22. Twawaaf-ul-Wadaa´ [Twawaaf ya kuaga]

130- Atapomaliza kutekeleza haja zake zote na akaazimia kurudi nyumbani, basi ni wajibu kwake kuiaga Nyumba kwa kutufu. Ibn ´Abbaas amesema:

“Watu walikuwa wamezowea kuondoka kupitia sehemu yoyote watakayo. Ndipo Mtume (Swalla ´Allaahu ´alayhi wa sallam) akasema: “Asiondoke yeyote mpaka iwe kitendo chake cha mwisho ni Twawaaf.”[1]

131- Mwanzoni ilikuwa mwanamke mwenye hedhi ni mwenye kuamrishwa kusubiri mpaka atapotwaharika ili aweze kufanya Twawaaf-ul-Wadaa´[2]. Kisha baadaye akaruhusiwa kuondoka nyumbani pasi na kusubiri. Ibn ´Abbaas amesema:

“Mtume (Swalla ´Allaahu ´alayhi wa sallam) amemruhusu mwanamke mwenye hedhi kuondoka nyumbani kabla ya kufanya Twawaaf-ul-Wadaa´ ikiwa hapo mwanzo alitufu Twawaaf-ul-Ifaadhwah.”[3]

132- Ikiwezekana inafaa kwake kubeba maji ya zamzam kiasi anachoweza kwa ajili ya kujipatia baraka kwayo:

“Mtume wa Allaah (Swalla ´Allaahu ´alayhi wa sallam) alikuwa akiyabeba kwenye chombo. Alikuwa akiwamwagia wagonjwa na akiwapa wanywe.”[4]

Bali uhakika wa mambo ni kwamba:

“Alikuwa akituma ujumbe kwenda kwa Suhayl bin ´Amr kutokea al-Madiynah kabla Makkah haijakombolewa: “Tupe maji ya zamzam na wala usikatae.” Hivyo anamtumia vyombo viwili.”[5]

133- Atapomaliza kufanya Twawaaf, basi atatoka nje kawaida kama wanavyotoka watu misikitini. Asitoke kinyumenyume na atangulize mguu wake wa kushoto[6] na huku akisema:

اللهم صل على محمد وسلم اللهم إني أسألك من فضلك

“Ee Allaah! Mswalie Muhammad na msalimishe. Ee Allaah! Nakuomba kutoka katika fadhilah Zako.”

[1] Ameipokea Muslim na wengineo. al-Bukhaariy amepokea mfano wake. Imetajwa katika ”al-Irwaa’” (1086) na Swahiyh Abiy Daawuud” (1747).

[2] Yamethibiti haya katika Hadiyth ya al-Haarith bin ´Abdillaah bin Aws kwa Ahmad na wengineo. Imetajwa katika “Swahiyh Abiy Daawuud” (1748).

[3] Ameipokea Ahmad kwa cheni ya wapokezi Swahiyh yenye kuafikiana na masharti ya al-Bukhaariy na Muslim. Vilevile wamepokea mfano wake, kama ilivyobainishwa katika ”al-Irwaa’” (1067). Ina Hadiyth zengine zenye kuitolea ushahidi kutoka katika Hadiyth ya ´Aaishah. Imetajhwa katika ”Swahiy Abiy Daawuud” (1748).

[4] Ameipokea al-Bukhaariy katika ”at-Taariykh” kutoka kwa ´Aaishah (Radhiya Allaahu ´anhaa. Vilevile ameipokea atTirmidhiy ambaye ameonelea kuwa ni nzuri. Imetajwa katika ”al-Ahaadiyth as-Swahiyhah” (883).

[5] Ameipokea al-Bayhaqiy kwa cheni ya wapokezi ilio nzuri kutoka kwa Jaabir (Radhiya Allaahu ´anh). Ina upooezi wenye kuitolea ushahidi lakini uliokatika, cheni ya wapokezi Swahiyh katika ”al-Muswannaf” (9127) ya ´Abdur-Razzaaq. Ibn Taymiyyah amesema kuwa Salaf walikuwa wakiyapeleka.

[6] Tazama ”al-Kalim at-Twayyib”, uk. 51-52, ya Shaykh-ul-Islaam Ibn Taymiyyah kwa uhakiki wangu.

  • Mhusika: Imaam Muhammad Naaswir-ud-Diyn al-Albaaniy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Manaasik-ul-Hajj wal-´Umrah, uk. 40-41
  • Imechapishwa: 20/07/2018