32. Hukumu ya pesa inategemea na jinsi zinavyotumiwa

196- Abu Hurayrah (Radhiya Allaahu ´anh) ameeleza kuwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Hakika mali hii ni kijani kibichi na tamu. Mwenye kuichukua kwa haki na akaitumia kwa haki amepata msaada mzuri kwayo. Na mwenye kuichukua pasi na haki ni kama mfano wa mwenye kula pasi na kushiba.”[1]

197- Khawlah bint Qays (Radhiya Allaahu ´anhaa) ameeleza kuwa amemsikia Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akisema:

“Hakika mali hii ni kijani kibichi. Mwenye kuichukua kwa haki basi atabarikiwa nayo. Yule ambaye kwa tamaa kubwa ataitumia kama jinsi inavyopenda nafsi yake katika mali ya Allaah na Mtume wake basi hana siku ya Qiyaamah isipokuwa Moto.”[2]

at-Tirmidhiy amesema:

“Hadiyth ni nzuri na ni Swahiyh.”

198- Wanachuoni wanasema mwenye mali akiitumia mali yake kwa njia iliokuwa nzuri basi anakuwa katika manzilah ya juu kabisa. Allaah (Ta´ala) amesema:

وَمَا أَمْوَالُكُمْ وَلَا أَوْلَادُكُم بِالَّتِي تُقَرِّبُكُمْ عِندَنَا زُلْفَىٰ إِلَّا مَنْ آمَنَ وَعَمِلَ صَالِحًا فَأُولَـٰئِكَ لَهُمْ جَزَاءُ الضِّعْفِ بِمَا عَمِلُوا وَهُمْ فِي الْغُرُفَاتِ آمِنُونَ

“Na si mali zenu na wala auladi wenu ambavyo vitakukurubisheni Kwetu muwe karibu isipokuwa yule aliyeamini na akatenda mema, basi hao watapata malipo maradufu kutokana na yale waliyoyatenda, nao watakuwa katika maghorofa wenye amani.” (34:37)

Ambaye ataizingatia Qur-aan basi ataona kuwa kuna Aayah nyingi zenye kuisifu mali. Zinakuelekeza uweze kuchuma, kufanya biashara na kukusanya.

199- Sa´iyd bin al-Musayyib amesema:

“Hakuna kheri kwa mtu asiyetafuta mali ili aweze kulipa deni lake, kuilinda heshima yake na kuacha urithi pindi anapofariki.”

200- Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alisema kumwambia Sa´d:

“Ni bora kwako ukiwaacha warithi wako hali ya kuwa ni matajiri kuliko kuwaacha hali ya kuwa ni masikini wakiwaomba watu.”[3]

201- Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Hakuna mali iliyonifaa zaidi kuliko mali ya Abu Bakr.”[4]

202- Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alisema kumwambia ´Amr bin al-´Aasw:

“Ni uzuri wa mali iliyoje ilio na mwanaume mwmea.”[5]

203- Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alimuomba Anas akasema:

“Ee Allaah! Ikithirishe mali yake na kizazi chake na umbariki kwayo.”[6]

204- Sa´iyd bin al-Musayyab aliacha dinari 400.000.

205- Sufyaan ath-Thawriy ambaye alikuwa anajulikana kwa kuipa kwake nyongo dunia aliacha dinari 200.000. Akasema:

“Bora kuwaachia dirhamu 10.000 na kulipa hesabu zao kuliko mimi kuwahitajia watu wengine.”

206- Sufyaan ath-Thawriy alikuwa akisema pia:

“Mali katika zama hizi ni kama silaha.”

207- Salaf hawakuacha siku zote kusifu pesa ikiwa ni kwa sababu vilevile ya kuwasaidia mafukara. Maswahabah wengi walizitafuta pesa na wakaziacha.

[1] al-Bukhaariy (4/32) na Muslim (7/126).

[2] at-Tirmidhiy (2480).

[3] al-Bukhaariy (6733) na Muslim (2/12).

[4] Ahmad (2/253).

[5] Ahmad (4/202).

[6] al-Bukhaariy (2/101).

 

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Ahmad al-Qurtwubiy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Qam´-ul-Hirsw biz-Zuhd wal-Qanaa´ah, uk. 121-123
  • Imechapishwa: 18/03/2017