17. Ni ipi hukumu ya aliyechelewesha kulipa mpaka akaingiliwa na Ramadhaan nyingine?

Swali 17: Ni ipi hukumu ya ambaye aliacha kulipa swawm ya Ramadhaan mpaka akaingiliwa na Ramadhaan ilio baada yake ilihali hakuwa na udhuru?  Je, inatosha kwake kutubia pamoja na kulipa au ni lazima vilevile kutoa kafara?

Jibu: Ni lazima kwake kutubia kwa Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala) na kulisha masikini kwa kila siku moja aliyoacha pamoja na kulipa funga. Kafara ni nusu ya pishi kwa kipimo cha ile pishi ya Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kwa kile chakula kilichozoeleka kuliwa katika nchi kama mfano wa tende, ngano, mchele au vyenginevyo. Kiwango chake ni 1,5 kg kwa njia ya kukadiria. Hana kafara nyingine zaidi ya hiyo. Hivo ndivo walivyofutu baadhi ya Maswahabah (Radhiya Allaahu ´anhum) akiwemo Ibn ´Abbaas (Radhiya Allaahu ´anhumaa).

Lakini kama alikuwa na udhuru kwa mfano mgonjwa au msafiri au mwanamke alikuwa na udhuru kama mfano wa ujauzito au kunyonyesha ambapo angelifunga basi angelihisi uzito, hakuna kinachomlazimu zaidi ya kulipa.

  • Mhusika: Imaam ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdllaah bin Baaz
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: As-ilah Muhimmah tata´alaqah bisw-Swiyaam, uk. 23-24
  • Imechapishwa: 29/04/2019