Ahl-us-Sunnah wal-Jamaa´ah wanaonelea kuwa Qur-aan ni maneno ya Allaah yaliyoteremshwa na hayakuumbwa. Imeanza Kwake na Kwake ndiko itarudi. Amezungumza kwa Qur-aan kihakika. Alimzungumzisha nayo Jibriyl ambapo akashuka nayo kwenye moyo wa Muhammad (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Haya yanathibitishwa na Qur-aan na Sunnah. Miongoni mwa dalili za Qur-aan ni pamoja na maneno ya Allaah (Ta´ala):

وَإِنْ أَحَدٌ مِّنَ الْمُشْرِكِينَ اسْتَجَارَكَ فَأَجِرْهُ حَتَّى يَسْمَعَ كَلاَمَ اللّهِ

”Na ikiwa mmoja wa washirikina akikuomba umlinde, basi mlinde mpaka asikie maneno ya Allaah.”[1]

Bi maana Qur-aan. Allaah (Ta´ala) amesema vilevile:

كِتَابٌ أَنزَلْنَاهُ إِلَيْكَ مُبَارَكٌ لِّيَدَّبَّرُوا آيَاتِهِ وَلِيَتَذَكَّرَ أُوْلُوا الْأَلْبَابِ

“Kitabu Tumekiteremsha kwako chenye baraka ili wapate kuzingatia kwa makini Aayah zake na ili wapate kukumbuka wale wenye akili.”[2]

Amesema (Ta´ala) tena:

وَإِنَّهُ لَتَنزِيلُ رَبِّ الْعَالَمِينَ نَزَلَ بِهِ الرُّوحُ الْأَمِينُ عَلَى قَلْبِكَ لِتَكُونَ مِنَ الْمُنذِرِينَ بِلِسَانٍ عَرَبِيٍّ مُّبِينٍ

“Hakika huu ni uteremsho wa Mola wa walimwengu; ameuteremsha roho mwaminifu [na kuiingiza] kwenye moyo wako ili uwe miongoni mwa waonyaji kwa lugha ya Kiarabu ilio wazi.”[3]

Kuhusiana na dalili za Sunnah, Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Hakuna yeyote awezaye kunichukua kunipeleka kwa watu wake ili nifikishe maneno ya Mola Wangu? Kwani hakika Quraysh wamenizuia kuyafikisha maneno ya Mola Wangu.”[4]

Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alisema kumwambia al-Baraa´ bin ´Aazib:

اللّهُـمَّ أَسْـلَمْتُ نَفْـسي إِلَـيْكَ، وَفَوَّضْـتُ أَمْـري إِلَـيْكَ، وَوَجَّـهْتُ وَجْـهي إِلَـيْكَ، وَأَلْـجَـاْتُ ظَهـري إِلَـيْكَ، رَغْبَـةً وَرَهْـبَةً إِلَـيْكَ، لا مَلْجَـأَ وَلا مَنْـجـا مِنْـكَ إِلاّ إِلَـيْكَ، آمَنْـتُ بِكِتـابِكَ الّـذي أَنْزَلْـتَ وَبِنَبِـيِّـكَ الّـذي أَرْسَلْـت

”Ee Allaah! Nimeisalimisha nafsi yangu Kwako, nimeyaegemeza mambo yangu Kwako, nimeuelekeza uso wangu Kwako, nimeutegemeza mgongo wangu Kwako hali ya kuwa ni mwenye kukutarajia na mwenye kukuogopa, hapana sehemu ya kukimbilia wala ya kujiokoa isipokuwa Kwako. Nimekiamini Kitabu Chako ulichokiteremsha na Nabii Wako Uliyemtuma.”[5]

´Amr bin Diynaar amesema:

“Kabla ya miaka elfu sabini nimekutana na watu wakisema: “Allaah ndiye Muumbaji na vyengine vyote vimeumbwa isipokuwa tu Qur-aan. Qur-aan ni maneno ya Allaah na hayakuumbwa. Imeanza Kwake na Kwake ndiko itarudi.”[6]

Qur-aan imeanza Kwake ina maana ya kwamba Allaah ndiye wa kwanza kuzungumza kwayo. Hapa kuna Radd kwa Jahmiyyah wanaosema kuwa Allaah aliumba maneno katika kitu kingine.

Kwake ndiko itarudi inaweza kuwa na maana mbili:

1- Hakuna mwingine asiyekuwa Allaah mwenye kusifiwa kuwa amezungumza kwa Qur-aan. Kwa msemo mwingine ni kwamba hakuna yeyote anayesifiwa kwamba amezungumza kwayo isipokuwa Allaah pekee. Yeye ndiye ambaye amezungumza kwayo na maneno ni sifa ya mzungumzaji.

2- Qur-aan itanyanyuliwa kwa Allaah (Ta´ala). Imepokelewa katika baadhi ya mapokezi ya kwamba Qur-aan itatoka kwenye misahafu na kwenye vifua na kupanda kwa Allaah. Haya yatapitika pale ambapo watu wataacha kuuitendea kazi Qur-aan kabisa kabisa. Kwa hivyo Allaah ainyanyue kutokana na kuiheshimisha – na Allaah ndiye anajua zaidi.

[1] 09:06

[2] 38:29

[3] 26:192-195

[4] Abu Daawuud (4734), at-Tirmidhiy (2925), an-Nasaa’iy katika ”al-Kubraa’” (7727), Ibn Maajah (201), Ahmad (3/390) na al-Haakim (2/669) ambaye amesema kuwa ni Swahiyh. al-Haytamiy: ”Wapokezi wake ni waaminifu.” (Majma´-uz-Zawaa’id (6/35))

[5] al-Bukhaariy (247) na Muslim (2710).

[6] Tazama ”as-Sunan al-Kubraa” (10/43, 205) ya al-Bayhaqiy na ”at-Tamhiyd” (24/186) ya Ibn ´AbdilBarr.

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Fath Rabb-il-Bariyyah, uk. 63-64
  • Imechapishwa: 04/05/2020