32. Mwenye busara na kuwatembelea ndugu

1- Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Kuna mtu alimtembelea ndugu yake katika kijiji. Allaah akamtuma Malaika kwenda kusimama kwenye daraja na kumsubiri njiani. Akamuuliza: “Unaenda wapi?” Mtu yule akasema: “Kwa ndugu yangu anayeishi katika kijiji hiki.” Malaka yule akamwambia: “Kuna kitu chochote unachomtafutia?” Mtu yule akasema: “Hapana. Isipokuwa tu mimi nampenda kwa ajili ya Allaah.” Ndipo akasema: “Mimi ni mjumbe wa Allaah. Allaah (Tabaarak wa Ta´ala) anakupenda kama unavompenda.”

2- Ni wajibu kwa mwenye busara kuwatembelea ndugu zake na kuwajulia hali. Pindi yule mwenye kuwatembelea anakusudia matembezi basi anapata mambo mawili:

1- Thawabu huko Aakhirah.

2- Kufurahi kwa kutangamana na mtu yule.

3- ´Abdullaah bin Rajaa´ al-Ghadaaniy amesema:

“´Utbah al-Ghulaam alikuwa akibaki kwenye makaburi na nje jangwani kisha anatoka katika miji na kuishi huko. Inapofika siku ya ijumaa anaingia Baswrah, anaswali swalah ya ijumaa, anawaona ndugu zake na kuwasilimia.”

4- al-Firyaabiy amesema:

“Alinijia mimi Wakiy´ bin l-Jarraah kutoka Yerusalemu wakati alipokuwa njiani anaelekea ´Umrah. Akasema: “Ee Abu Muhammad! Si kwamba nilikuwa njiani naelekea kwako, lakini nimependa kukutembelea na kuwa kwako.” Akalala kwangu siku moja. Kadhalika akanijia Ibn-ul-Mubaarak kutoka Yerusalemu wakati alipokuwa njiani analekea ´Umrah. Akalala kwangu siku tatu. Nikasema kumwambia: “Ee Abu ´Abdir-Rahmaan! Baki kwangu siku kumi.” Akasema: “Hapana. Ugeni ni siku tatu.”

5- Matembezi ya watu yako katika aina mbili:

1- Matembezi kati ya watu wawili ambao hali zao ziko sawa. Hakuna kasoro wala chuki katika uhusiano wao. Ikiwa ni namna hii, basi napendelea watembeleane na kukutana mara nyingi. Kutembeleana huku hakuleti kuchoshwa. Badala yake kunazidisha kuanisika.

2- Mapenzi kati ya watu hao wawili si kamilifu na bado kuna haya kati yao. Ikiwa ni namna hii, napendelea watembeleane mara chache. Matembezi haya yanaleta kuchoshwa.

6- al-Hasan bin Swaalih amesema:

“Kila mapenzi ambayo hayazidi isipokuwa tu wakati wa kukutana si ya kweli.”

7- Ikiwa uhusiano kati ya mtu na nduguze ni mzuri, haidhuru kitu kule kukutana kwao mara chache kwa sababu uhusiano wao ni mtimilifu. Mapenzi yanayodhurika kwa kukutana mara chache si ya kweli. Yule ambaye hatohakikisha uhusiano mtimilifu na mapenzi kamilifu basi ahakikishe asiwatembelei wengine mara nyingi. Anaweza kuudhika na kuchoshwa.

8- Ibn ´Abbaas amesema:

“Mtu ambaye ni mtukufu zaidi kwenye macho yangu ni yule anayewapita watu wote ili aje kukaa karibu nami.”

9- Qataadah amesema kuhusiana na maneno ya Allaah (Ta´ala):

وَيَسْتَجِيبُ الَّذِينَ آمَنُوا وَعَمِلُوا الصَّالِحَاتِ

“Anawaitika wale walioamini na wakatenda mema… ”[1]

 “Maana yake ni kwamba wanawaombea ndugu zao.”

وَيَزِيدُهُم مِّن فَضْلِهِ

“…  na anawazidishia kutoka katika fadhila Zake.” [2]

“Maana yake ni kwamba wanawaombea ndugu wa ndugu zao.”

10- ´Aamir bin Qays amesema:

“Naikumbuka Baswrah kwa sababu ya mambo mane; kuitikia adhaana, kiu wakati wa mchana, kwa sababu ndugu zangu wako huko na kwa sababu ndio kwetu.”

[1] 42:26

[2] 42:26

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Hibbaan al-Bustiy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Rawdhat-ul-´Uqalaa’ wa Nuzhat-ul-Fudhwalaa’, uk. 114-117
  • Imechapishwa: 02/05/2018