29. al-´Ayyaashiy upotoshaji wa tano wa al-Baqarah

al-´Ayyaashiy amesema kuhusu Kauli ya Allaah (Ta´ala):

يَا بَنِي إِسْرَائِيلَ اذْكُرُوا نِعْمَتِيَ الَّتِي أَنْعَمْتُ عَلَيْكُمْ وَأَنِّي فَضَّلْتُكُمْ عَلَى الْعَالَمِينَ

“Enyi wana wa Israaiyl! Kumbukeni neema Yangu Niliyokuneemesheni na hakika Mimi Nimekufadhilisheni juu ya walimwengu.” (02:47)

“Haaruun bin Muhammad al-Halabiy amesema: “Nilimuuliza Abu ´Abdillaah kuhusu Kauli ya Allaah:

يَا بَنِي إِسْرَائِي

“Enyi wana wa Israaiyl!”

Akajibu: “Ni sisi tu.”

Muhammad bin ´Aliy amenieleza ya kwamba alimuuliza Abu ´Abdillaah kuhusu Kauli ya Allaah:

يَا بَنِي إِسْرَائِي

“Enyi wana wa Israaiyl!”

Akasema: “Inahusu watu wa familia ya Muhammad (´alayhis-Salaam) tu.”

Abu Daawuud ameeleza kutoka kwa wale waliomsikia Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akisema:

“Mimi ni mja wa Allaah na jina langu ni Ahmad. Mimi ni mja wa Allaah na ninaitwa Israaiyl. Yale Aliyowaamrisha Israaiyl Ameniamrisha mimi na pindi Alipowakusudia Israaiyl Ananikusudia mimi.”

Mhakiki ameelekeza katika vitabu “al-Burhaan” (01/95) na “al-Bihaar (07/178).

Wana wa Israaiyl wanaozungumzishwa katika Qur-aan ni mayahudi. Ni muislamu yupi anaridhia kuambiwa kuwa ni Israaiyl, seuze watu wa familia ya Muhammad (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam)? Vipi na wakati Allaah Amewakemea katika Aayah nyingi ikiwa ni pamoja na:

مَن لَّعَنَهُ اللَّـهُ وَغَضِبَ عَلَيْهِ وَجَعَلَ مِنْهُمُ الْقِرَدَةَ وَالْخَنَازِيرَ وَعَبَدَ الطَّاغُوتَ

“Yule ambaye Allaah Amemlaani na Akamghadhibikia na Akawafanya miongoni mwao manyani na nguruwe na wakaabudu twaaghuut [mashaytwaan].” (05:60)

Waliwaua Mitume:

كُلَّمَا جَاءَهُمْ رَسُولٌ بِمَا لَا تَهْوَىٰ أَنفُسُهُمْ فَرِيقًا كَذَّبُوا وَفَرِيقًا يَقْتُلُونَ

“Kila alipowajia Mtume kwa yale yasiyoyapenda nafsi zao; kundi waliwakadhibisha [Mitume hao] na kundi [lingine] wakawaua.” (05:70)

وَأُشْرِبُوا فِي قُلُوبِهِمُ الْعِجْلَ بِكُفْرِهِمْ

“Wakanyweshwa katika nyoyo zao [mapenzi ya kumuabudu] ndama kwa kufuru yao.” (02:93)

Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema kuhusu wao:

“Enyi ndugu wa manyani na nguruwe.”

Tendo hili la Raafidhwah linaashiria kuonyesha kwamba wana uhusiano maalum na mayahudi na wanajenga madaraja na wao kwa njia ya watu wa familia ya Muhammad (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kuwa ni wana wa Israaiyl. Waislamu ni wenye kujitenga mbali kabisa na upotoshaji huu mkubwa wa watu wa nyumba ya Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam).

Aayah hizi Allaah Anawazungumzisha mayahudi waliomkufuru Allaah, Mtume Wake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na Kitabu Chake. Ni vipi Abu ´Abdillaah anaweza kusema kuwa wao ni wana wa Israaiyl? Vipi kwa mara nyingine anaweza kusema kuwa Aayah hii inahusu watu wa familia ya Muhammd (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) tu? Ninaapa kwa Allaah ya kwamba Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) hakusema kuwa yeye ni Israaiyl.

Yule mwenye kugundua uongo wa Raafidhwah juu ya Allaah na Mtume Wake na upotoshaji wao wa kutisha juu ya Kitabu cha Allaah basi ataona kuwa wamewazidi mayahudi na manaswara inapokuja katika kumsemea Allaah uongo, upotoshaji wa Kitabu Chake na kumtuhumu ukafiri huu ´Aliy (Radhiya Allaahu ´anhu) na watu wa familia yake.

  • Mhusika: ´Allaamah Rabiy´ bin Haadiy al-Madkhaliy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: al-Intiswaar li Kitaab-il-´Aziyz al-Jabbaar, uk. 60-61
  • Imechapishwa: 19/03/2017