Utata wa watu hawa ni kile kisomo cha Salaf wengi; wanaposimama katika:

إِلاَّ اللّهُ

“… isipokuwa Allaah.”[1]

kwenye Aayah:

فَأَمَّا الَّذِينَ في قُلُوبِهِمْ زَيْغٌ فَيَتَّبِعُونَ مَا تَشَابَهَ مِنْهُ ابْتِغَاء الْفِتْنَةِ وَابْتِغَاء تَأْوِيلِهِ وَمَا يَعْلَمُ تَأْوِيلَهُ إِلاَّ اللّهُ وَالرَّاسِخُونَ فِي الْعِلْمِ يَقُولُونَ آمَنَّا بِهِ كُلٌّ مِّنْ عِندِ رَبِّنَا

“Basi wale ambao katika nyoyo zao mna upotovu hufuata zile zenye kutatiza kwa kutafuta fitina na kutafuta tafsiri zake [zinazoendana na wao] – na hakuna ajuaye tafsiri zake isipokuwa Allaah na wale wenye msingi madhubuti katika elimu husema: “Tumeziamini; zote zinatoka kwa Mola wetu.”[2]

Wamejenga utata wao juu ya misingi miwili:

1- Aayah zinazozungumzia sifa ni zenye kutatiza.

2- Tafsiri iliyotajwa katika Aayah ni kulifasiri andiko kidhahiri na kwenda katika maana inayoenda kinyume na udhahiri huo. Natija inayopatikana ni kuwa Aayah zinazozungumzia sifa zinakuwa na maana inayoenda kinyume na ile ya dhahiri na hakuna aijuaye isipokuwa Allaah pekee. Wanaraddiwa ifuatavyo:

1- Nini wanachomaanisha wanaposema kuwa ni zenye kutatiza? Wanamaanisha kuwa maana ndio yenye kutatiza au uhakika wake?

Ikiwa wanamaanisha hilo la kwanza, na ndivyo ilivyo, basi Aayah zinazozungumzia sifa sio zenye kutatiza kwa sababu maana yake iko wazi.

Ikiwa wanakusudia hilo la pili, basi ni kweli Aayah zinazozungumzia sifa ni zenye kutatiza. Kwa sababu hakuna yeyote anayejua uhakika wa sifa na namna yake zaidi ya Allaah. Kwa hivyo tunapata kujua kuwa sio sahihi kusema hali ya kutofungamanisha kuwa Aayah zinazozungumzia sifa ni zenye kutatiza bila ya kufafanua suala hili.

2- Maneno yao “Tafsiri iliyotajwa katika Aayah ni kulifasiri andiko kulitoa nje ya udhahiri wake na kwenda katika maana inayoenda kinyume na udhahiri huo” sio sahihi. Maana hii imezushwa na haijulikani na waarabu na Maswahabah ambao Quraan imeteremshwa kwa lugha yao. Maana wanazozitambua ni zifuatazo:

1- Ina maana ya tafsiri. Katika hali hii wanachuoni wanajua tafsiri yake. Ibn ´Abbaas amesema:

“Mimi ni mmoja katika wale waliobobea kabisa katika elimu ambao wanajua tafsiri yake.”[3]

Kutokana na tafsiri hii wengi katika Salaf wamesimama wanapofika katika maneno ya Allaah (Ta´ala):

وَمَا يَعْلَمُ تَأْوِيلَهُ إِلاَّ اللّهُ وَالرَّاسِخُونَ

“Hakuna ajuaye tafsiri zake isipokuwa Allaah na wale wenye msingi madhubuti katika elimu… “

2- Ina maana ya uhakika wa jambo na mwisho wake. Katika hali hii hatujui tafsiri ya yale Allaah aliyojielezea Mwenyewe na Qiyaamah. Mfano wa hilo ni yale aliyosema Maalik na wengine juu ya kulingana na mengineyo. Kujengea juu ya hilo wengi katika Salaf wamesimama wanapofika katika maneno ya Allaah (Ta´ala):

وَمَا يَعْلَمُ تَأْوِيلَهُ إِلاَّ اللّهُ

“… hakuna ajuaye tafsiri zake isipokuwa Allaah.”

3- Allaah ameiteremsha Qur-aan ili tuizingatie. Ametuhimiza kuizingatia yote. Aayah zinazozungumzia sifa hazikuvuliwa. Yale masisitizo ya kuizingatia ina maana kwamba kuna uwezekano mtu akaelewa maana yake. Vinginevyo kusingekuwa na maana yoyoye ya kusisitizwa kuzingatia maana yake. Kusisitiza juu ya jambo ambalo mtu hawezi kulifikia ni upuuzi, jambo ambalo haliwezekani likawepo katika maneno ya Allaah na ya Mtume Wake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Masisitizo ya kuizingatia Qur-aan yote ina maana kwamba mtu anaweza kuzifahamu zile Aayah zinazozungumzia sifa endapo mtu atazingatia. Mtu ambaye yuko karibu zaidi ya kulielewa hilo ni Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na Maswahabah zake. Kwa sababu Qur-aan imeteremshwa kwa lugha yao na ni watu wenye kujisalimisha kwa haraka inapokuja katika kuizingatia Qur-aan na khaswa katika mambo ya dini ambayo ni muhimu zaidi. Abu ´Abdir-Rahmaan as-Sulamiy amesema:

“Wale ambao walikuwa wakitusomesha Qur-aan – ´Uthmaan bin ´Affaan, ´Abdullaah bin Mas´uud na wengineo – wametueleza kwamba: “Baada ya kuhifadhi Aayah kumi kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam), tulikuwa hatuzivuki mpaka tujifunze elimu yazo na kuzitendea kazi.” Tukajifunza Qur-aan, elimu na matendo.”

Vipi basi watakuwa ni wajinga juu ya Aayah zinazozungumzia sifa wakati ndio jambo muhimu zaidi katika dini?

4- Maoni yao yanalazimisha ya kwamba Allaah ameteremsha katika Kitabu Chake matamshi yasiyokuwa na maana yoyote yasiyobainisha haki. Kwa mujibu wa maoni yao yanapelekea kwamba sentesi hizi ni sawa na herufi za kialfabeti na si jengine. Hili linapingana na hekima ya Allaah ya kuteremsha Vitabu na kuwatuma Mitume.

[1] 03:07

[2] 03:07

[3]Tafsiyr al-Qur-aan al-´Adhwiym (1/348) ya Ibn Kathiyr.

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Fath Rabb-il-Bariyyah, uk. 81-83
  • Imechapishwa: 11/05/2020