24. Kuamini kuonekana kwa Allaah siku ya Qiyaamah

Imaam Ahmad bin Hanbal (Rahimahu Allaah) amesema:

“Inatakiwa kuamini kuonekana kwa Allaah siku ya Qiyaamah. Kumepokelewa Hadiyth nyingi Swahiyh kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kuhusiana na suala hili.”

MAELEZO

Ahl-us-Sunnah wal-Jamaa´ah wanaamini kwamba waumini watamuona Mola wao kwa macho yao siku ya Qiyaamah.  Imekuja kwenye Qur-aan tukufu:

وُجُوهٌ يَوْمَئِذٍ نَّاضِرَةٌ إِلَىٰ رَبِّهَا نَاظِرَةٌ

“Nyuso siku hiyo zitang´ara – zikimtazama Mola wake.”[1]

لِّلَّذِينَ أَحْسَنُوا الْحُسْنَىٰ وَزِيَادَةٌ

“Kwa wale waliofanya wema watapata mazuri kabisa na ziada.”[2]

Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema kwamba mazuri ni Pepo na ziada ni kuutazama uso wa Allaah (´Azza wa Jall). Kuna dalili nyingi zinazothibitisha hilo. Mtume mkarimu (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Hakika nyinyi mtamuona Mola wenu kama mnavyouona mwezi huu mwandamo – hamtosongamana katika kumuona.”[3]

Hapa kunafananishwa uonekanaji na sio muonaji atachokiona. Yote haya ni maandiko yanayofahamisha kwamba waumini watamuona Mola wao kwenye uwanja wa mkusanyiko siku ya Qiyaamah.

Ahl-ul-Bid´ah wanaona kinyume. Baadhi wamepindukia na wakathibitisha kuonekana duniani na Aakhirah. Kwa msemo mwingine wanasema kuwa baadhi ya watu wanamuona Allaah hapa duniani na watamuona huko Aakhirah. Haya ni maoni walionayo Suufiyyah waliopindukia. Wengine wamechupa mipaka katika kukanusa na matokeo yake wakakanusha kuonekana hapa duniani na huko Aakhirah. Hivi ndivo wanavoona Jahmiyyah na Mu´tazilah wakanushaji.

Ama kuhusu makafiri Allaah amesema juu yao:

كَلَّا إِنَّهُمْ عَن رَّبِّهِمْ يَوْمَئِذٍ لَّمَحْجُوبُونَ

“Sivyo hivyo! Hakika wao Siku hiyo bila shaka watazuiwa wasimuone Mola wao.”[4]

Hawatomuona kabisa. Kumuona ni neema kubwa kabisa miongoni mwa neema.

[1] 75:22-23

[2] 10:26

[3] al-Bukhaariy (554) na Muslim (633).

[4] 83:15

  • Mhusika: ´Allaamah Zayd bin Muhammad al-Madkhaliy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: at-Ta´liyqaat al-Latwiyfah ´alaa Usuwl-is-Sunnah al-Muniyfah, uk. 78-79
  • Imechapishwa: 10/10/2019