22 – Madhambi yanamnyima mtenda dhambi kupata du´aa ya Mtume

Madhambi yanamnyima yule mtenda dhambi kupata du´aa ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na Malaika. Amesema (Ta´ala):

الَّذِينَ يَحْمِلُونَ الْعَرْشَ وَمَنْ حَوْلَهُ يُسَبِّحُونَ بِحَمْدِ رَبِّهِمْ وَيُؤْمِنُونَ بِهِ وَيَسْتَغْفِرُونَ لِلَّذِينَ آمَنُوا رَبَّنَا وَسِعْتَ كُلَّ شَيْءٍ رَّحْمَةً وَعِلْمًا فَاغْفِرْ لِلَّذِينَ تَابُوا وَاتَّبَعُوا سَبِيلَكَ وَقِهِمْ عَذَابَ الْجَحِيمِ رَبَّنَا وَأَدْخِلْهُمْ جَنَّاتِ عَدْنٍ الَّتِي وَعَدتَّهُمْ وَمَن صَلَحَ مِنْ آبَائِهِمْ وَأَزْوَاجِهِمْ وَذُرِّيَّاتِهِمْ ۚ إِنَّكَ أَنتَ الْعَزِيزُ الْحَكِيمُ وَقِهِمُ السَّيِّئَاتِ ۚ وَمَن تَقِ السَّيِّئَاتِ يَوْمَئِذٍ فَقَدْ رَحِمْتَهُ ۚ وَذَٰلِكَ هُوَ الْفَوْزُ الْعَظِيمُ

“Wale wabebao ´Arshi na walio pembezoni mwake wanasabihi kwa himdi za Mola wao na wanamuamini na wanawaombea msamaha wale walioamini [kwa madhambi yao]: “Mola wetu, umekienea kila kitu kwa huruma na ujuzi! Hivyo basi wasamehe wale waliotubu na wakafuata njia Yako na wakinge na adhabu ya moto uwakao kwa ukali mno! Mola wetu! Waingize katika mabustani yenye kudumu milele ambayo Umewaahidi pamoja na waliotengenea miongoni mwa baba zao, na wake zao, na kizazi chao! Kwani hakika Wewe ni Mwenye nguvu kabisa, Mwenye hekima – na wakinge na matendo maovu, kwani Unayemkinga na maovu siku hiyo hakika Umemrehemu; na huko ndiko kufuzu kukubwa.”[1]

Hakika Allaah (Subhaanah) amemuamrisha Mtume Wake kuwaombea waumini wanaume na waumini wanawake. Hii [iliyoko juu] ni du´aa ya Malaika ambao wanawaombea waumini wenye kutubia na wenye kufuata Kitabu cha Allaah na Sunnah za Mtume Wake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Hawana njia nyenginezo isipokuwa hizi mbili. Kwa ajili hiyo wasiwepo wengine wenye kutaraji kupata maombi haya endapo hawatokuwa na zile sifa zinazotakikana.

[1] 40:7-9

  • Mhusika: Imaam Ibn Qayyim-il-Jawziyyah
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: ad-Daa’ wad-Dawaa’, uk. 75
  • Imechapishwa: 09/01/2018