16. Tofauti za Salaf na Khalaf

Kwa kufupiliza mtu anaweza kusema kwamba Maswahabah ni kweli walitofautiana, lakini walikuwa wakikemea tofauti na wakijiepusha nazo kadiri na uwezo. Hayo hayafanywi na wale wenye kufuata kichwa mchunga japokuwa wanaweza kujiepusha na kiasi kikubwa cha tofauti. Matokeo yake hawaafikiani, hawajibidishi juu ya jambo la umoja. Bali uhakika wa mambo ni kwamba wanakubaliana na tofauti. Kwa hiyo tofauti kati ya pande mbili hizo ni kubwa sana.

Ama tofauti inapokuja katika mtazamo wa athari iko wazi. Pamoja na tofauti za Maswahabah (Radhiya Allaahu ´anhum) katika mambo ya mataga, walikuwa ni wenye kuchunga sana jambo la umoja na ni wenye kujiepusha ipasavyo na mambo yatakayokuja kuwatenganisha na kuleta mpasuko. Kwa mfano wako katika wao ambao walikuwa wanaonelea kuwa imewekwa katika Shari´ah kusoma Basmalah kwa sauti ya juu kabla ya kuanza kusoma al-Faatihah, wengine wanaona kuwa hilo halikuwekwa katika Shari´ah. Baadhi yao wanaona kuwa imewekwa katika Shar´ah kunyanyua mikono, wengine hawaonelei kufanya hivo. Baadhi ya wengine wanaona kuwa wudhuu´ unachenguka kwa kumgusa mwanamke, wengine hawaonelei hivo. Pamoja na haya yote walikuwa wote wakiswali nyuma ya imamu mmoja. Hakuna yeyote ambaye alikuwa akidharau kuswali nyuma ya imamu ambaye ana mtazamo kinyume na yeye.

Ama wale wanaofuata kichwa mchunga tofauti zao ni kinyume kabisa na hivo. Miongoni mwa athari yake ni kwamba waislamu walitofautiana katika nguzo kubwa baada ya shahaadah, nayo si nyingine ni swalah. Walikataa kuswali nyuma ya imamu mmoja kwa hoja kwamba swalah ya imamu huyo ni batili au angalau kwa uchache imechukizwa. Haya tumeyaona wenyewe na kuyasikia[1]. Vipi wasifanye hivo ilihali baadhi ya vitabu vya madhehebu ndivo vyenye kusema kuwa swalah yake imechukizwa au ni batili? Natija ya hilo ikapelekea kukuta Mihraab nne kwenye msikiti mmoja mbapo kila mmoja anawaswalisha wafuasi wa madhehebu yake na wakati mwingine unakuta wengine wanamsubiria imamu wao ilihali imamu wa madhehebu mengine amesimama yuko anaswali!

Bali tofauti imefikia pabaya zaidi kwa baadhi ya wale wenye kufuata kichwa mchunga. Wako ambao wanakataza kuoana kati ya Hanafiyyah na Shaafi´iyyah. Halafu kukatolewa fatwa kutoka kwa baadhi ya wanachuoni wa Hanafiyyah, mtu huyo anaitwa “muftiy wa watu na majini”, ambaye akajuzisha ndoa kama hiyo kwa sababu mwanamke wa Shaafi´iyyah ana hukumu moja kama mwanamke wa kiyahudi na wa kinaswara[2]. Hiyo ina maana japo si moja kwa moja kwamba mwanaume wa Shaafi´iyyah hawezi kumuoa mwanamke wa Hanafiyyah, kama ambavo haijuzu kwa mwanaume wa kiyahudi au wa kinaswara kumuoa mwanamke wa Kiislamu.

Hii mifano miwili ni michache tu katika mifano mingi. Inamwekea wazi kabisa yule mwenye busara athari mbaya inayotokana na mambo ya tofauti za wale waliokuja nyuma na uendelevu juu yake, kinyume na tofauti za Salaf. Tofauti za Salaf hazikuwa na athari yoyote mbaya kwa Ummah. Kwa ajili hiyo wao si wenye kuguswa na Aayah zinazokataza kutofautiana katika dini tofauti na wale waliokuja nyuma. Allaah atuongoze sote katika njia Yake iliyonyooka.

[1] Rejea katika mlango wa pili katika kitabu “Maa laa yajuuz fiyh-il-Khilaaf”, uk. 65-72, utapata mifano mingi wa yale tuliyoashitia na namna wanachuoni wa al-Azhar walivyotumbukia katika mambo kama hayo.

[2] al-Bahr ar-Raa-iq.

  • Mhusika: Imaam Muhammad Naaswir-ud-Diyn al-Albaaniy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Swifatu Swalaat-in-Nabiy, uk. 57-59
  • Imechapishwa: 22/01/2019