Jumla ya waliohudhuria katika vita vya Badr ilikuwa waislamu 310; 86 katika Muhaajiruun, 61 katika al-Aws na 170 katika al-Khazraj. Idadi chache ya al-Aws ukilinganisha na al-Khazraj (pamoja na kwamba wao walikuwa na nguvu na wenye subira zaidi katika vita) ni kwa sababu walikuwa wakiishi sehemu ya juu ya al-Madiynah. Wakati ilipofikia wakati wa kutoka ilikuwa wepesi kwa al-Khazraj kutoka kwa sababu ya kuishi kwao karibu.

Wanahistoria wametofautiana sana juu ya idadi ya wanajeshi walioshiriki katika vita vya Badr na majina ya baadhi yao. az-Zuhriy, Muua bin ´Uqbah, Muhammad bin Ishaaq bin Yasaar, Muhammad bin ´Umar al-Waaqidiy, Sa´iyd bin Yahyaa al-Umawiy katika ”al-Maghaaziy”, al-Bukhaariy na wanachuoni wengine wa kale wamewataja. Ibn Hazm amewataja kwa mpangilio kama nilivyofanya katika kitabu chake cha “as-Siyrah”. Amedai kwamba nane katika wao hawakushiriki nafsi zao katika vita vya Badr na kwamba walipata tu fungu lao kutoka kwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Aliwataja baadhi yao ´Uthmaan, Twalhah na Sa´iyd bin Zayd. Miongoni mwa wanachuoni waliokuja nyuma ambao wameyazungumzia maudhui haya kwa uzuri ni Shaykh, Imaam na Haafidhw Dhwiyaa’-ud-Diyn Abu ´Abdillaah Muhammad bin ´Abdil-Waahid al-Maqdisiy (Rahimahu Allaah). Ameyafanyia kitabu maalum na ameyaingiza vilevile katika kitabu chake “al-Ahkaam”.

Kuhusiana na washirikina walikuwa, kama alivosema Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam), kati ya 900 mpaka 100.

Siku hiyo waliuawa waislamu 14; sita kutoka katika Muhaajiruun, sita kutoka katika al-Khazraj na wawili kutoka katika al-Aws. Wa kwanza kuuawa alikuwa Mihjaa´, mtumwa wa ´Umar bin al-Khattwaab (Radhiya Allaahu ´anh) aliyeachwa huru. Kuna maoni vilevile yanayosema kwamba wa kwanza alikuwa ni Haarithah bin Sarraaqah.

Siku hiyo waliuawa washirikina 70. Kuna maoni mengine yanayosema walikuwa chini ya hapo. Walishikwa mateka idadi mfano wa hiyo.

Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alimaliza suala la Badr na mateka katika Shawwaal.

  • Mhusika: Imaam Ismaa´iyl bin Kathiyr ad-Dimashqiy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: al-Fusuwl fiy Siyrat-ir-Rasuwl, uk. 52-53
  • Imechapishwa: 10/10/2018