Wanaraddiwa kwa njia mbalimbali:

Ya kwanza: Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala) amejithibitishia Mwenyewe majina na sifa Zake na akathibitishiwa na Mtume Wake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Kumkanushia nayo Allaah au kukanusha baadhi yake ni kukanusha yale aliyothibitisha Allaah na Mtume Wake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam), mambo ambayo ni kupingana na Allaah na Mtume Wake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam).

Ya pili: Kupatikana sifa hizi kwa viumbe au baadhi ya viumbe kujiita kitu katika majina hayo hakupelekei kumfananisha Allaah na viumbe Wake. Allaah ana majina na sifa ambazo ni maalum Kwake na viumbe wana majina na sifa ambazo ni maalum kwao pekee. Kama ambavo Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala) ana dhati isiyofanana na dhati za viumbe basi kadhalika ana majina na sifa zisizofanana na majina na sifa za viumbe. Kushirikiana katika majina na maana yenye kuenea hakulazimishi kushirikiana katika uhakika. Allaah amejiita Mwenyewe kuwa ni mjuzi na mpole na amewaita baadhi ya waja Wake kwamba ni wajuzi. Amesema:

وَبَشَّرُوهُ بِغُلَامٍ عَلِيمٍ

“Wakambashiria kijana mjuzi.”[1]

Bi maana Ishaaq.

Akamwita mwengine kuwa ni mpole. Amesema:

فَبَشَّرْنَاهُ بِغُلَامٍ حَلِيمٍ

“Tukambashiria kijana mvumilivu.”[2]

Bi maana Ismaa´iyl.

Lakini hata hivyo mjuzi huyu si kama mjuzi huyu na mpole huyu si kama mpole huyu. Amejiita Mwenyewe kwa kusema:

إِنَّ اللَّـهَ يَأْمُرُكُمْ أَن تُؤَدُّوا الْأَمَانَاتِ إِلَىٰ أَهْلِهَا وَإِذَا حَكَمْتُم بَيْنَ النَّاسِ أَن تَحْكُمُوا بِالْعَدْلِ ۚ إِنَّ اللَّـهَ نِعِمَّا يَعِظُكُم بِهِ ۗ إِنَّ اللَّـهَ كَانَ سَمِيعًا بَصِيرًا

“Hakika Allaah anakuamrisheni kurudisha amana kwa wenyewe na pindi mtakapohukumu kati ya watu, basi hukumuni kwa uadilifu. Hakika uzuri ulioje anayokuwaidhini kwayo Allaah. Hakika Allaah ni Mwenye kusikia, Mwenye kuona.”[3]

Amewaita baadhi ya waja Wake kwamba ni wenye kusikia na kuona pale aliposema:

إِنَّا خَلَقْنَا الْإِنسَانَ مِن نُّطْفَةٍ أَمْشَاجٍ نَّبْتَلِيهِ فَجَعَلْنَاهُ سَمِيعًا بَصِيرًا

“Hakika Sisi tumemuumba mtu kutokana na tone la manii iliyochanganyika ili tumjaribu tukamjaalia ni mwenye kusikia na mwenye kuona.”[4]

Lakini msikiaji huyu si kama msikiaji huyu na muonaji huyu si kama muonaji huyu. Amejiita Mwenyewe kwamba ni mpole na Mwenye huruma pale aliposema:

إِنَّ اللَّـهَ بِالنَّاسِ لَرَءُوفٌ رَّحِيمٌ

“Hakika Allaah kwa watu ni Mwenye huruma mno, Mwenye kurehemu.”[5]

Akawaita baadhi ya waja Wake kwamba ni wapole na wenye huruma pale aliposema:

لَقَدْ جَاءَكُمْ رَسُولٌ مِّنْ أَنفُسِكُمْ عَزِيزٌ عَلَيْهِ مَا عَنِتُّمْ حَرِيصٌ عَلَيْكُم بِالْمُؤْمِنِينَ رَءُوفٌ رَّحِيمٌ

”Hakika amekujieni Mtume anayetokana na nyinyi wenyewe. Yanamuhuzunisha yanayokutaabisheni, anakuhangaikieni na kwa waliomuamini ni mpole na mwenye huruma.”[6]

Lakini hata hivyo mpole huyu si kama mpole huyu na mwenye huruma huyu si kama mwenye huruma yule.

Vivyo hivyo amejisifu kwa sifa na akawasifu waja Wake mfano wa hivo. Mfano pale aliposema:

وَلَا يُحِيطُونَ بِشَيْءٍ مِّنْ عِلْمِهِ إِلَّا بِمَا شَاءَ

“Wala hawawezi kukizunguka chochote kutoka katika ujuzi Wake isipokuwa kwa akitakacho.”[7]

Akajisifu Mwenyewe kwa sifa ya ujuzi na akawasifu waja Wake kwa ujuzi pale aliposema:

وَمَا أُوتِيتُم مِّنَ الْعِلْمِ إِلَّا قَلِيلًا

“Hamkupewa ujuzi isipokuwa kidogo tu.”[8]

وَفَوْقَ كُلِّ ذِي عِلْمٍ عَلِيمٌ

”Hakika juu ya kila mwenye ujuzi yuko mwenye ujuzi zaidi.”[9]

وَقَالَ الَّذِينَ أُوتُوا الْعِلْمَ

“Wakasema wale waliopewa elimu.”[10]

Amejisifu Mwenyewe kwa sifa ya nguvu pale aliposema:

إِنَّ اللَّـهَ لَقَوِيٌّ عَزِيزٌ

“Hakika Allaah ni Mwenye nguvu kabisa asiyeshindikana.”[11]

إِنَّ اللَّـهَ هُوَ الرَّزَّاقُ ذُو الْقُوَّةِ الْمَتِينُ

“Hakika Allaah ndiye Mwingi wa kuruzuku, Mwenye nguvu madhubuti.”[12]

Akawasifu waja Wake kwa sifa ya nguvu pale aliposema:

اللَّـهُ الَّذِي خَلَقَكُم مِّن ضَعْفٍ ثُمَّ جَعَلَ مِن بَعْدِ ضَعْفٍ قُوَّةً ثُمَّ جَعَلَ مِن بَعْدِ قُوَّةٍ ضَعْفًا وَشَيْبَةً

“Allaah ndiye ambaye amekuumbeni kutokana na udhaifu, kisha akajaalia baada ya udhaifu, nguvu, kisha akajaalia baada ya nguvu udhaifu na uzee.”[13]

Zipo Aayah zengine nyingi.

Ni jambo linalotambulika kwamba majina na sifa za Allaah zinamuhusu Yeye tu na kulingana Naye na majina ya viumbe yanawahusu na kulingana nao wao. Kushirikiana katika majina na maana hakulazimishi kushirikiana katika ukweli wa mambo. Hayo ni kwa sababu haiwezekani kufanana kati ya waitwaji wala wasifiwaji wawili hao, jambo ambalo liko wazi – na himdi zote njema anastahiki Allaah.

Ya tatu: Ambaye hana sifa za ukamilifu hastahiki kuwa mungu. Kwa ajili hiyo Ibraahiym alisema kumwambia baba yake:

لِمَ تَعْبُدُ مَا لَا يَسْمَعُ وَلَا يُبْصِرُ

“Kwa nini unaabudu vile visivyosikia na visivyoona.”[14]

Amesema (Ta´ala) akiwaraddi wale walioabudu ndama:

أَلَمْ يَرَوْا أَنَّهُ لَا يُكَلِّمُهُمْ وَلَا يَهْدِيهِمْ سَبِيلًا

“Je, hawakuona kuwa huyo [ndama] hawazungumzishi na wala hawaongozi njia?”[15]

Ya nne: Kunathibitishwa sifa za ukamilifu na zinakanushwa pungufu. Ambaye hana sifa ima ni kitu kisichokuweko au ni kitu kipungufu. Allaah (Ta´ala) ametakasika kutokamana na hayo.

Ya tano: Kuzipindisha maana sifa kutoka katika udhahiri wake ni jambo halina dalili. Ni kitu cha batili. Kuzitegemeza kwa Allaah maana yake inalazimisha kwamba Allaah ametuzungumzisha ndani ya Qur-aan kwa mambo tusiyofahamu maana yake ilihali ametuamrisha kuizingatia Qur-aan yote. Ni vipi atatuamrisha kuzingatia kitu kisichofahamika maana yake?

Kupitia haya tumepata kubainikiwa kwamba ni lazima kuthibitisha majina na sifa za Allaah kwa njia inayolingana na Allaah pamoja na kukanusha kufanana na viumbe. Amesema (Ta´ala):

لَيْسَ كَمِثْلِهِ شَيْءٌ ۖ وَهُوَ السَّمِيعُ الْبَصِيرُ

“Hakuna chochote kinachofanana Naye – Naye ni Mwenye kusikia, Mwenye kuona.”[16]

Amejikanushia Mwenyewe kufanana na vitu na akathibitisha kuwa ana usikizi na uoni. Ni dalili inayoonyesha kwamba kuthibitisha sifa hakupelekei ufanano. Vilevile ni wajibu kuthibitisha sifa pamoja na kukanusha ufanano. Hii ndio maana ya maneno ya Ahl-us-Sunnah wal-Jamaa´ah wanapozungumzia kukanusha na kuthibitisha katika majina na sifa:

“Kuthibitisha pasi na kufananisha na kumtakasa pasi na kukanusha.”

[1] 51:28

[2] 37:101

[3] 04:58

[4] 76:02

[5] 22:65

[6] 09:128

[7] 02:255

[8] 17:85

[9] 12:76

[10] 28:80

[11] 22:40

[12] 51:58

[13] 30:54

[14] 19:42

[15] 07:148

[16] 42:11

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: ´Aqiydat-ut-Tawhiyd, uk. 71-73
  • Imechapishwa: 05/03/2020