29. Watoto wa Kiislamu wanatakiwa kulelewa kwa mujibu wa Uislamu

Abu Muhammad ´Abdullaah bin Abiy Zayd al-Qayrawaaniy (Rahimahu Allaah) amesema:

Pia wanatakiwa kufunzwa maneno na matendo ambayo Allaah ameyafaradhisha kwa waja kabla ya kubaleghe. Wafikie baleghe hali ya kuwa yamekwishakita ndani ya mioyo yao na wanahisi utulivu kwayo na waanasike juu yale wanayoyafanya.

MAELEZO

Wasiamrishwe kuswali peke yake, kuwatenganisha katika malazi na kuwapiga pindi wanapoacha jambo la lazima, bali wanatakiwa kufunzwa mambo mengine yaliyobaki ya dini ikiwa ni pamoja na mambo ya halali na haramu na tofauti kati ya tabia nzuri na tabia mbaya – kwa njia fupi. Tangu wakiwa watoto wanatakiwa kuingizwa mambo ya dini; adabu na tabia njema. Vilevile wakatazwe kutamka maneno ya haramu, matusi, maapizo, usengenyi na umbea. Pia wanatakiwa kukatazwa kufanya matendo ya haramu, kuiba, kuchukua mali za watu na usaliti. Waleleke juu ya njia ambayo dini yao, maisha yao ya kidunia, tabia na namna ya kutangamana kwao na watu kuko sawa.

Hii ndio natija ya malezi utotoni kabla ya kubaleghe; wakishabaleghe baada ya kuwa wameleleka juu ya malezi haya mazuri basi inakuwa rahisi kuwaongoza na wanaendelea juu ya malezi haya mazuri ambayo baadaye yanazidi na kuongezeka. Ni kama mfano wa mmea. Mmea unakuwa hatua kwa hatua mpaka baadaye unakuja kutoa matunda.

Haya ndio malezi mazuri. Tunatakiwa kuchukua misingi ya malezi yetu kutoka katika dini yetu. Hatuchukui kutoka katika malezi ya wamagharibi, kwa sababu hakuna kheri yoyote ndani yake.

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Bayaan-ul-Ma´aaniy fiy Sharh Muqaddimati Ibn Abiy Zayd al-Qayrawaaniy, uk. 27-28
  • Imechapishwa: 14/07/2021