24. Radd juu ya utata wa Tawassul zao za ki-Bid´ah na zilizoharamishwa II

Tisa: Miongoni mwa shubuha zao ni kufungamana na baadhi ya Hadiyth ambazo wamedhani kwamba zinasilihisha hoja zao. Kwa mfano Hadiyth ambayo imepokelewa na at-Tirmidhiy katika “Jaami´” yake kwa sanadi yake kupitia kwa ´Uthmaan bin Haniyf ambaye amesimulia kwamba kuna kipofu alikuja kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ambapo akamwambia: “Muombe Allaah aniponye.” Akasema: “Ukitaka nitakuombea na ukitaka kuwa na subira – na hilo ni bora kwako.” Akamwambia: “Niombee.” Ndipo akamwamrisha atawadhe na afanye vizuri wudhuu´ wake halafu aombe kwa kusema:

اللهم إني أسألك وأتوجه إليك بنبيّك محمد نبيّ الرّحمة، إني توجّهت به إلى ربّي في حاجتي هذه لتقضى، اللهم فشفِّعه فيَّ

“Ee Allaah! Hakika mimi nakuomba na natawasuli kwako kwa Mtume wako Muhammad; Mtume wa rehema. Ee Mola wangu! Mimi naelekea Kwako ili unitatulie haja yangu hii. Ee Allaah! Niponye.”[1]

at-Tirmidhiy amesema:

“Hadiyth hii ni nzuri na Swahiyh na geni. Hatuitambui isipokuwa kupitia upokezi wa Abu Ja´far. Huyu sio [yule Abu Ja´far] al-Khatwmiy.”

Wakasema kwamba katika Hadiyth hizi kuna dalili kwamba inafaa kwa mtu kumwelekea na kumwomba Allaah kupitia Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam).

Jibu ni kwamba endapo Hadiyth hii itakuwa kweli imesihi basi si jambo ambalo tunavutana. Kipofu huyu alitaka kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amwombee na akaelekea kwa Allaah kwa kuwepo kwake pia yeye (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam), jambo ambalo linafaa. Inafaa kwenda kwa mja mwema ambaye yuhai na ukamuomba akuombee kwa Allaah. Ndani yake hakuna dalili inayojuzisha kufanya Tawassul na kuwaelekea wafu na watu walioko mbali. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alimwamrisha kipofu huyu kumuomba Allaah akubali uombezi wa Allaah juu yake. Huku kunafahamisha kumuomba uombezi Allaah (Ta´ala) pekee. Hadiyth haifahamishi jengine zaidi ya hivi. Haifahamishi kwamba inafaa kufanya Tawassul kwa dhati za viumbe, kuwaita wafu na viumbe vilivyoko mbali.

Wanatumia dalili vilevile kwa Hadiyth za uongo ambapo wanasimulia kwamba eti Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Fanyeni Tawassul kwa dhati yangu. Kwani hakika dhati yangu mbele ya Allaah ni kubwa.”

Hii ni Hadiyth ya uongo ambayo kazuliwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Hivo ndivo alivosema Shaykh-ul-Islaam Ibn Taymiyyah (Rahimahu Allaah)[2].

[1] at-Tirmidhiy (3573).

[2] Majmuu´-ul-Fataawaa (01/319).

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Bayaan Haqiyqat-it-Tawhiyd, uk. 40-41
  • Imechapishwa: 02/04/2019