39. Kuimba nyimbo na kupiga dufu harusini

37- Nyimbo na kupiga dufu

Inajuzu kwa bwanaharusi kuwaacha wanawake harusini kutangaza ndoa kwa kupiga dufu na kuimba nyimbo zinazoruhusiwa ambazo hazina maelezo ya uzuri na maneno mabaya. Juu ya hilo kuna Hadiyth zifuatazo:

1- ar-Rabiy´ bint Mu´awwidh (Radhiya Allaahu ´anhaa) amesimulia akisema: “Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alikuja na kuingia nyumbani kwangu wakati ´Aliy alipomaliza kuoa na kutenda tendo la ndoa, akakaa karibu na mimi kama jinsi wewe ulivyokaa karibu na wewe (akimweleza yule anayemsimulia Hadiyth). Vijakazi wetu wakaanza kupiga dufu na kuimba kwa kuwasifu wale baba zao waliouawa siku ya Badr.” Mmoja wao akasema:

وفينا نبي يعلم ما في غد

“Kati yetu yuko Mtume ambaye anayajua yatayopitika kesho.”

Akasema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Acheni kusema hivo na semeni vile mlivokuwa mkisema.”[1]

2- ´Aaishah (Radhiya Allaahu ´anhaa) amesimulia ya kwamba alimsindikiza mwanamke kwa mwanaume mmoja katika Answaar siku ya harusi. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akasema:

“Ee ´Aaishah! Je, hamkuwa na burudani yoyote? Kwani hakika Answaar wanapenda burudani.””[2]

Katika upokezi mwingine imekuja ya kwamba (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alisema:

“Je, ulimpeleka pamoja naye kijakazi ambaye atampigia dufu na kumuimbia?” ´Aaishah akasema: “Aseme nini?” Akasema (´alayhis-Salaam): “Aseme:

أتيناكم أتيناكم … فحيونا نحييكم

Tumekujieni… tumekujieni…

لولا الذهب الأحم … ر ما حلت بواديكم

Ingelikuwa sio dhahabu nyekundu… asingelitwaa kwenye bonde lenu…

لولا الحنطة السمرا … ء ما سمنت عذاريكم

Ingelikuwa sio mtama wa dhahabu… wasingelinenepa wanawari wenu[3].

3- ´Aaishah (Radhiya Allaahu ´anhaa) amesimulia tena ya kwamba Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) aliwasikia watu wakiimba harusini wakisema:

وأهدي لها أكبش … يبحبحن في المربد

Nitampa kondoo wake… akichachawa

وحبك في النادي … ويعلم ما في غد

Na mapenzi yako katika klabu… na anajua yaliyoko kesho

Katika upokezi mwingine imekuja:

وزوجك في النادي … ويعلم ما في غد

Mume wako yuko klabuni… anajua yaliyoko kesho

Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akasema: “Hakuna anayejua yaliyoko kesho isipokuwa Allaah (Subhaanah).”[4]

4- ´Aamir bin Sa´d al-Bajaliy amesimulia akisema: “Niliingia kwa Qaradhwah bin Ka´b, Abu Mas´uud (na akamtaja mwingine watatu ambaye kanitoka) ambapo nikawaona wajakazi wakipiga dufu na wakiimba. Hivi mnakubaliana na mambo kama haya ilihali nyinyi ni Maswahabah wa Muhammad (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam)?” Wakasema: “Alitupa ruhusa ya kufanya hivo kwenye sherehe za harusi na wakati wa maombolezo ya msiba.”

Katika upokezi mwingine imekuja:

“… na katika kumlilia maiti pasi na kuomboleza.”[5]

5- Abu Balaj Yahyaa bin Saliym amesema: “Nilimwambia Muhammad bin Haatwib: “Nimeoa wanawake wawili na hakukuwa sauti ya dufu katika [harusi] yoyote katika wao.” Muhamamd (Radhiya Allaahu ´anh) akasema: “Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Kinachopambanua yaliyo kati ya halali na haramu ni sauti ya dufu.”[6]

6- Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Itangazeni ndoa.”[7]

[1] Ameipokea al-Bukhaariy (02/352), (09/166-167), al-Bayhaqiy (07/288-289), Ahmad (06/359-360) na al-Muhaamiliy katika “Swalaat-ul-´Iydayn” (139) na wengineo.

[2] Ameipokea al-Bukhaariy (09/184-185), al-Haakim (02/184), al-Bayhaqiy amepokea kutoka kwake (07/288).

[3] Ameipokea at-Twabaraaniy kama ilivyo katika “az-Zawaa-id” (01/167/01) na katika “al-Fath” amenyamaziwa. Ndani yake kuna udhaifu. Lakini baadaye nimekuja kupata njia nyingine kupitia kwa ´Aaishah inayoipa nguvu kama nilivyobainisha katika “al-Irwaa´” (1995).

[4] Ameipokea at-Twabaraaniy katika “as-Swaghiyr”, uk. 69 kwa nambari 830 kwa mpangilio, al-Haakim (02/184-185), al-Bayhaqiy (07/289). al-Haakim amesema:

“Ni Swahiyh kwa masharti ya Muslim” na adh-Dhahabiy akaafikiana naye.

[5]  Ameipokea al-Haakim, al-Bayhaqiy na siyaaq na upokezi mwingine ni wake, an-Nasaa´iy (02/93), at-Twayaalisiy (1221).

[6] an-Nasaa´iy (02/91), at-Tirmidhiy (02/170) ambaye amesema kuwa ni Hadiyth ni nzuri, Ibn Maajah na wengineo, al-Haakim na siyaaq ni yake, al-Bayhaqiy (07/289), Ahmad (03/418), Abu ´Aliy at-Twuusiy katika “al-Mukhtaswar”, al-Haakim (01/109-110). al-Haakim amesema:

“Mlolongo wa wapokezi wake ni Swahiyh” na adh-Dhahabiy akaafikiana naye.

Mimi naonelea kuwa mlolongo wa wapokezi wake ni mzuri. Nimebainisha hilo katika “al-Irwaa´” (1994).

[7] Ameipokea Ibn Hibbaan (1285), at-Twabaraaniy (01/01/69).

  • Mhusika: Imaam Muhammad Naaswir-ud-Diyn al-Albaaniy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Aadaab-uz-Zafaaf, uk. 179-183
  • Imechapishwa: 27/03/2018