32. Kufuatafuata athari za Mitume na kujenga juu yake msikiti

Swali: Je, ni bora kujenga msikiti yale maeneo ambayo aliswali Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) au yabaki kama yalivyo au kuyatengenezea bustani za umma?

Jibu: Haijuzu kwa muislamu kufautafuata zile athari za Mitume kwa ajili ya kuswali au kujenga juu yake msikiti. Kufanya hivo ni miongoni mwa zile njia zinazopelekea katika shirki. Kwa ajili hii ´Umar (Radhiya Allaahu ´anh) alikuwa akiwakataza watu kutokamana na jambo hilo na akisema:

“Hakika si venginevyo waliangamia wale waliokuwa kabla yenu kwa sababu ya kufuatafuata athari za Mitume yao.”[1]

Alikata (Radhiya Allaahu ´anh) mti uliokuwa Hudaybiyah ambao Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alipewa kiapo chini yake wakati alipowaona baadhi ya watu wanaenda huko na kuswali chini yake. Alifanya hivo kwa ajili ya kufunga njia za shirki na kuutahadharisha Ummah kutokamana na Bid´ah. Alikuwa (Radhiya Allaahu ´anh) mwenye hekima katika matendo yake na maisha yake na mwenye kupupia juu ya kufunga njia zinazopelekea katika shirki na sababu zake. Allaah amjaze kheri juu ya Ummah wa Muhammad. Kwa ajili hiyo Maswahabah (Radhiya Allaahu ´anhum) hawakujenga msikiti juu ya athari zake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) katika njia ya kuelekea Makkah na Tabuuk kwa sababu ya kujua kwao kuwa jambo hilo linaenda kinyume na Shari´ah Yake na jambo hilo linasababisha kutumbukia ndani ya shirki kubwa. Isitoshe ni miongoni mwa Bid´ah ambazo amezitahadharisha (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) pale aliposema:

“Yeyote atakayezua kitendo kisichokuwa katika amri yetu atarudishiwa mwenyewe.”[2]

Kuna maafikiano juu ya usahihi wake kupitia kwa ´Aaishah (Radhiya Allaahu ´anhaa).

Vilevile amesema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Yeyote atakayefanya kitendo kisichoafikiana na amri yetu atarudishiwa mwenyewe.”[3]

Ameipokea Muslim katika “as-Swahiyh” yake.

Alikuwa (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akisema katika Khutbah ya ijumaa:

“Amma ba´d: Hakika mazungumzo bora ni Kitabu cha Allaah na uongofu bora ni uongofu wa Muhammad (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Uovu wa mambo ni yale yaliyozuliwa na kila Bid´ah ni upotevu.”[4]

Ameipokea Muslim katika “as-Swahiyh” yake.

Zipo Hadiyth nyingi zenye maana kama hii.

[1] Mukhtaswar-ul-Mukhtaswar (01/26).

[2] al-Bukhaariy (2697) na Muslim (1718).

[3] Muslim (1718).

[4] Muslim (867).

  • Mhusika: Imaam ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah bin Baaz
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: at-Tahdhiyr min Fitnat-il-Qubuur, uk. 116-117
  • Imechapishwa: 18/07/2022