3. Virusi vya corona – Kufanyia kazi matibabu ya Kiislamu

3- Shari´ah ya Kiislamu imekuja kuhimiza mtu kufanya sababu na kujitibisha. Mtu kujitibisha ni jambo halipingani na kumtegemea Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala). Shari´ah ya Kiislamu imekuja kwa sampuli mbili za matibabu: Tiba ya kujilinda kabla ya kujitokeza kwa maradhi yenyewe na tiba ya kujitibisha inayokuwa baada ya maradhi kujitokeza. Yule mwenye kusoma kitabu “at-Twibb an-Nabawiy” cha ´Allaamah Ibn-ul-Qayyim (Rahimahu Allaah) basi ataona maajabu kuhusu maudhui haya juu ya yale yaliyokuja na Shari´ah ya Uislamu. Kwa mfano upande wa tiba ya kujilinda Mtume wetu (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Yule mwenye kupambaukiwa na akala tende saba za ´Ajwah basi hatodhurika siku hiyo kwa sumu wala uchawi.”[1]

Vilevile Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Hakuna mja yeyote atakayesema mara tatu asubuhi ya kila mchana na jioni ya kila usiku:

بِسْمِ اللهِ الَّذِي لاَ يَضُرُّ مَعَ اسْمِهِ شَيء في الأرْضِ وَلاَ في السَّمَاءِ وَهُوَ السَّمِيعُ العَلِيمُ

“Kwa jina la Allaah ambaye hakidhuru pamoja na jina Lake chochote katika ardhi na katika mbingu Naye ni Mwenye kusikia, mjuzi.”

isipokuwa hakuna chochote kitachomdhuru.” ´Abdullaah bin Khubayb amesema:

 “Usiku mmoja wenye mvua na giza kali tulitoka nje tukimtafuta Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ili atuombee du´aa. Tukamuwahi ambapo akasema: “Sema.” Sikusema kitu.” Akasema tena: “Sema.” Sikusema kitu.” Akasema tena: “Sema.” Nikasema: “Niseme nini, ee Mtume wa Allaah?” Akasema: “Sema mara tatu: “Hakika Yeye ni Allaah – Mmoja pekee” na Suurah al-Falaq na an-Naas wakati unapoingiliwa na jioni na unapopambazukiwa. Kutakutosheleza kutokamana na kila kitu.”

Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alikuwa haachi kuomba du´aa hizi wakati anapoingiliwa na jioni na wakati anapoingiliwa na asubuhi:

اللهُمَّ إِنِّي أَسْأَلُكَ الْعَافِيَةَ فِي الدُّنْيَا والآخِرَةِ اللَّهُمَّ إِنِّي أَسْأَلُكَ الْعَفْوَ والْعَافِيَةَ في دِيني ودُنْيَايَ وأَهْلِي وَمَالِي اللَّهُمَّ اسْتُرْ عَوْرَاتِي وآمِنْ رَوْعَاتِي اللَّهُمَّ احْفَظنِي بَيْنَ يَدَيَّ وَمِنْ خَلْفِي وَعَنْ يَمِيني وَعَنْ شِمَالِي وَمِنْ فَوْقِي وَأَعُوذُ بِعَظَمَتِكَ أَنْ أُغْتَالَ مِنْ تَحْتِي

“Ee Allaah! Hakika mimi nakuomba usalama duniani na Aakhirah. Ee Allaah! Hakika mimi nakuomba msamaha na usalama katika dini, dunia, familia yangu na mali yangu. Ee Allaah! Nifichie aibu zangu na unisalimishie hisia zangu. Ee Allaah! Nihifadhi mbele yangu, nyuma yangu, upande wangu wa kuume, kushotoni kwangu, juu yangu na chini yangu. Naomba ulinzi kwa utukufu Wako kuuliwa kutoka chini yangu.”

Kupitia du´aa hizi mja analindwa kikamilifu kutoka katika kila pande.

Inapokuja katika upande wa tiba ya kujitibu, imepokelewa nasaha na maelekezo matukufu kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam), itarefuka kukiyataja. Rejea katika kitabu “Zaad-ul-Ma´aad” cha Ibn-ul-Qayyim.

[1] al-Bukhaariy (5445) na Muslim (2047).

  • Mhusika: Shaykh ´Abdur-Razzaaq bin ´Abdil-Muhsin al-´Abbaad
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: https://ar.islamway.net/article/80439/%D9%81%D9%8A%D8%B1%D9%88%D8%B3-%D9%83%D9%88%D8%B1%D9%88%D9%86%D8%A7-%D8%A7%D9%84%D8%AC%D8%AF%D9%8A%D8%AF-%D9%81%D9%8A%D8%B1%D9%88%D8%B3-%D8%A7%D9%84%D8%B5%D9%8A%D9%86
  • Imechapishwa: 10/03/2020