18. Radd juu ya utata wa kwamba wanachokusudia kwa uombezi na si kuwaabudu

Sita: Miongoni mwa shubuha zao ni kufungamana kwao na jambo la uombezi kwa vile wanasema: “Sisi hatukusudii kutoka kwa mawalii kwamba watutatulie haja zetu badala ya Allaah. Lakini tunachokusudia kutoka kwao ni kwamba watuombee mbele ya Allaah. Kwa sababu wao ni waja wema na wana nafasi mbele ya Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala). Uombezi ni jambo limethibiti katika Qur-aan na Sunnah. Hiki ndicho tunachokusudia kwao.”

Jibu ni kwamba haya ndio yaleyale yaliyosemwa na washirikina hapo kabla pale walipokuwa wanatoa sababu ya kufungamana kwao na viumbe badala ya Allaah. Allaah (Ta´ala) amesema kuhusu wao:

وَالَّذِينَ اتَّخَذُوا مِن دُونِهِ أَوْلِيَاءَ مَا نَعْبُدُهُمْ إِلَّا لِيُقَرِّبُونَا إِلَى اللَّـهِ زُلْفَىٰ

“Wale waliojichukulia badala Yake walinzi [wakisema:] “Hatuwaabudu isipokuwa ili wapate kutukurubisha kwa Allaah tumkaribie.”[1]

وَيَعْبُدُونَ مِن دُونِ اللَّـهِ مَا لَا يَضُرُّهُمْ وَلَا يَنفَعُهُمْ وَيَقُولُونَ هَـٰؤُلَاءِ شُفَعَاؤُنَا عِندَ اللَّـهِ

“Wanaabudu badala ya Allaah ambavyo haviwadhuru wala haviwanufaishi na huku wanasema: “Hawa ni waombezi wetu mbele ya Allaah.”[2]

Uombezi ni haki. Lakini ni milki ya Allaah pekee:

قُل لِّلَّـهِ الشَّفَاعَةُ جَمِيعًا ۖ لَّهُ مُلْكُ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ

”Sema: “Uombezi wote ni wa Allaah pekee – ni Wake pekee ufalme wa mbingu na ardhi.”[3]

Uombezi unaombwa kutoka kwa Allaah na si kutoka kwa wafu. Allaah ametueleza kwamba uombezi haupatikana isipokuwa kwa sharti mbili:

1- Sharti ya kwanza: Kupatikane idhini ya Allaah kumpa yule mwombeaji. Amesema (Ta´ala):

مَن ذَا الَّذِي يَشْفَعُ عِندَهُ إِلَّا بِإِذْنِهِ

“Nani huyu ambaye anashufai mbele Yake bila ya idhini Yake?”[4]

2- Sharti ya pili: Yule mwenye kuombewa awe miongoni mwa wale ambao Allaah anaridhia maneno na matendo yake. Isitoshe awe katika waumini na wapwekeshaji. Amesema (Ta´ala):

وَلَا يَشْفَعُونَ إِلَّا لِمَنِ ارْتَضَىٰ

“… na wala hawataomba uombezi wowote isipokuwa kwa yule ambaye Amemridhia.”[5]

وَكَم مِّن مَّلَكٍ فِي السَّمَاوَاتِ لَا تُغْنِي شَفَاعَتُهُمْ شَيْئًا إِلَّا مِن بَعْدِ أَن يَأْذَنَ اللَّـهُ لِمَن يَشَاءُ وَيَرْضَىٰ

”Malaika wangapi mbinguni haitowafaa kitu chochote uombezi wao isipokuwa baada ya kuwa Allaah ametolea idhini kwa amtakaye na akaridhia.”[6]

يَوْمَئِذٍ لَّا تَنفَعُ الشَّفَاعَةُ إِلَّا مَنْ أَذِنَ لَهُ الرَّحْمَـٰنُ وَرَضِيَ لَهُ قَوْلًا

“Siku hiyo hautofaa uombezi isipokuwa kwa yule Atakayepewa idhini na Mwinngi wa huruma na akamridhia aseme.”[7]

Allaah hakuruhusu kuomba uombezi kutoka kwa Malaika, Mitume wala masanamu. Kwa sababu hiyo ni milki Yake pekee na vilevile inaombwa kutoka Kwake:

قُل لِّلَّـهِ الشَّفَاعَةُ جَمِيعًا ۖ لَّهُ مُلْكُ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ

”Sema: “Uombezi wote ni wa Allaah pekee – ni Wake pekee ufalme wa mbingu na ardhi.”[8]

Yeye ndiye anampa idhini mwombaji aweze kuombea. Asipompa idhini basi hatotangulia mbele Yake kuombea. Mambo si kama yalivo kwa viumbe ambapo wanaombeana pasi na idhini zao na wakati mwingine wanakubali maombi yao ijapokuwa hawako radhi nayo. Yule kiumbe anayeombwa anahitajia muombezi na wasaidizi na ndio maana wanalazimika kukubali maombi yao japokuwa hawako radhi nayo. Kuhusu Allaah (Subhaanah) ni mkwasi Asiyemuhitajia yeyote. Kinyume chake kila mmoja ni mwenye kumuhitajia Yeye. Jengine ni kwamba kiumbe hajui hali zote za raia wake mpaka afikishiwe khabari. Ama kuhusu Allaah juu ya kila jambo ni mjuzi. Hakuna hali ya kiumbe Wake yeyote inayomfichika. Kwa hiyo hana haja ya mwenye kumfikishia.

Uhakika wa uombezi mbele ya Allaah (Subhaanah) ni kwamba Allaah Mwenyewe ndiye ambaye anawapa watu wa Ikhlaasw ambapo anawasamehe na kuwaghufuria kwa kupitia du´aa ya yule aliyempa idhini kwa ajili ya kumkirimu.

[1] 39:03

[2] 10:18

[3] 39:44

[4] 02:255

[5] 21:28

[6] 53:26

[7] 20:109

[8] 39:44

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Bayaan Haqiyqat-it-Tawhiyd, uk. 33-34
  • Imechapishwa: 28/03/2019