22. Himaya ya Mtume (صلى الله عليه وسلم) kuihami Tawhiyd na kufunga kila njia inayopelekea katika shirki

Shaykh-ul-Islaam Muhammad bin ´Abdil-Wahhaab (Rahimahu Allaah) amesema:

1- Allaah (Ta´ala) amesema:

لَقَدْ جَاءَكُمْ رَسُولٌ مِّنْ أَنفُسِكُمْ عَزِيزٌ عَلَيْهِ مَا عَنِتُّمْ حَرِيصٌ عَلَيْكُم بِالْمُؤْمِنِينَ رَءُوفٌ رَّحِيمٌ

”Hakika amekujieni Mtume anayetokana na nyinyi wenyewe. Yanamuhuzunisha yanayokutaabisheni, anakuhangaikieni na kwa waliomuamini ni mpole na mwenye huruma.” (at-Tawbah 09:128)

2- Abu Hurayrah (Radhiya Allaahu ´anh) ameeleza kwamba Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Msizifanye nyumba zenu kuwa makaburi na wala msilifanye kaburi langu kuwa ni lenye kutembelewa mara kwa mara. Niswalieni; kwani hakika swalah zenu hunifikia popote mlipo.”[1]

Ameipokea Abu Daawuud kwa cheni ya wapokezi nzuri na wapokezi wake ni waaminifu.

3- ´Aliy bin al-Husayn alimuona mtu anaenda kwenye kijitundu kilichokuwa mahali pa kaburi la Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ili apate kuingia na kuomba ambapo akamkataza na akasema:

“Hivi nikuhadithie Hadiyth niliyoisikia kutoka kwa baba yangu ambaye na yeye kaisikia kutoka kwa babu yangu Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) wa Allaah ambaye amesema: “Msilifanye kaburi langu kuwa ni lenye kutembelewa mara kwa mara wala nyumba zenu kuwa makaburi. Niswalieni; kwani hakika swalah zenu hunifikia popote mlipo.”[2]

Imepokelewa katika “al-Mukhtaarah”.

MAELEZO

Katika mlango huu mwandishi wa kitabu amebainisha namna ambavyo Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alivyoihami Tawhiyd dhidi ya maneno na matendo ya kishirki. Mlango huu unazungumzia kuihami Tawhiyd na kuziba njia zote zinazopelekea katika shirki. Ndani yake kuna utetezi wa kimaneno na matahadharisho ya shirki na yale yote maneno na matendo yote yanayopelekea huko.

1- Allaah (Ta´ala) amesema:

لَقَدْ جَاءَكُمْ رَسُولٌ مِّنْ أَنفُسِكُمْ عَزِيزٌ عَلَيْهِ مَا عَنِتُّمْ حَرِيصٌ عَلَيْكُم بِالْمُؤْمِنِينَ رَءُوفٌ رَّحِيمٌ

”Hakika amekujieni Mtume anayetokana na nyinyi wenyewe. Yanamuhuzunisha yanayokutaabisheni, anakuhangaikieni na kwa waliomuamini ni mpole na mwenye huruma.”

Huu ni wasifu wake na Ummah wote ndio wanaozungumzishwa na khaswakhaswa Quraysh kwa sababu wao wanamjua na wanajua ukoo wake na kwamba anatokamana na wao. Kuna kisomo kingine kisichokuwa cha kawaida kiko namna hii:

مِّنْ أَنفَسِكُمْ

“… anayetokamana na watukufu wenu… “[3]

Allaah (Ta´ala) amesema:

عَزِيزٌ عَلَيْهِ مَا عَنِتُّمْ

“Yanamuhuzunisha yanayokutaabisheni.”

Bi maana anaudhiwa na jambo lolote linalokudhuruni na linalokutaabisheni. Haya ni kwa sababu ya kukuhurumieni na kukupendeni na kupupia kwake juu ya kuongoka kwenu na kukutahadharisheni na Moto kwa matendo na maneno yake. Ni mpole kwa waumini. Alikuwa na hisia juu yao. Lakini hata hivyo alikuwa ni mkali kwa maadui wa Allaah kwa sababu ya ukafirin na upotevu wao. Mtu aliye na sifa hizi ni wajibu kumfuata na kumpenda, lakini walipindua mambo chini juu na wakamchukia kufikia kiasi cha kwamba wakataka kumuua.

Mtu aliye na sifa hizi hauachi Ummah wake pasi na kuwatakia kheri. Ndio maana kawaamrisha Tawhiyd, akawahimiza watu kuwa na msimamo na kutahadhari kutokamana na shirki na sababu zote zinazopelekea huko. Miongoni mwa aliyoyasema:

“Msipindukie kwangu kama walivyopindukia manaswara kwa ´Iysaa mwana wa Maryam.”

“Nakutahadharisheni na kupetuka mipaka.”

2- Abu Hurayrah (Radhiya Allaahu ´anh) ameeleza kwamba Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Msizifanye nyumba zenu kuwa makaburi na wala msilifanye kaburi langu kuwa ni lenye kutembelewa mara kwa mara. Niswalieni; kwani hakika swalah zenu hunifikia popote mlipo.”

Sehemu inayotembelewa mara kwa mara ni mahali ambapo kunaendewa mara kwa mara na kuomba mtu akiwa mahali hapo, akaswali, akaomba msaada na mfano wa hayo. Hakuingii katika haya kutembelea kaburi la Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) pasi na kulifungia safari, kuchupa mipaka au kuabudu kwenye kaburi hilo.

(Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Msizifanye nyumba zenu kuwa makaburi… “

Bi maana msizifanye kama makaburi ambapo hakuswaliwi wala kusomwa Qur-aan makaburini. Bali kinyume chake swalini na someni Qur-aan katika nyumba zenu. Imekuja katika Hadiyth:

“Zifanyeni baadhi ya swalah zenu katika nyumba zenu na wala msiyafanye kuwa makaburi.”[4]

Ni dalili inayothibitisha kuwa makaburini hakuswaliwi na wala hakusomwi Qur-aan. Swalah zinazoswali nyumbani ni swalah za sunnah.

(Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Niswalieni… “

Amesisitiza (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kumswalia.

3- ´Aliy bin al-Husayn alimuona mtu anaenda kwenye kijitundu kilichokuwa mahali pa kaburi la Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ili apate kuingia na kuomba ambapo akamkataza na akasema:

“Hivi nikuhadithie Hadiyth niliyoisikia kutoka kwa baba yangu ambaye na yeye kaisikia kutoka kwa babu yangu Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) wa Allaah ambaye amesema: “Msilifanye kaburi langu kuwa ni lenye kutembelewa mara kwa mara wala nyumba zenu kuwa makaburi. Niswalieni; kwani hakika swalah zenu hunifikia popote mlipo.”

Imepokelewa katika “al-Mukhtaarah”.

´Aliy bin al-Husayn ni Zayn-ul-´Aabidiyn.

Kumswalia Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kunakuwa kila mahali. Anaweza kuswaliwa mtu akiwa nyumbani, sokoni na njiani. Kumswalia sio kwenye kaburi peke yake. Kwa ajili hii ndio maana ´Aliy bin al-Husayn alimkemea mtu yul. Alimbainishia kwamba kitendo chake hakikuwekwa katika Shari´ah na kwamba anachotakiwa ni yeye kumswalia pasi na kukaa kwenye kaburi lake na kuomba.

Sunnah hii imepokelewa na watu wa nyumbani kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Wote wamebainisha kwamba kuyatembelea makaburi mara kwa mara ni jambo linalopelekea katika shirki. Ikiwa yule aliyelitembelea atasimama hapo kwa muda mrefu, akaswali na akaomba kwenye kaburi hilo basi hilo litampelekea katika shirki na kuchua mipaka. Haya yamekatazwa na Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Wale wenye kuyafanya makaburi kuwa ni mahali pa kuswalia, wakayajengea, wakayaweka chokaa, wayavisha vitambara na nguo ni mambo yanayopelekea kuwafanya wale wasiokuwa na elimu kufikiria kuwa ni yenye kuadhimishwa na kwamba yananufaisha. Yote haya yametokea pamoja na kuwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ameihami Tawhiyd na akatahadharisha kutokamana na shirki.

[1] Abu Daawuud (2042), Ahmad (8790), at-Twabaraaniy katika ”al-Awsatw” (8030) na al-Bayhaqiy katika ”Shu´ab-ul-Iymaan” (4162). Swahiyh kwa mujibu wa al-Albaaniy katika ”Swahiyh-ul-Jaami´” (7226).

[2] Abu Ya´laa (469), ´Abdur-Razzaaq (7826) na Ibn Abiy Shaybah (7542). Ni yenye nguvu kwa mujibu wa al-Albaaniy katika ”Tahdhiyr-us-Saajid” (9).

[3] al-Haakim (02/240).

[4] al-Bukhaariy (432) na Muslim (777).

  • Mhusika: Imaam ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah bin Baaz
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh Kitaab-it-Tawhiyd, uk. 78-80
  • Imechapishwa: 05/10/2018