32. Mambo ya wajibu ya dini ambayo yanapaswa kutamkwa na ulimi na kuitakidiwa na moyo

Abu Muhammad ´Abdullaah bin Abiy Zayd al-Qayrawaaniy (Rahimahu Allaah) amesema:

Miongoni mwa hayo ni kuamini kwa moyo na kutamka kwa ulimi ya kwamba Allaah ni Mungu mmoja. Hapana mungu wa haki asiyekuwa Yeye.

MAELEZO

Sambamba na kuitamka haki ni lazima vilevile kuiamini moyoni. Lengo si kutamka kwa ulimi peke yake; ni lazima kuamini pia. Wala haitoshi kuamini peke yake pasi na kutamka. Ni lazima yapatikane yote mawili.

Unaposema kuwa hapana mwabudiwa wa haki isipokuwa Allaah, unakuwa umetamka shahaadah kwa ulimi wako. Ni lazima pia kuamini ndani ya moyo wako maana yake na yale yanayojulishwa nayo. Aidha ni lazima kutendea kazi kwa viungo vyako muqtadha yake. Shahaadah sio neno linalotamkwa peke yake. Shahaadah ni neno tukufu ambalo lina maana na muqtadha yake. Ni lazima uyafahamu haya. Kushuhudia ya kwamba hapana mungu wa haki isipokuwa Allaah ni neno tukufu ambalo ndio funguo ya Uislamu na imani. Ni neno ambalo linahitaji kutiliwa manani na kufahamika.

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Bayaan-ul-Ma´aaniy fiy Sharh Muqaddimati Ibn Abiy Zayd al-Qayrawaaniy, uk. 30
  • Imechapishwa: 15/07/2021