32. Sura ya tano: Ubainifu wa ufahamu wa kimakosa katika kuiwekea kikomo ´ibaadah

5- ´Ibaadah ni kukomeka (Tawqiyfiyyah). Kwa maana kwamba hakusuniwi kitu isipokuwa kwa dalili kutoka katika Qur-aan na Sunnah. Kitu ambacho hakukuwekwa katika Shari´ah kinazingatiwa kuwa ni Bid´ah yenye kurudishwa. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Mwenye kufanya kitendo kisichoafikiana na amri yetu basi atarudishiwa mwenyewe.”[1]

Bi maana kitendo hicho atarudishiwa mwenyewe na hakitokubaliwa. Bali anapata madhambi. Kwa sababu ni maasi na sio utiifu. Isitoshe, mfumo uliosalimika katika kutekeleza ´ibaadah zilizowekwa katika Shari´ah ni ukati na kati baina ya uwepesishaji na uzembeaji na baina ya ususuwavu na uchupaji mipaka. Amesema (Ta´ala) kumwambia Mtume Wake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

فَاسْتَقِمْ كَمَا أُمِرْتَ وَمَن تَابَ مَعَكَ وَلَا تَطْغَوْا

“Basi kuwa na msimamo imara kama ulivyoamrishwa na aliyetubia pamoja nawe na wala usivuke mpaka.”[2]

Aayah hii tukufu inapiga msitari wa mbingu salama katika kufanya ´ibaadah.  Hayo yanapatikana kwa kunyooka wakati wa kuyatenda kwa njia ya ukati na kati isiyokuwa ndani yake na uchupaji mipaka wala uzembeaji. Bali inakuwa kwa mujibu wa Shari´ah kama ulivyoamrishwa. Kisha akakazia kwa kusema:

وَلَا تَطْغَوْا

“… na wala usivuke mpaka.”

Twughyaan ni kuvuka mpaka kwa ususuwavu na ugumu. Kwa msemo mwingine ni kuchupa mipaka. Wakati (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alipojua kuwa Maswahabah watatu waliyadogesha matendo yake kwa vile mmoja wao alisema: “Mimi nitafunga na sintokula”, mwengine akasema: “Mimi nitaswali na sintopumzika” na watatu akasema: “Mimi sintooa wanawake.” Akasema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Lakini mimi mara nafunga na nafungua na naoa wanawake. Atakayeipa mgongo Sunnah yangu basi si katika mimi.”[3]

Hii leo kuna makundi mawili yenye kujigonga kuhusiana na suala la ´ibaadah:

Kundi la kwanza: Wamefanya upungufu katika ufahamu wa ´ibaadah na wakachukulia sahali katika kuitekeleza kiasi cha kwamba wakaharibu katika aina zake nyingi. Isitoshe wamezipufisha katika matendo maalum na nembo ndogo zinazofanywa msikitini peke yake. Wanaona kuwa hakuna nafasi ya ´ibaadah nyumbani, ofisini, dukani,  barabarani,  biashara, siasa, hukumu wakati wa magomvi wala kwenginepo katika mambo mbalimbali ya kimaisha. Ni kweli kwamba bora ni msikitini na ndipo kunaposwaliwa ndani yake vipindi vya swalah tano. Lakini ´ibaadah imekusanya maisha yote ya muislamu; ndani ya msikiti na nje yake.

Kundi la pili: Wamefanya ususuwavu katika kuzitendea kazi ´ibaadah kwenda katika kiwango cha uchupaji mipaka kiasi cha kwamba wakayanyanyua mambo yaliyopendekezwa mpaka katika ngazi ya ulazima, wakaharamisha baadhi ya mambo yaliyo ya halali, wakamuhumu upotevu au kumtia makosani yule mwenye kwenda kinyume na mfumo wake na wakakosea ufahamu wake. Uongofu bora ni uongofu wa Muhammad (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na uovu wa mambo ni yale yaliyozuliwa.

[1] Muslim (4468).

[2] 11:112

[3] al-Bukhaariy (5063) na Muslim (3389).

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: ´Aqiydat-ut-Tawhiyd, uk. 58-59
  • Imechapishwa: 27/02/2020