32. Du´aa ya kupanda vyombo vya safari au mnyama

138- ´Aliy bin Rabiy´ah amesema:

“Nilikuwepo wakati kulipoletwa mnyama kwa ´Aliy bin Abiy Twaalib (Radhiya Allaahu ´anhu) ili apande juu yake. Alipoweka mguu wake katika mapandio alisema:

بسم الله

“Kwa jina la Allaah.”

Wakati alipokaa juu ya mgongo wake akasema:

الْحَمْدُ لله

“Himdi zote ni Zake Allaah.”

Kisha akasema:

سُبْحانَ الَّذِي سَخَّرَ لَنَا هَذَا وَمَا كُنَّا لَهُ مُقْرِنِينَ وَإِنَّا إِلَى رَبِّنَا لَمُنقَلِبُونَ

“Ametakasika ambaye Ametudhalilishia sisi hiki (chombo au huyu mnyama); hatukuwa sisi kwacho ni wenye uwezo! Nasi kwa Mola Wetu tutarejea.” (az-Zukhruf 43 : 13-14)

Halafu akasema:

الْحمد لله الْحمد لله الْحمد لله الله أَكبر الله أَكبر الله أَكبر

”Himdi zote ni Zake Allaah. Himdi zote ni Zake Allaah. Himdi zote ni Zake Allaah. Allaahu Akbar. Allaahu Akbar. Allaahu Akbar.”

Kisha akasema:

سُبْحَانَكَ اللهم إِني ظَلَمْتُ نَفْسي فاغْفِرْ لي فإِنه لا يغفرُ الذُّنُوبَ إِلاَّ أَنتَ

”Umetakasika. Ee Allaah! Hakika mimi nimeidhulumu nafsi yangu. Hivyo nisamehe. Hakika hakuna anayesamehe madhambi isipokuwa Wewe.”

Kisha akaanza kucheka. Kukasemwa: ”Ee kiongozi wa waumini! Kwa nini unacheka?” Akasema: ”Nilimuona Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akifanya kama nilivyofanya kisha akacheka. Nikasema: ”Ee Mtume wa Allaah! Kwa nini unacheka?” Akasema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akasema:

”Hakika ya Mola Wako (Subhaanahu wa Ta´ala) Anastaajabu kwa mja Wake pindi anaposema: ”Ee Allaah! Nisamehe!” [na kusema:] ”Anajua kuwa hakuna mwengine zaidi yangu Mimi anayesamehe madhambi.”

139- Wakati Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alipokuwa anakaa kwenye ngamia yake ili asafiri anasema:

الله أَكبر الله أَكبر الله أَكبر

”Allaahu Akbar. Allaahu Akbar. Allaahu Akbar.”

Kisha anasema:

سُبْحانَ الَّذِي سَخَّرَ لَنَا هَذَا وَمَا كُنَّا لَهُ مُقْرِنِينَ وَإِنَّا إِلَى رَبِّنَا لَمُنقَلِبُونَ

“Ametakasika ambaye Ametudhalilishia sisi hiki (chombo au huyu mnyama); hatukuwa sisi kwacho ni wenye uwezo! Nasi kwa Mola Wetu tutarejea.” (az-Zukhruf 43 : 13-14)

Kisha akasema:

اللهُمَّ إِنِّي أَسْأَلُكَ في سَفَرِنَا هذَا البرَّ والتَّقْوَى وَمِنَ الْعَمَل ما تَرْضَى. اللهُمَّ هَوِّنْ عَلَيْنَا سَفَرَنَا هَذَا واطْوِ عَنَّا بَعْدَهُ اللَّهُمَّ أَنْتَ الصاحِبُ في السَّفَرِ والْخَلِيفَةُ في الأَهْلِ اللَّهُمَّ إِني أَعُوذُ بِكَ مِنْ وَعْثَاءِ السَّفَر وَكَآبَةِ الْمَنْظَرِ وَسُوءِ الْمُنْقَلِب في الْمَالِ والأَهْلِ

”Ee Allaah! Hakika sisi tunakuomba katika safari yetu hii wema, Taqwa na matendo unayoyaridhia. Ee Allaah! Tusahilishie safari yetu hii na tufupishie umbali wake. Ee Allaah! Wewe ndiye mwenye kutulinda katika safari na Mchungaji wa familia iliyobaki. Ee Allaah! Hakika mimi najikinga kwako kutokana na ugumu wa safari, mtazamo mbaya na uovu wa kubadilikiwa katika mali na familia.”

Njiani tunaporejea nyumbani husema hivo hivo na huzidisha:

يِبُونَ تَائِبُونَ عَابِدُونَ لِرَبِّنَا حامِدُونَ

“Tunarudi, hali ya kuwa tunatubia, tunaabudu na Mola wetu tunamhimidi.”

140- Katika upokezi mwingine:

”Wakati Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na Maswahabah zake walipokuwa wakipanda mahala husema:

الله أَكبر

”Allaahu Akbar.”

Wakati wanapoteremka mahala husema:

سُبْحَانَ الله

”Ametakasika Allaah.”

  • Mhusika: Shaykh-ul-Islaam Ahmad bin Taymiyyah
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Swahiyh-ul-Kalim at-Twayyib, uk. 93-95
  • Imechapishwa: 21/03/2017