26. Jeshi la waislamu katika vita vya Badr

Tutataja kwa ufupi vita vya pili vya Badr. Ilikuwa ni vita vikubwa ambavyo Allaah alifarikisha kati ya haki na batili, akaupa nguvu Uislamu na akaitokomeza kufuru na makafiri.

Katika Ramadhaan mwaka wa 02 Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alifikiwa na khabari kwamba kuna msafara unaokuja kutoka Shaam. Msafara huo ulikuwa ukiongozwa na Abu Sufyaan Sakhr bin Harb na ulikuwa na wanaume thelathini au arobaini wa Quraysh. Ulikuwa ni msafara mkubwa kabisa ambao ulikuwa na mali nyingi za Quraysh. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akawashaji´isha watu waliokuwepo kutoka kuuendea. Haikuwa kundi kubwa. Walikuwa kama wanaume 310. Kulikuwa kumebaki siku nane iingie Ramadhaan. Wakati huo Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alimfanya Ibn Umm Maktuum kubaki al-Madiynah (Radhiya Allaahu ´anh) kama khalifa na kuwaswalisha watu. Walipofika Rawhaa´ (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akamrudisha Abu Lubaabah bin ´Abdi-Mundhir na akamfanya kuwa khalifa al-Madiynah.

Hawaku na farasi wowote zaidi ya farasi wa az-Zubayr na wa al-Miqdaad al-Aswad al-Kindiy. Walikuwa na ngamia 70. Watu wawili, watatu, wane mpaka zaidi ya hapo walikuwa wakipokezana kwenye ngamia mmoja. Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam), ´Aliy na Mardhad bin Abiy Mardhad al-Ghanwiy wakipokezana ngamia mmoja. Zayd bin Haarithah, Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam), Anasah na Abu Kabshah ambao ni watumwa walioachwa huru na Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na Hamzah wakipokezana ngamia mmoja. Abu Bakr, ´Umar na ´Abdur-Rahmaan bin ´Awf wakipokezana na kadhalika.

  • Mhusika: Imaam Ismaa´iyl bin Kathiyr ad-Dimashqiy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: al-Fusuwl fiy Siyrat-ir-Rasuwl, uk. 45-46
  • Imechapishwa: 26/04/2018