Kuna damu aina mbili zenye kumtoka aliyefunga:

1- Damu yenye kutoka puani, yenye kutoka kwenye majeraha na damu ya maupele au majipu. Hizi haziathiri funga. Bali swawm ni sahihi.

2- Damu ya ugonjwa inayomtoka mwanamke pia haiathiri funga. Bali swawm yake ni sahihi pamoja na kuendelea kwake kutoka kama ambavo haimzuii kuswali, kutufu Ka´bah na kujamiiana na mumewe. Kwa sababu damu hii haina kidhibiti. Ni damu yenye kuendelea kama kutokwa na damu puani na kwenye majeraha. Wala hakuna dalili inayofahamisha kumzuia kutokamana na ´ibaadah hizi kama ambavo dalili za wazi zimefahamisha kumzuia kutokamana na ´ibaadah hizi kwa sababu ya kuwa na hedhi na damu ya uzazi.

3- Iwapo mfungaji atang´oa jino na akatema ile damu na asiimeze, basi swawm yake ni sahihi. Kwa sababu hakufanya hivo kwa kupenda kwake na wala hakuna dalili ya wazi yenye kuonyesha funga inaathirika kwa jambo hilo au kuiathiri. Kimsingi ni kusihi kwa swawm ya mfungaji isipokuwa kwa dalili inayofahamisha juu ya kuharibika kwake, jambo ambalo hakuna.

4- Haifai kwa mwenye hedhi na damu ya uzazi kufunga. Wanatakiwa kula Ramadhaan na walipe. Wakifunga swawm zao hazitosihi. Wanachuoni wameafikiana juu ya hilo[1]. Imethibiti kwa al-Bukhaariy na Muslim kupitia kwa Mu´aadhah ambaye amesema: “Nilimuuliza ´Aaishah nikasema: “Inakuweje mwenye hedhi analipa swawm na halipi swalah?” ´Aaishah Akasema: “Kwani wewe ni Haruuriyyah?” Nikasema: “Mimi sio Haruuriyyah, bali nauliza tu.” Akasema: “Hayo yalikuwa hakitupata ambapo tunaamrishwa kulipa swawm na hatuamrishwi kulipa swalah.”[2]

Vilevile imethibiti katika “as-Swahiyh” ya al-Bukhaariy kupitia kwa Abu Sa´iyd al-Khudhriy (Radhiya Allaahu ´anh) aliyesimulia kwamba Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Je, anapopata hedhi si haswali wala hafungi?” Tukasema: “Ndio.” Akasema: “Basi huo ndio upungufu wa dini yake.”[3]

Hii ni rehema ya Allaah kwa wanawake. Kwa sababu swalah inakariri mara tano mchana na usiku na hivo kuna uzito kuilipa. Ama kuhusu funga ni ´ibaadah ya kimwaka ambayo haiwi isipokuwa mara moja kwa mwaka na hivyo ndio maana ikawa ni lazima kuilipa na hakuna uzito. Ni jambo lina manufaa kwa mwanamke.

Wakati mwanamke aliyefunga atapopata damu ya hedhi au damu ya uzazi sehemu ya mchana basi swawm yake ya siku hiyo itakuwa yenye kuharibika. Ni mamoja ameipata mwanzoni mwa mchana au mwishoni mwake. Haijalishi kitu hata kama itakuwa muda mchache tu kabla ya jua kuzama. Katika hali hiyo atalazimika kuilipa siku hiyo.

Tunamuomba Allaah aturuzuku Ikhlaasw katika matendo, makusudio mema katika yale tunayoyafanya, nia njema na matendo, ukweli katika maneno na matendo. Kwani hakika Yeye ni Mwingi wa kutoa na mkarimu. Allaah ndiye mwenye kuongoza katika njia iliyonyooka.

Swalah na salamu zimwendee Mtume wetu Muhammad, kizazi chake na Maswahabah zake wote.

[1] Tazama ”al-Mughniy” (03/152).

[2] al-Bukhaariy (321) na Muslim (335).

[3] al-Bukhaariy (304).

  • Mhusika: ´Allaamah ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah ar-Raajihiy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Mukhtaswaru fiy Ahkaam-is-Swiyaam, uk. 34-36
  • Imechapishwa: 23/05/2019