Shaykh-ul-Islaam Muhammad bin ´Abdil-Wahhaab (Rahimahu Allaah) amesema:

Ngazi ya pili ni Imani. Imegawanyika sehemu sabini na kitu. Ya juu yake ni neno “hapana mwenye haki ya kuabudiwa isipokuwa Allaah” na ya chini yake ni kuondosha kitu chenye kudhuru katika njia. Hayaa ni sehemu katika imani.

Nguzo zake ni sita: Kumuamini Allaah, Malaika Wake, Vitabu Vyake, Mitume Wake, kuamini siku ya Mwisho na uamini Qadar; kheri na shari yake.

Dalili ya nguzo hizi sita ni Kauli Yake (Ta´ala):

لَّيْسَ الْبِرَّ أَن تُوَلُّوا وُجُوهَكُمْ قِبَلَ الْمَشْرِقِ وَالْمَغْرِبِ وَلَـٰكِنَّ الْبِرَّ مَنْ آمَنَ بِاللَّـهِ وَالْيَوْمِ الْآخِرِ وَالْمَلَائِكَةِ وَالْكِتَابِ وَالنَّبِيِّينَ

“Si wema pekee kuelekeza nyuso zenu upande wa mashariki na magharibi, lakini wema wa kweli kabisa ni mwenye kuamini Allaah na siku ya Mwisho na Malaika na Kitabu na Manabii.” (al-Baqarah 02:177)

Dalili ya Qadar ni Kauli Yake (Ta´ala):

إِنَّا كُلَّ شَيْءٍ خَلَقْنَاهُ بِقَدَرٍ

”Hakika kila kitu Sisi Tumekiumba kwa makadirio.” (al-Qamar 54:49)

MAELEZO

Imani ni yale yaliyofungamana na moyo. Allaah anatakiwa kusadikishwa na kwamba Yeye ni Mola wa walimwengu ambaye ndiye ambaye anastahiki kuabudiwa. Malaika pia wanatakiwa kusadikishwa na vitabu, Mitume, kufufuliwa baada ya kufa, Pepo, Moto na Qadar, kheri na shari yake. Yote haya yamefungamana na moyo. Ni msingi mkubwa kabisa ambao ni lazima. Hakuna Uislamu pasi na imani na wala hakuna imani pasi na Uislamu. Ni lazima yapatikane yote mawili. Viungo vya mwili vya Uislamu ni lazima. Uislamu wa kwenye moyo na imani pia ni lazima. Kwa ajili hiyo Allaah amekusanya kati ya hivyo viwili katika Kitabu Chake kitukufu. Vivyo hivyo Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amevikusanya vyote viwili.

Uislamu ni kule kujisalimisha kwa nje ambako kunapelekea kuacha kumuasi Allaah na kuacha kumuasi. Imani inahusiana na yale matendo ya ndani yaliyofungamana na moyo na usadikishaji wake. Wakati mwingine imani huitwa Uislamu na Uislamu huitwa imani. Kunapotajwa imani peke yake huingia vyote viwili. Kunapotajwa Uislamu peke yake huingia vyote viwili. Amesema (Ta´ala):

إِنَّ الدِّينَ عِندَ اللَّـهِ الْإِسْلَامُ

”Hakika dini mbele ya Allaah ni Uislamu.” (03:19)

Unakusanya yale yaliyojificha na yale yenye kuonekana. Kadhalika pindi inapotajwa imani peke yake kunaingia vyote viwili. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema katika Hadiyth Swahiyh:

“Imani imegawanyika sehemu sabini na kitu. Ya juu yake ni neno “hapana mwenye haki ya kuabudiwa isipokuwa Allaah” na ya chini yake ni kuondosha kitu chenye kudhuru katika njia.”[1]

Imani hapa imekusanya vyote; nguzo za Uislamu na matendo mengine yote yenye kuonekana kama inavyokusanya pia yale yenye kufichikana. Kama ambavyo vilevile imekusanya Ihsaan.

[1] Muslim (35).

  • Mhusika: Imaam ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah bin Baaz
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh Thalaathat-il-Usuwl, uk. 42-44
  • Imechapishwa: 21/01/2017