2. Kufunika uso kunachangia kuhifadhi tupu

Miongoni mwa dalili za Qur-aan ni:

1- Kauli ya Allaah (Ta´ala):

وَقُل لِّلْمُؤْمِنَاتِ يَغْضُضْنَ مِنْ أَبْصَارِهِنَّ وَيَحْفَظْنَ فُرُوجَهُنَّ وَلَا يُبْدِينَ زِينَتَهُنَّ إِلَّا مَا ظَهَرَ مِنْهَا ۖ وَلْيَضْرِبْنَ بِخُمُرِهِنَّ عَلَىٰ جُيُوبِهِنَّ ۖ وَلَا يُبْدِينَ زِينَتَهُنَّ إِلَّا لِبُعُولَتِهِنَّ أَوْ آبَائِهِنَّ أَوْ آبَاءِ بُعُولَتِهِنَّ أَوْ أَبْنَائِهِنَّ أَوْ أَبْنَاءِ بُعُولَتِهِنَّ أَوْ إِخْوَانِهِنَّ أَوْ بَنِي إِخْوَانِهِنَّ أَوْ بَنِي أَخَوَاتِهِنَّ أَوْ نِسَائِهِنَّ أَوْ مَا مَلَكَتْ أَيْمَانُهُنَّ أَوِ التَّابِعِينَ غَيْرِ أُولِي الْإِرْبَةِ مِنَ الرِّجَالِ أَوِ الطِّفْلِ الَّذِينَ لَمْ يَظْهَرُوا عَلَىٰ عَوْرَاتِ النِّسَاءِ ۖ وَلَا يَضْرِبْنَ بِأَرْجُلِهِنَّ لِيُعْلَمَ مَا يُخْفِينَ مِن زِينَتِهِنَّ ۚ وَتُوبُوا إِلَى اللَّـهِ جَمِيعًا أَيُّهَ الْمُؤْمِنُونَ لَعَلَّكُمْ تُفْلِحُونَ

“Na waambie Waumini wanawake wainamishe macho yao na wahifadhi tupu zao na wala wasidhihirishe mapambo yao isipokuwa yale yanayodhihirika [kwa kuwa hakuna njia ya kuyaficha]; hivyo waangushe khimari zao mpaka vifuani mwao. Na wasidhihirishe mapambo yao isipokuwa kwa waume zao, baba zao, baba za waume wao, wana wao wa kiume, wana wa kiume wa waume zao, kaka zao, wana wa kiume wa kaka zao, wana wa kiume wa dada zao, wanawake wao [dada zao wa Kiislamu], wale iliyowamiliki mikono yao ya kuume, watumishi wanaume wasio na matamanio [tena kwa wanawake], au watoto ambao [bado] hawaelewi [kitu kuhusu] yanayohusu uke. Na wala wasipige miguu yao [wanapotembea] yajulikane yale wanayoyaficha katika mapambo yao. Na tubuni kwa Allaah nyote, enyi Waumini ili mpate kufaulu!”[1]

Dalili katika Aayah hii yenye kuonesha kuwa ni wajibu kwa mwanamke kufunika uso wake mbele ya wanaume ajinabi ni ifuatayo:

Ya kwanza: Allaah (Ta´ala) amewaamrisha waumini wanawake kuhifadhi tupu zao. Kile kilichoamrishwa kinaamrisha vilevile kile chenye kupelekea katika hilo. Hakuna mtu yeyote mwenye akili timamu anashaka juu ya kwamba kufunika uso kunachangia kuhifadhi tupu. Kwa sababu kuonesha uso kunapelekea wanaume kuutazama, kuangalia uzuri wake na kuburudika nao. Hilo [hatimae] linapelekea katika hili la lile. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Macho yanazini na kuzini kwake ni kule kuangalia… ” mpaka aliposema: “… na tupu ima inasadikisha hilo au kulikadhibisha.”[2]

[1] 24:31

[2] al-Bukhaariy (6243) na Muslim (2657).

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: al-Hijaab, uk. 6-7
  • Imechapishwa: 26/03/2017