Swali: Katika mji wetu kuna msikiti ambao kuna kaburi ndani yake. Je, swalah inafaa katika msikiti huu pamoja na kuzingatia ya kwamba kilichotangulia kujengwa ni msikiti au kaburi? Pamoja na kuzingatia kwamba kuna watu wengi wanaokuja kutoka katika miji yao kwa ajili ya kulitembelea kaburi hili, kulichinjia na kuweka pesa ndani yake.

Jibu: Misikiti ambayo iko na makaburi hakuswaliwi ndani yake. Ni lazima kuyachimbua makaburi hayo na kuyaweka mbali na makaburi yanayotambulika na kusibaki ndani yake kaburi. Ni mamoja kaburi la walii au mwengine. Si yule anayeitwa walii au mwengine. Bali ni lazima kulifukua na kuliweka mbali na makaburi ya watu wote. Haijuzu kuyachinjia makaburi, kuyaletea pesa wala kuyawekea nadhiri. Bali mambo haya ni katika shirki kubwa. Ni lazima kuyafukua makaburi katika misikiti na kuhamisha mabaki yake kwenda katika makaburi ya umma ndani ya shimo lake maalum. Kila kaburi liwe ndani ya shimo lake maalum kama makaburi mengine. Kuhusu misikiti haijuzu kuweka ndani yake makaburi. Kwa sababu Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amekataza jambo hilo na akatahadharisha. Amewasema vibaya mayahudi na manaswara kwa kufanya hivo. Imethibiti kutoka kwake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ya kwamba amesema:

”Allaah awalaani mayahudi na manaswara. Wameyafanya makaburi ya Mitume wao kuwa ni mahali pa kuswalia.”

Amesema (Radhiya Allaahu ´anhaa):

“Anatahadharisha waliyoyafanya.”

Kuna maafikiano juu yake[1].

Vilevile amesema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) wakati Umm Salamah na Umm Habiybah (Radhiya Allaahu ´anhumaa) walipomwambia kuhusu kanisa lililokuwa na mapicha na wakamsifia lilikuwa na kadhaa na kadhaa ambapo akasema:

“Hao ndio wale ambao wanapofiwa na mtu mwema, basi hujenga juu ya kaburi lake msikiti na huchora ndani yake picha hiyo. Hao ndio viumbe waovu kabisa mbele ya Allaah.”[2]

Akaeleza kwamba wale wanaojenga misikiti juu ya makaburi ndio viumbe waovu kabisa.

Amesema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) tena:

“Tanabahini! Hakika wale waliokuwa kabla yenu walikuwa wakiyafanya makaburi ya Mitume wao kuwa mahali pa kuswalia. Tanabahini! Msiyafanye makaburi kuwa mahali pa kuswalia. Hakika mimi nawakatazeni na hilo.”[3]

Amekataza (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kujenga makaburi juu ya misikiti.

Ni jambo linalotambulika kwamba anayeswali kwenye kaburi basi amelifanya kuwa msikiti. Vilevile ambaye amejenga ili kuswaliwe ndani yake basi ameufanya kuwa msikiti.

Kwa hivyo ni lazima kuyaweka makaburi mbali na misikiti na kusiwekwi ndani yake makaburi kwa ajili ya kutekeleza amri ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na pia kutahadhari na laana yenye kutoka kwa Mola wetu kwa ambaye amejenga juu ya makaburi. Amesema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

”Allaah awalaani mayahudi na manaswara. Wameyafanya makaburi ya Mitume wao kuwa ni mahali pa kuswalia.”

Hivyo ikatambulika kwa jambo hilo ya kwamba haijuzu kuyafanya kuwa ni mahali pa kuswalia. Bali ni lazima makaburi yawe kando na misikiti iwe kando. Makaburi yawe kando na kusijengwe juu yake misikiti. Misikiti iwe mbali na makaburi na kusiwe ndani yake makaburi. Bali yawe yenye kusalimika kutokamana na hayo. Kukiwepo ndani ya msikiti kaburi basi kusiswaliwe ndani yake kwa ajili ya kutahadhari na laana hii na kutahadhari na njia zinazopelekea katika shirki. Kwa sababu mtu akiswali katika msikiti huu basi pengine shaytwaan akampambia kumwomba maiti huyu, kumwomba uokozi, kumswalia au kumsujudia maiti huyu na matokeo yake akatumbukia katika shirki kubwa. Jengine ni kwamba haya ni miongoni mwa matendo ya mayahudi na manaswara na hivyo ni lazima kwenda kinyume na, kujiweka mbali na mwenendo wao na kutokamana na matendo yao maovu.

Lakini ikitambulika kuwa msikiti ulijengwa juu ya kaburi basi ni lazima kuubomoa msikiti. Ikiwa makaburi ndio yalitangulia kisha baadaye ikajengewe, basi ni lazima kuubomoa msikiti. Lakini ikiwa haijulikani basi yafukuliwe makaburi na yatawekwa mbali kwenye makaburini na msikiti utabaki na kutaswaliwa. Kwa sababu kimsingi ni kuwepo misikiti kabla ya makaburi.

[1] al-Bukhaariy (436) na Muslim (529).

[2] al-Bukhaariy (427) na Muslim (528).

[3] Muslim (532).

  • Mhusika: Imaam ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah bin Baaz
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: at-Tahdhiyr min Fitnat-il-Qubuur, uk. 118-120
  • Imechapishwa: 18/07/2022