37. Dalili kwamba mja anafanya au kuacha kwa kutaka kwake

Ahl-us-Sunnah wal-Jamaa´ah wanaamini kuwa Allaah ndiye anayeumba, anayeruzuku na anayeendesha mambo kama anavotaka na anavopenda na waja wana matakwa, wanapenda na wana khiyari. Wanafanya matendo kwa kutaka kwao na kupenda kwao. Kwa hiyo wana matakwa na utashi, si kama wanavosema Jahmiyyah na Jabriyyah. Lakini matakwa yao si yenye kujitegemea, kama wanavosema Mu´tazilah. Mfano wa hili ni katika maneno Yake (Ta´ala):

وَمَا تَشَاءُونَ إِلَّا أَن يَشَاءَ اللَّـهُ

“Hamtoweza kutaka isipokuwa atake Allaah.”[1]

Maneno Yake:

وَمَا تَشَاءُونَ

“Hamtoweza kutaka… “

Ni Radd kwa Jabriyyah ambao wanapinga matakwa ya mja. Maneno Yake:

إِلَّا أَن يَشَاءَ اللَّـهُ

“… isipokuwa atake Allaah.”

Ni Radd kwa Mu´tazilah Qadariyyah ambao wanapinga matakwa na utashi wa Allaah.

وَمَا تَشَاءُونَ إِلَّا أَن يَشَاءَ اللَّـهُ رَبُّ الْعَالَمِينَ

”Hamtotaka isipokuwa atake Allaah, Mola wa walimwengu.”[2]

وَمَا تَشَاءُونَ إِلَّا أَن يَشَاءَ اللَّـهُ ۚ إِنَّ اللَّـهَ كَانَ عَلِيمًا حَكِيمًا

“Hamtoweza kutaka isipokuwa atake Allaah, hakika Allaah ni Mjuzi wa yote, Mwenye hekima.”[3]

Kuadhibiwa na kulipwa thawabu kunatokana na matendo ya waja ambayo wameyafanya wenyewe kwa kutaka na kupenda kwao. Wanaadhibiwa kwa maasi kwa sababu wao ndio ambao wameyafanya mambo haya kwa kutaka kwao. Walikuwa na uwezo wa kuyaacha, kujiepusha nayo na kujitenga nayo mbali. Isitoshe wamekatazwa nayo. Wameyafanya kwa kutaka kwao wenyewe. Kwa hiyo wanaadhibiwa kwa hayo. Kwa ajili hiyo yule asiyekuwa na matakwa na utashi, kama mwendawazimu, mdogo na mwenye kulala, basi hachukuliwi hatua. Kwa sababu hana matakwa wana utashi. Kuhusu mwenye akili na ambaye kishabaleghe atachukuliwa hatua juu ya matendo yake. Kwa sababu ana uwezo wa kufanya na kuacha. Allaah amempa uwezo wa hili na lile; anaweza kwenda kuswali na wakati huohuo anaweza kwenda kuzini. Ana uwezo wa kufanya yote mawili. Akijizuia kutokamana na uzinzi na akaenda kuswali basi Allaah (´Azza wa Jall) atamlipa thawabu. Akipinduka na akaenda kuzini na akaacha kuswali Allaah atamuadhibu juu ya matendo yake na matakwa yake. Maneno yake:

“Hakuna kitu ulimwenguni kinachotoka nje ya makadirio Yake… “

Yote haya ni Radd kwa Mu´tazilah Qadariyyah. Maneno yake:

“… wala hakitoki isipokuwa kutokana na makadirio Yake.”

Amesema (Ta´ala):

فَعَّالٌ لِّمَا يُرِيدُ

“Mwingi wa kufanya Atakalo.”[4]

إِنَّ اللَّـهَ يَفْعَلُ مَا يَشَاءُ

“Hakika Allaah anafanya atakavyo.”[5]

كَذَٰلِكَ اللَّـهُ يَفْعَلُ مَا يَشَاءُ

“Hivo ndivyo Allaah hufanya atakavyo.”[6]

[1] 76:30

[2] 81:29

[3] 76:30

[4] 85:16

[5] 22:18

[6] 03:40

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh ´Aqiydat-il-Imaam Mujaddid Muhammad bin ´Abdil-Wahhaab, uk. 57-58
  • Imechapishwa: 18/03/2021