Shaykh-ul-Islaam Muhammad bin ´Abdil-Wahhaab (Rahimahu Allaah) amesema:

… jibu: “Kwa alama Zake na viumbe Vyake. Miongoni mwa alama Zake ni usiku, mchana, jua na mwezi. Miongoni mwa viumbe Vyake ni mbingu saba na ardhi saba, vilivyomo ndani yake na vilivyomo kati yake.”

MAELEZO

Alama ni ishara ya kitu chenye kujulisha na kuibainisha alama hiyo.

Alama za Allaah ni aina mbili; za kilimwengu na za Kishari´ah. Alama za kilimwengu ni viumbe na alama za Kishari´ah ni Wahy ambao Allaah amewateremshia Mitume Yake. Kutokana na haya tukifasiri kwamba ni alama za kilimwengu na za Kishari´, basi maneno ya mtunzi (Rahimahu Allaah):

“Kwa alama Zake na viumbe Vyake.”

yanajulisha kwamba zile maalum ni ushirikiano wa zile zilizoenea. Na tukifanya kuwa ni maalum juu ya zile alama za Kishari´ah, basi itakuwa ni ushirikiano unaoleta tofauti na upambanuzi. Hali vovyote ilivyo, Allaah (´Azza wa Jall) anatambulika kwa alama Zake za kilimwengu ambazo ni vile viumbe Vyake vikubwa na yale mambo ya ajabu na hekima ya hali ya juu inayopatikana ndani yake. Vivyo hivyo anatambulika kwa alama za Kishari´ah na yaliyomo ndani yake katika uadilifu, manufaa na kuzuia madhara.

Katika kila kitu ipo alama

Inayofahamisha kuwa Yeye ni Mmoja

Alama zote za Allaah zinajulisha ukamilifu wa uwezo wake, hekima na rehema. Jua ni moja katika alama za Allaah (´Azza wa Jall) kwa sababu linatembea kwa nidhamu na njia ya kipekee tangu hapo Allaah (´Azza wa Jall) alipoliumba na litaendelea kufanya hivo mpaka pale Allaah (Ta´ala) atapotoa idhini ya kuharibika kwa ulimwengu. Kwa ajili hiyo jua linatembea kwa kutulia kwake. Amesema (Ta´ala):

وَالشَّمْسُ تَجْرِي لِمُسْتَقَرٍّ لَّهَا ۚ ذَٰلِكَ تَقْدِيرُ الْعَزِيزِ الْعَلِيمِ

“Na jua linatembea kwa muda wake wa kutulia [kituoni] kwake. Hayo ni makadirio ya Mwenye nguvu zisizoshindika, Mjuzi wa kila kitu.” (Yaa Siyn 36 : 38)

Vilevile ni miongoni mwa alama za Allaah (Ta´ala) kwa sababu ya ukubwa na athari yake. Ama ukubwa wake, ni likubwa, na kuhusu athari yake, ni kwamba linanufaisha miili, miti, mito, bahari na vyenginevyo. Tukilitazama jua ambalo ni alama kubwa na ule umbali mkubwa kati yetu sisi na lenyewe, pamoja na hayo tunapata joto lake kali. Kisha litazame tena na uone ni kitu gani mwangaza wake mkubwa unachangia unapowafanya watu kuhifadhi kiasi kikubwa cha pesa. Wakati wa mchana mtu hana haja ya mwangaza mwingine na kwa hivyo ananufaika kwa kuhifadhi pesa zake. Hili ni katika moja ya alama Zake ambazo sisi hatuzifahamu isipokuwa kitu kidogo tu.

Vivyo hivyo mwezi ni miongoni mwa alama za Allaah (´Azza wa Jall). Ameupangia vituo na kila usiku una kituo chake:

وَالْقَمَرَ قَدَّرْنَاهُ مَنَازِلَ حَتَّىٰ عَادَ كَالْعُرْجُونِ الْقَدِيمِ

“Na mwezi pia Tumeukadiria vituo [unatembea] mpaka unarudi kana kwamba ni shina la mtende lilopinda la zamani.” (Yaa Siyn 36 : 39)

Huanza hali ya kuwa ni mdogo kisha unakuwa polepole mpaka ukakamilika kuwa mkubwa. Halafu baada ya hapo ukarudi kuwa mdogo. Unafanana na mtu ambaye anaumbwa akiwa mnyonge. Baada ya hapo anakuwa na nguvu polepole mpaka siku moja anarudi kuwa mnyonge kwa mara nyingine tena – ametukuka Allaah, mbora wa Waumbaji!

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh Thalaathat-il-Usuwl, uk. 47-48
  • Imechapishwa: 20/05/2020