisa, na badala yake wakamwende ambaye ana fadhilah ya chini kulikoni, naye si mwingine ni ami yake ´Abbaas. Kwa nini walimwacha ambaye ana fadhilah za juu zaidi na kumwendea ambaye anashindwa fadhilah? Hakuna sababu nyingine isipokuwa ni kwa kuwa aliye na fadhilah zaidi tayari amekwishakufa na maiti haombwi chochote. Anayeombwa ni ambaye yuhai. Huyu ndiye anaombwa mali, du´aa, msaada na kadhalika. Ikiwa ni muweza na yuko mbele yako. Amesema (Ta´ala):

وَتَعَاوَنُوا عَلَى الْبِرِّ وَالتَّقْوَىٰ

“Saidianeni katika wema na uchaji.” (al-Maaidah 05:02)

“Simama, ee ´Abbaas, na uombe! Akasimama ´Abbaas na akawaombea.”Haya ndio majibu kwao kuhusu qadhiya hii ya ´Umar (Radhiya Allaahu ´anh) kutawassul kwa ´Abbaas (Radhiya Allaahu ´anh). Hakutawassul kwa dhati ya ´Abbaas, kwa haki ya ´Abbaas au kwa jaha ya ´Abbaas. Kwa sababu hili ni jambo batili. Alichofanya ´Umar (Radhiya Allaahu ´anh) ni kutawassul kwa du´aa ya ´Abbaas ambapo akamwambia:

Na hili ni jambo linalojuzu na halina ubaya.

[1]Ameipokea al-Bukhaariy (1010) kutoka katika Hadiyth ya Anas bin Maalik (Radhiya Allaahu ´anh).

[2] Ameipokea Ahmad (195), Abu Daawuud (1398), at-Tirmidhiy (3562) na Ibn Maajah (2894) kutoka katika Hadiyth ya ´Umar bin al-Khattwaab (Radhiya Allaahu ´anh). at-Tirmidhiy amesema:

“Hadiyth ni nzuri (Hasan) na Swahiyh.”

[3] Ameipokea Abu Zar´ah ad-Dimashqiy (1/602), al-Laalakaa´iy katika “Sharh I´tiqaad Ahl-is-Sunnah” (9/214-215). al-Albaaniy amesahihisha cheni ya wapokezi wake.

[4] Tazama “al-Mughniy” (3/346) na “al-Kaafiy” (1/535).

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh Nawaaqidh-il-Islaam, uk. 66-68
  • Imechapishwa: 11/08/2018