35. Haifai kuhudhuria mwaliko ambao ndani yake kuna maasi

33- Kuacha kuhudhuria mwaliko ambao ndani yake kuna maasi

Haijuzu kuhudhuria mwaliko ikiwa ndani yake kuna maasi. Isipokuwa ikiwa kama mtu amekusudia kuyakemea au kujaribu kuyaondosha. Akiyaondosha ni sawa. Vinginevyo itawajibika kurudi. Kumepokelewa juu ya hilo Hadiyth:

1- ´Aliy amesimulia akisema:

“Nilifanya chakula ambapo nikamwalika Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Alikuja na kuona mapicha ambapo akarejea. Nikasema: “Ee Mtume wa Allaah! Ni kipi kilichokurudisha, baba yangu na mama yangu wawe fidia yako?” Akasema: “Hakika kwenye nyumba kuna mapicha na Malaika hawaingii nyumba iliyo na mapicha.”[1]

2- ´Aaishah anasimulia ya kwamba alinunua mito iliyokuwa na picha. Wakati Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alipoiona alisimama mlangoni na wala hakuingia. Nikatambua usoni mwake kuchukia ambapo nikasema: “Ee Mtume wa Allaah! Natubia kwa Allaah na kwa Mtume Wake, nimefanya nini?” Akasema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam): “Vipi kuhusu mto huu?” Nikasema: “Nimekununulia ili uweze kuukalia na kuutumia kama mto.” Akasema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallaam): “Hakika watu wa picha hizi.. “

Katika upokezi mwingine imekuja:

“Hakika wale wanaotengeneza picha hizi wataadhibiwa siku ya Qiyaamah na wataambiwa: “Vipeni uhai vile mlivyoumba na nyumba ambayo kuna mfano wa picha kama hizi hawaingii Malaika.” Basi hakuingia mpaka nilipoiondosha.”

3- Amesema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Yule mwenye kumuamini Allaah na siku ya Mwisho, basi asiketi kwenye meza kunakohudumiwa pombe.”[2]

Matendo ya as-Salaf as-Swaalih (Radhiya Allaahu ´anhum) yalikuwa hivi tulivyoelezea. Mifano ya hilo ni mingi. Nitafupika kwa yale ninayoikumbuka hivi sasa ikiwa ni pamoja na ifuatayo:

Mosi: Aslam – ambaye ni mtumwa aliyeachwa huru na ´Umar bin al-Khattwaab (Radhiya Allaahu ´anh) – amesimulia ya kwamba wakati alipofika Shaam mtu mmoja katika manaswara alimtengenezea chakula na akamwambia ´Umar: “Mimi nitapenda mkija kwangu na kunipa heshima wewe na wenzako – mtu huyu alikuwa ni kiongozi katika wakuu wa Shaam. ´Umar akamwambia: “Sisi hatuingii makanisa yenu kwa ajili ya picha zilizomo ndani yake.”[3]

Pili: Ibn Mas´uud – ´Uqbah bin ´Amr – amesimulia ya kwamba kuna mtu alimtengenezea chakula kisha akamwalika. Akamwambia: “Je, nyumbani kwako kuna picha?” Akajibu: “Ndio.” Akakataa kuingia mpaka kwanza avunje picha hiyo ndio akaingia.”[4]

Tatu: Imaam al-Awzaa´iy amesema:

“Hatuingii katika karamu ya ndoa ambapo kuna matari au ala za muziki.”[5]

[1] Ameipokea Ibn Maajah (02/323), Abu Ya´laa katika “al-Musnad” (01/31), (01/37) na (02/39). Ziada ni yake na mlolongo wa wapokezi wake ni Swahiyh.

[2] Ameipokea al-Haakim katika (04/288) na matamshi ni yake, at-Tirmidhiy na sehemu yake nyingine ni an-Nasaa´iy, Ahmad (03/339), al-Jurjaaniy (150) kupitia njia zengine. Abu az-Zubayr amepokea kutoka kwa Jaabir. al-Haakim amesema: “Ni Swahiyh juu ya masharti ya Muslim.” adh-Dhahabiy ameafikiana naye na at-Tirmidhiy amesema: “Ni Hadiyth nzuri.” Ina shawahidi nyingi ambazo unaweza kuziona katika at-Targhiyb wat-Tarhiyb (01-89-91).

[3] Ameipokea al-Bayhaqiy kwa mlolongo wa wapokezi Swahiyh.

Tambua ya kwamba katika maneno ya ´Umar kuna dalili ya wazi juu ya kosa linalofanywa na baadhi ya Mashaykh ambao wanahudhuria makabisa ambayo yamejaa picha na masanamu. Wanafanya hivo kwa kuitikia matakwa ya baadhi ya wahusika au wengineo. Laiti mambo yangelikomea hapo! Lakini kwa masikitiko makubwa ni kwamba wanasikia maneno ya kufuru na upotevu kutoka kwa baadhi ya wale wanaozungumza hapo ndani – na huenda wakawa waislamu – halafu wananyamaza na hawazungumzi kitu na wala hawadhihirishi hukumu ya Kishari´ah katika hilo ilihali wanatambua. Tahamaki unawasikia wanasema kuwa eti hakuna tofauti kati ya Uislamu na ukristo na kwamba dini ni ya Allaah na nchi ni ya wote. Sivyo tu bali wanawahukumia wengine wasiokuwa waislamu shahaadah pamoja na kujua kwao ya kwamba muislamu mwenyewe haitakiwi kumhukumia shahaadah isipokuwa kwa masharti yanayotambulika kwao na mikhalafa mingineyo. Hakika sisi ni wa Allaah na Kwake ndiko tutakorejea.

[4] Ameipokea al-Bayhaqiy pia na mlolongo wa wapokezi wake ni Swahiyh kama alivyosema al-Haafidhw katika “al-Fath” (09/204). Abu Bakr bin al-Marwaziy ameiwekea taaliki katika kitabu “al-Wara´” (01/20).

[5] Ameipokea Abul-Hasan al-Harbiy katika “al-Fawaa-id al-Muntaqaah” (04/03/01) kwa mlolongo wa wapokezi Swahiyh kutoka kwake.

  • Mhusika: Imaam Muhammad Naaswir-ud-Diyn al-Albaaniy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Aadaab-uz-Zafaaf, uk. 162-166
  • Imechapishwa: 24/03/2018