Kunahukumiwa kuwa Ramadhaan imeingia kwa moja kati ya njia mbili:

1- Kwa kuona mwezi mwandamo. Amesema (Ta´ala):

فَمَن شَهِدَ مِنكُمُ الشَّهْرَ فَلْيَصُمْهُ

“Basi atakayeshuhudia miongoni mwenu mwezi [mpya] na afunge  swawm.”

Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Mtakapoona mwezi mwandamo basi fungeni.”

Ameipokea al-Bukhaariy na Muslim.

Si sharti mwezi uonekane na kila mtu. Bali itakuwa ni lazima kwa watu wote kufunga mwezi ukionekana na yule ambaye ushahidi wake unakubaliwa kwa kuingia mwezi.

Ni sharti ili ushahidi wa kuona mwezi uweze kukubaliwa shahidi huyo awe amekwishabaleghe, mwenye akili, muislamu na ambaye khabari zake zinaaminiwa kutokana na uaminifu na macho yake. Kuhusu mdogo mwezi hauthibiti kwa ushahidi wake kwa sababu haaminiwi. Mwendawazimu ana haki zaidi ya kutokuaminiwa. Kafiri pia hauthibiti mwezi kwa ushahidi wake kutokana na Hadiyth ya Ibn ´Abbaas (Radhiya Allaahu ´anhumaa) ambaye amesema:

“Kuna mbedui alikuja kwa Mtume wa Allaah  (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akasema: “Mimi nimeona mwezi mwandamo wa Ramadhaan.” Akasema: “Je, unashuhudia ya kwamba hapana mungu wa kweli isipokuwa Allaah?” Akasema: “Ndio.” Akasema: “Je, unashuhudia kwamba Muhammad ni Mtume wa Allaah?” Akasema: “Ndio.” Akasema: “Ee Bilaal! Watangazie watu wafunge kesho.”

Wameipokea watano isipokuwa Ahmad[1].

Pia mwezi hauthibiti kwa ushahidi wa ambaye haaminiwi kwa sababu anatambulika kwa wongo, kukurupuka au kwa sababu ni mdhaifu wa macho kwa njia ya kwamba hawezi kuuona hivyo mwezi hauthibiti kwa ushahidi wake kwa sababu ya mashaka juu ya ukweli wake au dhana yenye nguvu juu ya wongo wake.

Mwezi wa Ramadhaan unathibiti kwa ushahidi wa mwanamme mmoja. Hilo ni kutokana na maneno ya Ibn ´Umar (Radhiya Allaahu ´anhumaa):

“Watu waliona mwezi mwandamo ambapo na mimi nikamweleza Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kuwa nimeuona. Akafunga na akawaamrisha watu kufunga.”

Ameipokea Abu Daawuud na al-Haakim ambaye amesema iko kwa mujibu wa sharti za Muslim.

Yule ambaye atakuwa na yakini ya kuuona basi ni lazima kwake kuwajuza jambo hilo watawala. Vivyo hivyo kwa yule mwenye kuona mwenzi mwandamo wa Shawwaal na Dhul-Hijjah. Kwa sababu hayo yanapelekea katika ulazima wa kufunga, kufungua na hijah. Kitu ambacho wajibu hautimii isipokuwa kwacho basi nacho ni wajibu. Akiuona peke yake sehemu ya mbali ambapo hawezi kumjulisha mtawala basi atatakiwa kufunga na kujitahidi kufikisha khabari kwa watawala kwa kiasi cha atavoweza.

Kukitangazwa kuthibiti kwa mwezi kupitia mahakama kwa njia ya redio au nyengine basi ni lazima kutendea kazi jambo hilo kwa kuanza na kuisha kwa mwezi katika mwezi wa Ramadhaan au mwezi mwingine. Kwa sababu utangazaji kupitia njia ya mahakama ni hoja ya Kishari´ah ambayo ni lazima kuitendea kazi. Kwa ajili hiyo ndio maana Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alimwamrisha Bilaal kuwatangazia watu juu ya kuthibiti kwa mwezi ili wafunge wakati ilipothibiti kwake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) juu ya kuanza kwake na akafanya tangazo hilo lenye kuwalazimisha kufunga.

Kukithibiti kuingia kwa mwezi uthibitikaji wa Kishari´ah basi mashukio ya mwezi hayana mazingatio yoyote. Kwa sababu Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amefungamanisha hukumu kwa kuonekana kwa mwezi na si kwa mashukio yake. Amesema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Mtakapouona mwezi basi fungeni na mtakapouona fungueni.”

Ameipokea al-Bukhaariy na Muslim.

Vilevile amesema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Watu wawili waislamu wakitoa ushahidi basi fungeni na fungueni.”

Ameipokea Ahmad[2].

[1] Ibn Khuzaymah na Ibn Hibbaan wameisahihisha. Lakini ina kasoro ya Irsaal.

[2] Cheni ya wapokezi wake haina neon pamoja na kwamba kuna tofauti juu yake. Pamoja na hivo ina shawahidi kwa Abu Daawuud. ad-Daaraqutwniy amesema:

”Cheni ya wapokezi wake ni yenye kuungana na Swahiyh.”

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Majaalis Shahr Ramadhwaan, uk. 21-22
  • Imechapishwa: 10/04/2020