35. Allaah hana mtoto wala wazazi

Amesema (Jalla wa ´Alaa):

لَمْ يَلِدْ وَلَمْ يُولَدْ

“Hakuzaa na wala hakuzaliwa.”[1]

Hana mwanzo wala mwisho. Hakuna kiumbe yeyote anayefanana Naye. Kwa sababu mtoto hufanana na wazazi wake na ni sehemu katika wao. Amesema (Ta´ala):

وَجَعَلُوا لَهُ مِنْ عِبَادِهِ جُزْءًا

“Wakamfanyia kati ya waja Wake sehemu.”[2]

Bi maana mwana. Mtoto ni sehemu ya mzazi. Hapa wanarudiwa manaswara ambao wamedai kuwa al-Masiyh ni mwana wa Allaah – Allaah ametakasika kutokamana na yale wanayoyasema! Wanaraddiwa vilevile washirikina wa kiarabu ambao walikuwa wakidai kuwa Malaika ni wasichana wa Allaah. Wale wanaosema kuwa Allaah ana mtoto ni watu aina mbili:

1 – Manaswara wenye kusema kuwa Anaye mtoto wa kiume.

2 – Washirikina wenye kusema kuwa Anaye wasichana.

Allaah (Jalla wa ´Alaa) wamewarudi wote wawili na kusema:

لَمْ يَلِدْ وَلَمْ يُولَدْ

“Hakuzaa na wala hakuzaliwa.”

Allaah hana mtoto. Hana haja ya mtoto. Mtoto hufanana na wazazi na ni sehemu kutoka kwao. Allaah hana sehemu kutoka kwa viumbe Wake. Allaah ametakasika kutokamana na jambo kama hilo! Jengine ni kwamba mtoto ni mwenye kushirikiana na mzazi – na Allaah hana mshirika kwa njia zote. Kwa hivyo ametakasika kutokamana na wazazi na mwana.

[1] 112:03

[2] 43:15

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Bayaan-ul-Ma´aaniy fiy Sharh Muqaddimati Ibn Abiy Zayd al-Qayrawaaniy, uk. 31-32
  • Imechapishwa: 19/07/2021