22. Kutia manuwizi wakati wa kufunga ndoa na wakati wa jimaa

20- Yanayotakiwa kunuiwa kwa ndoa

Mwanaume na mwanamke wanatakiwa kwa kuoana kwao wanuie kujihifadhi nafsi zao kutokamana na kutumbukia katika yale aliyoharamisha Allaah. Kule kufanya kwao tendo la ndoa wanaandikiwa swadaqah kutokana na Hadiyth ya Abu Dharr (Radhiya Allaahu ´anh) aliyesimulia kwamba:

“Kuna watu kutoka katika Maswahabah wa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) walimwambia Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam): “Ee Mtume wa Allaah! Wakwasi wamejinyakulia thawabu tele; wanaswali kama tunavyoswali, wanafunga kama tunavyofunga, wanatoa kwa ziada ya mali zao.” Akasema: “Je, Allaah hakukujaalieni mtayotoa swadaqah? Hakika kwa kila Tasbiyh moja kuna swadaqah, Takbiyr moja kuna swadaqah, Tahliyl moja kuna swadaqah, Tamhiyd moja kuna swadaqah, kuamrisha mema ni swadaqah, kukataza maovu ni swadaqah, kufanya kwake jimaa mmoja wenu ni swadaqah.” Ndipo wakasema: “Ee Mtume wa Allaah! Vipi mmoja wetu atayaendea matamanio yake halafu apate ujira?” Akasema: “Je, mnaonaje lau angeyaweka hayo katika haramu si angelipata dhambi?” Wakasema: “Ndio.” Akasema: “Basi vivyo hivyo endapo atayaweka katika halali anapata ujira.” Halafu akataja mambo mengine ambayo ni swadaqah. Halafu akasema: “Haya yote yanatoshelezwa na Rakaa´ mbili za dhuhaa.”[1]

[1] Ameipokea Muslim (03/82) na siyaaq ni yake, an-Nasaa´iy katika “´Ishrat-un-Nisaa´” (02/78), Ahmad (05/167), (169) na (178) na ziada yote ni yake. Mlolongo wa wapokezi wake ni Swahiyh juu ya masharti ya Muslim. Ziada nyingine ni ya an-Nasaa´iy.

as-Suyuutwiy amesema katika “Idhkaar-ul-Adhkaar”:

“Udhahiri wa Hadiyth ni kwamba jimaa ni swadaqah japokuwa mtu hatonuia kitu.”

Huenda haya yanahusiana na yale matukio yote. Vinginevyo naonelea kuwa ni lazima mtu anuie wakati wa kumuoa mwanamke. Hayo ndio tuliyotaja hapo juu. Allaah ndiye mjuzi zaidi.

  • Mhusika: Imaam Muhammad Naaswir-ud-Diyn al-Albaaniy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Aadaab-uz-Zafaaf, uk. 137-138
  • Imechapishwa: 18/03/2018