24. Chimbuko na chemchem ya ukanushaji

Ukanushaji (التعطيل) ni jambo lililoenea baada ya karne bora – Maswahabah, Taabi´uun na waliokuja baada ya Taabi´uun – ingawa msingi wake ulisimikwa mwisho wa zama za Taabi´uun. Mtu wa kwanza kukanusha ilikuwa al-Ja´d bin Dirham. Alisema:

“Allaah hakumfanya Ibraahiym kuwa kipenzi wa karibu (خليلاً) na wala hakumzungumzisha Muusa maneno ya kikweli.”

Khaalid bin ´Abdillaah al-Qasriy akamuua ambaye Hishaam bin ´Abdil-Malik alimtawalisha ´Iraaq na Shaam. Siku ya idi alitoka akaenda kwenye uwanja wa idi akiwa na mnyororo wa al-Ja´d. Akawakhutubia watu na kuwaambia:

“Enyi watu! Chinjeni! Allaah akubali vichinjwa vyenu. Mimi namchinja al-Ja´d bin Dirham. Anadai kwamba Allaah hakumfanya Ibraahiym kuwa kipenzi wa karibu na wala hakumzungumzisha Muusa maneno ya kikweli.”

Kisha akashuka chini na kumchinja[1]. Hilo lilipitika siku ya ´Iyd-ul-Adhwhaa mwaka wa 119. Kwa mnasaba wa hilo Ibn-ul-Qayyim (Rahimahu Allaah) amesema katika “an-Nuuniyyah”:

Kwa ajili hiyo al-Qasriy akamchinja

al-Ja´d siku ya kuchinja

Kwa sababu amesema kuwa Ibraahiym sio mpenzi Wake wa karibu

wala hakumzungumzisha Muusa maneno ya kikweli

Kila Sunniy akamshukuru kwa uchinjaji huo

Ni kichinjwa kizuri kilichoje alichofanya ndugu yangu!

´Aqiydah yake ikachukuliwa na mtu anayeitwa al-Jahm bin Swafwaan ambaye ananasibishiwa madhehebu ya wakanushaji Jahmiyyah. Yeye ndiye ambaye aliyaeneza madhehebu haya. Akauawa na Salm bin Ahwaz mwaka wa 128 Khurasaan.

Katika karne za 100 vikatarjumiwa vitabu vya kigiriki na vya kirumi katika lugha ya kiarabu na ndipo suala hili likazidi kuwa baya zaidi.

Katika karne ya kufuatia ya 200 kukaenea madhehebu ya Jahmiyyah kwa sababu ya mtu akitambulika kwa jina la Bishr bin Ghayyaath al-Maariysiy na kizazi chake ambacho maimamu waliafikiana juu ya kuwakemea. Wengi wao walionelea kuwa ni makafiri au wapotofu. ´Uthmaan bin Sa´iyd ad-Daarimiy alitunga kitabu akimraddi Bishr al-Mariysiy kwa jina ”Naqdhwu ´Uthmaan bin Sa´iyd ´alaa al-Kaafir al-´Aniyd fiymaa iftaraa ´alaa Allaah min at-Tawhiyd”. Mwenye kusoma kitabu hiki bila ya ushabiki na kwa elimu, ataona zilivyo dhaifu na batili hoja za wakanushaji hawa. Ataona kuwa tafsiri hizi ambazo zinapatikana kwa wengi waliokuja nyuma, kama mfano wa ar-Raaziy, al-Ghazaaliy, Ibn ´Aqiyl na wengineo, si lolote wala si chochote zaidi ya tafsiri mbovu za Bishr.

Ama chemchem ya madhehebu haya, yanatokana na mayahudi, washirikina, wasabai waliopotoka na wanafalsafa. Inasemekana kuwa al-Ja´d bin Dirham alichukua ´Aqiydah hii kutoka kwa Abaan bin Sam´aan, ambaye na yeye alichukua kutoka kwa Twaaluut, ambaye na yeye alichukua kutoka kwa myahudi Labiyd bin al-A´swaam ambaye alimfanyia uchawi Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Isitoshe inasemekana kuwa al-Ja´d anatoka Harraan ambapo kuna wakazi wengi wa washirikina, wasabai na wanafalsafa. Ni jambo lisilokuwa na shaka ya kwamba jamii ina taathira kubwa kwenye ´Aqiydah na tabia ya mtu.

Miongoni mwa ´Aqiydah ya watu hawa hawaamini kuwa Allaah ana sifa zilizothibiti. Wanaona kuwa kuthibitisha sifa kunapelekea Allaah kufanana na viumbe Wake. Sifa wanazothibitisha, ni zile zilizokanushwa, zenye kuegemezwa au zilizopandiana.

Sifa zilizokanushwa ni zile ambazo maana yake iko tupu isiyolingana na Allaah (´Azza wa Jall). Mfano wa hilo ni Allaah ni mmoja. Ina maana ya kwamba hakuna mwingine zaidi Yake.

Sifa zilizoegemezwa sio sifa anazosifiwa kwazo Allaah kama sifa zilizothibiti Kwake. Lakini anasifiwa nazo kwa mnasaba wa kwamba wanasifiwa nazo wengine. Kwa mfano wanasema kuwa Allaah ndiye Mwanzo na ndiye Sababu. Yeye ndiye Mwanzo na Sababu kwa kuzingatia ya kwamba kila kitu ni chenye kutokana na Yeye na sio kwa kuzingatia kwamba mwanzo na sababu ni sifa Zake zilizothibitishwa.

Sifa zilizopandiana ni zile ambazo zinakuwa zenye kukanushwa kwa njia fulani na zinakuwa zenye kuegemezwa kwa njia nyingine. Kwa mfano wanasema kuwa Allaah ndiye wa Mwanzo. Sifa hii kwa upande mmoja ni yenye kukanushwa kwa sababu ina maana kwamba Yeye sio kitu kinachozuka. Kwa upande mwingine ni yenye kuegemezwa kwa sababu vitu vyengine vyote vinakuja baada Yake.

Ikiwa hili ndio chimbuko la ´Aqiydah ya wakanushaji, mtu anaweza kujiuliza ni vipi mtu muumini au mwenye busara anaweza kuichukua na akaacha njia ya wale walioneemeshwa na Allaah – katika manabii, wakweli, mashahidi na watu wema.

[1] Khalqu Af´aal-il-´Ibaad, uk. 69, ya al-Bukhaariy.

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Fath Rabb-il-Bariyyah, uk. 66-68
  • Imechapishwa: 07/05/2020