31. Mlango kuhusu maneno Yake (Ta´ala) “Miongoni mwa watu wako wenye kuchukua asiyekuwa Allaah kuwa ni mungu mshirika ambapo wanawapenda kama mapenzi wanavyompenda Allaah… “

Shaykh-ul-Islaam Muhammad bin ´Abdil-Wahhaab (Rahimahu Allaah) amesema:

1- Allaah (Ta´ala) amesema:

وَمِنَ النَّاسِ مَن يَتَّخِذُ مِن دُونِ اللَّـهِ أَندَادًا يُحِبُّونَهُمْ كَحُبِّ اللَّـهِ

“Miongoni mwa watu wako wenye kuchukua asiyekuwa Allaah kuwa ni mungu mshirika ambapo wanawapenda kama mapenzi wanavyompenda Allaah… “ (al-Baqarah 02:165)

2-

قُلْ إِن كَانَ آبَاؤُكُمْ وَأَبْنَآؤُكُمْ وَإِخْوَانُكُمْ وَأَزْوَاجُكُمْ وَعَشِيرَتُكُمْ وَأَمْوَالٌ اقْتَرَفْتُمُوهَا وَتِجَارَةٌ تَخْشَوْنَ كَسَادَهَا وَمَسَاكِنُ تَرْضَوْنَهَا أَحَبَّ إِلَيْكُم مِّنَ اللّهِ وَرَسُولِهِ وَجِهَادٍ فِي سَبِيلِهِ فَتَرَبَّصُواْ حَتَّى يَأْتِيَ اللّهُ بِأَمْرِهِ وَاللّهُ لاَ يَهْدِي الْقَوْمَ الْفَاسِقِينَ

“Sema: “Ikiwa baba zenu na watoto wenu na ndugu zenu na wake zenu na jamaa zenu na mali mliyoichuma na biashara mnayoikhofia kuharibika kwake na majumba mnayoridhika nayo –  [ikiwa vyote hivi] ni vipenzi zaidi kwenu kuliko Allaah na Mtume Wake na kupambana jihaad katika njia Yake, basi ngojeeni mpaka Allaah alete Amri Yake; hakika Allaah hawaongoi watu mafasiki.” (at-Tawbah 09:24)

3- Anas (Radhiya Allaahu ´anh) ameeleza kwamba Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Hatoamini mmoja wenu mpaka mimi niwe kwake ni mpendwa zaidi kuliko baba yake, mtoto wake na watu wote.”[1]

Ameipokea al-Bukhaariy na Muslim.

4- al-Bukhaariy na Muslim wamepokea kwamba Anas (Radhiya Allaahu ´anh) amesimulia kuwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Mambo matatu yakipatikana kwa mtu hupata utamu wa imani; Allaah na Mtume Wake wawe ni wenye kupendwa zaidi kwake kuliko yeyote yule, ampende mtu na asimpendei jengine isipokuwa iwe ni kwa ajili ya Allaah na achukie kurudi katika ukafiri baada ya Allaah kumwokoa nao kama anavyochukia kutupwa ndani ya Moto.”[2]

Katika upokezi mwingine imekuja:

“Hatopata mmoja wenu utamu wa imani mpaka… “[3]

5- Ibn ´Abbaas (Radhiya Allaahu ´anhumaa) amesema:

“Mwenye kupenda kwa ajili ya Allaah na akachukia kwa ajili ya Allaah, kufanya urafiki kwa ajili ya Allaah na kujenga uadui kwa ajili ya Allaah, hakika hupatikana urafiki wa Allaah kwa hayo. Na wala mja hatohisi utamu wa imani – hata kama zitakuwa nyingi swalah na swawm zake – mpaka awe hivo. Leo watu wengi wamekuwa ni wenye kujenga udugu kwa ajili ya mambo ya kidunia, hilo haliwasaidii wenye nalo kitu.”

Ameipokea Ibn Jariyr.

6- Ibn ´Abbaas amesema kuhusu maneno Yake Allaah (Ta´ala):

إِذْ تَبَرَّأَ الَّذِينَ اتُّبِعُوا مِنَ الَّذِينَ اتَّبَعُوا وَرَأَوُا الْعَذَابَ وَتَقَطَّعَتْ بِهِمُ الْأَسْبَابُ

“Wale waliofuatwa watakapojitenga mbali na wale waliowafuata wakiwa wameshaiona adhabu [mbele yao] na yatawakatikia mafungamano yao.”

“Bi maana mapenzi.”

MAELEZO

1- Allaah (Ta´ala) amesema:

وَمِنَ النَّاسِ مَن يَتَّخِذُ مِن دُونِ اللَّـهِ أَندَادًا يُحِبُّونَهُمْ كَحُبِّ اللَّـهِ

“Miongoni mwa watu wako wenye kuchukua asiyekuwa Allaah kuwa ni mungu mshirika ambapo wanawapenda kama mapenzi wanavyompenda Allaah… “

Mlango huu unazungumzia mapenzi kwa Allaah na kwamba ni miongoni mwa ´ibaadah muhimu na bora zaidi na msingi wa dini. Kwa sababu kumpenda Allaah kunapelekea kumtakasia Yeye ´ibaadah, kutekeleza maamrisho Yake na kujiepusha na makatazo Yake.

Aayah inathibitisha kwamba wapo watu ambao wanamfanyia Allaah washirika katika masanamu, watu na mawe. Wanawaabudu kwa mapenzi anayostahiki kupendwa Allaah pekee. Wanawapenda washirika hawa kama mapenzi wanavyompenda Allaah au kama waumini wanavyompenda Allaah. Watu hawa wamepotea kwa vile wamewapenda wengine pamoja na Allaah, wamewawekea nadhiri, wamewanyenyekea na kuwaomba. Mapenzi ya kuwapenda wengine yanatakiwa kuwa ni yenye kuafikiana na mapenzi ya Allaah. Kwa mfano tunawapenda Mitume wa Allaah kwa sababu ni Mitume wa Allaah, hatuwaabudu kwa mapenzi haya. Kadhalika tunawapenda waumini; tunawapenda kwa sababu wamemtii Allaah na hivyo tunawasapoti. Ama kuhusu mapenzi ya kujidhalilisha na mapenzi ya ´ibaadah anatakiwa kutekelezewa Allaah pekee. Hayawi kwa mwengine. Washirikina wanawatekelezea mapenzi haya washirika. Bali baadhi yao wanathubutu kuapa kwa jina la Allaah kwa kusema uongo na wala hawawezi kuthubutu kufanya hivo kwa washirika wao na wanachuoni wao kwa sababu wanaona kuwa washirika hawa wanalipiza kisasi vibaya sana na kwa haraka kuliko Allaah.

 Allaah (Ta´ala) amesema:

وَالَّذِينَ آمَنُواْ أَشَدُّ حُبًّا لِّلّهِ

“Lakini wale walioamini wana mapenzi zaidi kwa Allaah.”

Ni mapenzi yenye nguvu na zaidi kabisa kuliko mapenzi ya washirikina hawa kwa waungu wao kwa sababu wanamwabudu Allaah kwa kumpwekesha na wanatambua haki Yake (´Azza wa Jall).

Allaah (Ta´ala) amesema:

وَلَوْ يَرَى الَّذِينَ ظَلَمُوا إِذْ يَرَوْنَ الْعَذَابَ أَنَّ الْقُوَّةَ لِلَّـهِ جَمِيعًا وَأَنَّ اللَّـهَ شَدِيدُ الْعَذَابِ

”Lau wale waliodhulumu wanaijua [adhabu inayowasubiri] watakapoona adhabu [mbele yao siku hiyo] kwamba nguvu zote ni za Allaah na kwamba hakika Allaah ni mkali wa kuadhibu.” (al-Baqarah 02:165)

Lau wangeliyaona hayo basi wangelimpenda Allaah zaidi, wakamuadhimisha na wangelimtakasia Yeye ´ibaadah. Lakini kwa sababu ya ujinga wao na uchache wa uoni wao kumewafanya kutumbukia katika shirki. Allaah (Ta´ala) amesema:

إِذْ تَبَرَّأَ الَّذِينَ اتُّبِعُوا مِنَ الَّذِينَ اتَّبَعُوا وَرَأَوُا الْعَذَابَ وَتَقَطَّعَتْ بِهِمُ الْأَسْبَابُ

“Wale waliofuatwa watakapojitenga mbali na wale waliowafuata wakiwa wameshaiona adhabu [mbele yao] na yatawakatikia mafungamano yao.”

Wakati wale mawalii wa Allaah waliokuwa wakiabudiwa watakapoona adhabu ndipo watajiweka mbali kabisa na wale waliokuwa wakiwaabudu. Watasema:

رَبَّنَا هَـٰؤُلَاءِ الَّذِينَ أَغْوَيْنَا أَغْوَيْنَاهُمْ كَمَا غَوَيْنَا ۖ تَبَرَّأْنَا إِلَيْكَ ۖ مَا كَانُوا إِيَّانَا يَعْبُدُونَ

“Mola wetu! Hawa ndio wale tuliowapotoa. Tumewapotoa kama tulivyopotoka. Tumejivua jukumu mbele Yako – hawakuwa wakituabudu sisi.” (al-Qaswasw 28:63)

Ama kuhusu mapenzi ya kimaumbile kama kupenda chakula, wanawake na watoto, mapenzi haya hayapunguzi mapenzi ya kumpenda Allaah midhali mtu hayatangulizi mbele kabla ya mapenzi ya kumpenda Yeye. Ikiwa yatapitiliza na kuwa na nguvu kiasi cha kwamba kwa mfano mtu akawa anamtii mke wake katika maasi, basi mapenzi haya yanapunguza imani kwa kiasi cha vile mtu atavyoyatanguliza mbele ya mapenzi ya Allaah. Ni lazima mapenzi haya yafungamanishwe na Shari´ah ya Allaah.

3- Anas (Radhiya Allaahu ´anh) ameeleza kwamba Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Hatoamini mmoja wenu mpaka mimi niwe kwake ni mpendwa zaidi kuliko baba yake, mtoto wake na watu wote.”

Ameipokea al-Bukhaariy na Muslim.

Hii ni dalili inayothibitisha kwamba ni wajibu kumpenda Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) yanayolingana naye yanayopelekea kumfuata na kutii maamrisho yake na kujiepusha na makatazo yake. Haihusiani na mapenzi ya kumwabudu (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam); ni lazima yawe ni yenye kuafikiana na mapenzi ya kumpenda Allaah.

4- al-Bukhaariy na Muslim wamepokea kwamba Anas (Radhiya Allaahu ´anh) amesimulia kuwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Mambo matatu yakipatikana kwa mtu hupata utamu wa imani; Allaah na Mtume Wake wawe ni wenye kupendwa zaidi kwake kuliko yeyote yule, ampende mtu na asimpendei jengine isipokuwa iwe ni kwa ajili ya Allaah na achukie kurudi katika ukafiri baada ya Allaah kumwokoa nao kama anavyochukia kutupwa ndani ya Moto.”

Katika upokezi mwingine imekuja:

“Hatopata mmoja wenu utamu wa imani mpaka… “

Ni dalili inayothibitisha kwamba mapenzi ya kumpenda Allaah na Mtume Wake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) yanatakiwa kutangulizwa mbele ya mapenzi ya kuwapenda mababa, watoto, mali na vyenginevyo. Hivyo mtu anatakiwa kumtii Allaah na kujiepusha na makatazo Yake japokuwa yatakuwa ni yenye kupingana na  matamanio ya mtoto wake, mke wake au wengineo. Allaah amesema:

قُلْ إِن كَانَ آبَاؤُكُمْ وَأَبْنَآؤُكُمْ وَإِخْوَانُكُمْ وَأَزْوَاجُكُمْ وَعَشِيرَتُكُمْ وَأَمْوَالٌ اقْتَرَفْتُمُوهَا وَتِجَارَةٌ تَخْشَوْنَ كَسَادَهَا وَمَسَاكِنُ تَرْضَوْنَهَا أَحَبَّ إِلَيْكُم مِّنَ اللّهِ وَرَسُولِهِ وَجِهَادٍ فِي سَبِيلِهِ فَتَرَبَّصُواْ حَتَّى يَأْتِيَ اللّهُ بِأَمْرِهِ وَاللّهُ لاَ يَهْدِي الْقَوْمَ الْفَاسِقِينَ

“Sema: “Ikiwa baba zenu na watoto wenu na ndugu zenu na wake zenu na jamaa zenu na mali mliyoichuma na biashara mnayoikhofia kuharibika kwake na majumba mnayoridhika nayo –  [ikiwa vyote hivi] ni vipenzi zaidi kwenu kuliko Allaah na Mtume Wake na kupambana jihaad katika njia Yake, basi ngojeeni mpaka Allaah alete Amri Yake; hakika Allaah hawaongoi watu mafasiki.”

Ni dalili inayothibitisha kwamba Jihaad katika njia ya Allaah inatakiwa kutangulizwa mbele kabla ya matamanio ya nafsi na ya jamaa wa karibu. Vinginevyo mtu anakuwa ni mwenye kuingia katika makemeo:

فَتَرَبَّصُواْ حَتَّى يَأْتِيَ اللّهُ بِأَمْرِهِ وَاللّهُ لاَ يَهْدِي الْقَوْمَ الْفَاسِقِينَ

“… basi ngojeeni mpaka Allaah alete Amri Yake; hakika Allaah hawaongoi watu mafasiki.”

Hizi ni miongoni mwa sababu za ukamilifu wa imani. Ni wajibu kuchukia ukafiri na makafiri na kuitakidi ubatilifu wake.

Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Watu saba Allaah atawafunika katika kivuli siku ambayo kutakuwa hakuna kivuli isipokuwa kivuli Chake; kiongozi  mwadilifu, kijana ambaye amekulia katika kumuabudu Allaah, mtu ambaye moyo wake umefungamana na misikiti, watu wawili ambao wamependana kwa ajili ya Allaah na hivyo wakakusanyika kwa ajili Yake na wakatengana kwa ajili Yake, mtu ambaye ameitwa na mwanamke mwenye cheo na akasema “Mimi namuogopa Allaah, Mola wa walimwengu”, mtu ambaye ametoa swadaqah kisiri kabisa mpaka mkono wake wa kushoto haujui kile kilichotolewa na mkono wake wa kulia na mtu ambaye amemkumbuka Allaah akiwa peke yake na akaanza kutitikwa na machozi.”

Zingatia “watu wawili ambao wamependana kwa ajili ya Allaah na hivyo wakakusanyika kwa ajili Yake na wakatengana kwa ajili Yake”.

5- Ibn ´Abbaas (Radhiya Allaahu ´anhumaa) amesema:

“Mwenye kupenda kwa ajili ya Allaah na akachukia kwa ajili ya Allaah, kufanya urafiki kwa ajili ya Allaah na kujenga uadui kwa ajili ya Allaah, hakika hupatikana urafiki wa Allaah kwa hayo. Na wala mja hatopata utamu yawa imani – hata kama zitakuwa nyingi swalah na swawm zake – mpaka awe hivo. Leo watu wengi wamekuwa ni wenye kujenga udugu kwa ajili ya mambo ya kidunia, hilo haliwasaidii wenye nalo kitu.”

Ameipokea Ibn Jariyr.

Utamu wa imani ni ladha ya imani. Ni dalili inayoonyesha kuwa urafiki wa Allah unapatikana kwa kupenda na kuchukia kwa ajili ya Allaah. Ibn ´Abbaas (Radhiya Allaahu ´anhumaa) amesema:

“Na wala mja hatohisi utamu wa imani – hata kama zitakuwa nyingi swalah na swawm zake – mpaka awe hivo.”

Bi maana mpaka apende na kuchukia kwa ajili ya Allaah. Amesema:

“Leo watu wengi wamekuwa ni wenye kujenga udugu kwa ajili ya mambo ya kidunia, hilo haliwasaidii wenye nalo kitu.”

Haya yalikuwa katika wakati wake (Radhiya Allaahu ´anhumaa). Watu wengi walikuwa ni wenye kupendana na ni wenye kuchukiana kwa ajili ya dunia. Hili ni jambo khatari. Halisaidii kitu. Bali ni jambo linawadhuru ikiwa linawazuia kutokamana na haki na kwenda kinyume na Shari´ah ya Allaah. Hata hivyo hakuna neno ikiwa watafanya kazi kwa ajili ya dunia katika biashara na kutafuta riziki ili waweze kumtii Allaah midhali mambo hayo hayadhuru imani yao na wala hayawapelekei kuingia katika madhambi.

6- Ibn ´Abbaas amesema kuhusu maneno Yake Allaah (Ta´ala):

إِذْ تَبَرَّأَ الَّذِينَ اتُّبِعُوا مِنَ الَّذِينَ اتَّبَعُوا وَرَأَوُا الْعَذَابَ وَتَقَطَّعَتْ بِهِمُ الْأَسْبَابُ

“Wale waliofuatwa watakapojitenga mbali na wale waliowafuata wakiwa wameshaiona adhabu [mbele yao] na yatawakatikia mafungamano yao.”

“Bi maana mapenzi.”

Bi maana mapenzi yaliokuwa baina yao yasiyoafikiana na dini ya Allaah. Yatakatika siku ya Qiyaamah, watafanyiana khiyana na yatakuwa uadui.

[1] al-Bukhaariy (15) na Muslim (44).

[2] al-Bukhaariy (16) na Muslim (43).

[3] al-Bukhaariy (6041).

  • Mhusika: Imaam ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah bin Baaz
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh Kitaab-it-Tawhiyd, uk. 105-107
  • Imechapishwa: 23/10/2018