24. Mtu wa tatu bora anayefuata baada ya Manabii na Mitume

Mtu wa kwanza ni Abu Bakr, kisha ´Umar, halafu ´Uthmaan (Radhiya Allaahu ´anhum). ´Uthmaan (Radhiya Allaahu ´anh) ana fadhila. Allaah amuwie radhi! Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alisema:

“Ni nani atayenunua kisima cha Ruumah na akatundike ndoo yake hapo pamoja na ndoo za waislamu ili apate badala ilio bora Peponi?” at-Tirmidhiy (3703) na an-Nasaa’iy (8063). Nzuri kwa mujibu wa al-Albaaniy katika ”Irwaa’-ul-Ghaliyl” (6/40).

´Uthmaan (Radhiya Allaahu ´anh) akakinunua na akapata ahadi hii kutoka kwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam).

Pindi ´Uthmaan (Radhiya Allaahu ´anh) alipojitolea kwa ajili ya jeshi la ´Usrah alikuja kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na dirhamu elfumoja na akaziweka kwenye miguu yake. ´Abdur-Rahmaan bin Samurah akasema:

“Nilimwona namna Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) anavyozigusa kwenye miguu yake na kusema: “Tokeo leo ´Uthmaan hatodhurika kutokana na anayoyafanya.” Alisema hivo mara mbili.” Ahmad (5/63) na at-Tirmidhiy (3701). Nzuri kwa mujibu wa al-Albaaniy katika ”Swahiyh at-Tirmidhiy” (3/515).

Fadhila nyingine ni kuwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alimtuma kwa Quraysh katika mkataba wa Hudaybiyah ili kutuliza fitina zao. Wengi katika Quraysh walikuwa na nafasi. ´Uthmaan (Radhiya Allaahu ´anh) akaenda kwao. Wakati watu walipotaka kumpa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) mkono wa usikivu na utiifu chini ya mti katika Hudaybiyah, Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akaweka mkono wake wa kuume juu ya mkono wake wa kushoto na akasema:

“Hii ni ya ´Uthmaan.”

Hii ni fadhila yake nyingine. Allaah amuwie radhi!

Alifanya fadhila nyingi, kujitolea kwa hali ya juu na akatoa mali nyingi kwa ajili ya Allaah. Allaah amuwie radhi!

Mpangilio huu Ahl-us-Sunnah wamekubaliana juu yake. Katika Maswahabah wote wanamfadhilisha kwanza Abu Bakr, kisha ´Umar, halafu ´Uthmaan kisha ´Aliy (Radhiya Allaahu ´anhum). Mpangilio huu wa ubora wao ndio mpangilio katika ukhalifah. Mwenye kutukana kitu katika ukhalifah wao ni mpotevu na ni mwenye kupoteza. Shaykh-ul-Islaam anasema kuwa ni mpotevu kuliko punda wa kufugwa[1]. Kulikuwa tofauti kati ya Ahl-us-Sunnah baina ya ´Aliy na ´Uthmaan. Baadhi ya Ahl-us-Sunnah walikuwa wakimfadhilisha ´Aliy juu ya ´Uthmaan. Baadaye Ahl-us-Sunnah wakakubaliana juu ya kwamba wa kwanza ni Abu Bakr, wa pili ni ´Umar, wa tatu ni ´Uthmaan na wanne ni ´Aliy. Wote walikuwa ni makhaliyfah waongofu. Allaah awawie radhi wote!

[1] Tazama “al-´Aqiydah al-Waasitwiyyah” (243).

  • Mhusika: ´Allaamah Rabiy´ bin Haadiy al-Madkhaliy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Qurrat-ul-´Aynayn bi Tawdhwiyh Ma´aaniy ´Aqiydat-ir-Raaziyayn, uk. 37-39
  • Imechapishwa: 15/10/2016