Haya ni machache katika sifa za wanachuoni kwake. Nimekomeka kutaja baadhi tu ya wanachuoni wanaojulikana kutokana na umaarufu wao kwa watu wote na kwa sababu nataka kubainisha haya kwa ufupi. La sivyo maneno ya kumsifu na kumtapa ni mengi sana.

Hivi sasa wasomaji wetu wapendwa wamejua ni maoni yepi wanachuoni hawa wako nayo na ni nafasi ipi Imaam huyu mtukufu yuko nayo, ambaye ametumia umri wake katika kuinusuru Dini ya Allaah. Umri wake ni zaidi ya miaka sabini na bado yuko katika mfumo huu; anailinda Dini ya Allaah kutokamana na dhana za watu wa batili, tafsiri mbovu za wajinga na upotoshaji wa waliopindukia.

Kadhalika msomaji amebainikiwa kupata kuona upotevu wa mwenye kumtia aibu, kumponda na kumsema vibaya juu ya Dini na mfumo wake. Hata hivyo ni jambo lisilowezekana kwa watu hawa wajinga kumsema vibaya na kuwatahadharisha wale wanaowasema vibaya baadhi ya Mitume wa Allaah, kama mfano wa Aadam na Muusa (´alayhimaas-Salaam), na kuwaponda Maswahabah wa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam), kama ´Uthmaan, Abu Dharr, Mu´aawiyah, ´Amr bin al-´Aasw na wengineo, kuwakufurisha Waislamu, kusema kuwa Qur-aan imeumbwa na kukusanya Bid´ah tele na upotevu mwingi. Shaykh Rabiy´ ameulekeza mshale wake dhidi ya Ahl-ul-Bid´ah wadh-Dhwalaal, lakini kitu walichokifanya ilikuwa ni kumdharau na kumponda ili kwa maneno yao ya kupamba waweze kuwadanganya watu Waislamu wajinga. Wao ni kama jinsi alivyosema Shaykh ´Abdul-Latwiyf Aal ash-Shaykh:

“Miongoni mwa ada za Ahl-ul-Bid´ah pale wanapokosa hoja na wakakosa upenyo, hujipoza kwa kutaja mapungufu ya Ahl-us-Sunnah, kuwasema vibaya na kujisifu wao wenyewe.”

Ndugu wapendwa!

Tahadhari kumsema Muislamu kwa kitu asichokuwa nacho. Usimsemi Muislamu vibaya bila ya hoja wala dalili. Kumbuka Kauli ya Allaah (Ta´ala):

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا إِن جَاءَكُمْ فَاسِقٌ بِنَبَإٍ فَتَبَيَّنُوا أَن تُصِيبُوا قَوْمًا بِجَهَالَةٍ فَتُصْبِحُوا عَلَىٰ مَا فَعَلْتُمْ نَادِمِينَ

“Enyi walioamini! Anapokujieni fasiki kwa habari yoyote, basi pelelezeni msije mkawasibu watu kwa ujinga, mkawa kuwa wenye kujuta juu ya ambayo mmeyafanya.” (49:06)

Ndugu mpendwa! Tambua ya kwamba miongoni mwa alama za Ahl-ul-Bid´ah na wapotevu ni kuwasema vibaya wanachuoni wanaopita katika mfumo wa waliotangulia. Kuhusiana na suala hili kumekuja mapokezi mengi kutoka kwa maimamu wa Sunnah. Baadhi yake ni haya yafuatayo:

Abu Zur´ah (Rahimahu Allaah) amesema:

“Ukimuona mtu kutoka Kuufah anamsema vibaya Sufyaan ath-Thawriy na Zaaidah, basi usiwe na shaka ya kwamba ni Raafidhwiy. Ukimuona mtu kutoka Shaam anamsema vibaya Mak-uul na al-Awzaa´iy, basi usiwe na shaka ya kwamba ni Naaswibiy. Ukimuona mtu kutoka Khuraasaan anamsema vibaya ´Abdullaah bin al-Mubaarak, basi usiwe na shaka ya kwamba ni Murjiy. Tambua ya kuwa mapote yote haya yana umoja juu ya kumchukia Ahmad bin Hanbal, kwa kuwa wote hawa amewapiga kwenye mioyo yao kwa mshale usiopona.”[1]

Nu´aym bin Hammaad amesema:

“Ukimuona mtu kutoka Iraaq anamsema vibaya Ahmad bin Hanbal, basi tilia mashaka Dini yake. Ukimuona mtu kutoka Baswrah anamsema vibaya Wahb bin Jariyr, basi tilia mashaka Dini yake. Ukimuona mtu kutoka Khuraasaan anamsema vibaya Ishaaq bin Raahawayh, basi tilia mashaka Dini yake.”[2]

Abu Ja´far Muhammad bin Haaruun al-Mukhramiy al-Fallaas amesema:

“Ukimuona mtu anamsema vibaya Ahmad bin Hanbal, basi tambua kuwa ni mtu wa Bid´ah mpotevu.”[3]

Abu Haatiym ar-Raaziy amesema:

“Ukimuona mtu kutoka Raaz au kutoka sehemu nyingine anamchukia Abu Zur´ah, basi tambua kuwa ni mtu wa Bid´ah.”[4]

Abu Haatiym amesema pia:

“Moja ya alama za Ahl-ul-Bid´ah ni kuwasema vibaya Ahl-ul-Athar.”[5]

Imaam Abu ´Uthmaan as-Swaabuuniy amesema:

“Alama ya watu wa Bid´ah ilio wazi kabisa kwa wafuasi wao na ishara yao ya wazi ni chuki yao kubwa dhidi ya wale wanaoeneza mapokezi ya Mtume ya (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) pamoja na kuwadharau na kuwaponda.”[6]

Abu Daawuud amesema katika shairi lake lililotangaa:

“Ole wako juu ya watu wanaocheza na dini yao ambapo ukawatukana na kuwaponda Ahl-ul-Hadiyth.”

as-Safaariyniy amesema:

“Hatuko kwa ajili ya kutaja hadhi ya Ahl-ul-Hadiyth, kwa kuwa hadhi yao inajulikana, athari zao ni nyingi na fadhilah zao ni nyingi. Hivyo yule mwenye kuwaponda, ni mbovu na ni mpungufu, na mwenye kuwachukia, ni katika kibaraka cha kundi la Iblisi.”[7]

Kwa haya nimekusanya baadhi ya sifa za wanachuoni kwa ´Allaamah na Shaykh Rabiy´ kwa yule mwenye kutafuta haki na ni mwenye kupenda Sunnah na watu wake. Kitabu kimeisha kwa haya na tunamuomba Allaah mwisho mwema na swalah na salamu zimwendee Mtume wetu Muhammad, ahli zake na Maswahabah zake.

Imeandikwa na Abu ´Abdillaah Khaalid bin Dhwahawiy ad-Dhwafayriy

Kazi hii ilikwisha usiku wa tarehe 28 Rabiy´-ul-Awwal, 1424

[1] Twabaqaat-ul-Hanaabilah (1/199-200).

[2] Taariykh Baghdaadiy (6/348) na Taariykh Dimashq (8/132)

[3] Utangulizi wa ”al-Jarh wat-Ta´diyl”, uk. 308-309, na ”Taariykh Dimashq” (5/294)

[4] Taariykh Baghdaadiy (10/329) na ”Taariykh Dimashq” (38/31)

[5] ”as-Sunnah” (1/1079) ya al-Laalakaaiy.

[6] ´Aqiydat-us-Salaf (101).

[7] Liwaaih-ul-Anwaar (2/355).

  • Mhusika: Shaykh Khaalid bin Dhwahwiy adh-Dhwafayriy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: http://www.rabee.net/ar/sharticles.php?cat=12&id=57
  • Imechapishwa: 09/12/2019