Swali 152: Tunauliza kuhusu jambo lililoenea katika miji mingi ya Kiislamu. Nalo ni yale mambo yanayofanywa na wafiwa wa maiti baada ya kumaliza kumzika maiti wao. Wanatayarisha banda la mahema au kitu kingine na wafiwa wa maiti wanakusanyika ndani yake baada ya kuyatengeneza katika moja ya viwanja au mitaani. Lengo inakuwa kuwapokea wanaokuja kutoa mkono wa pole, kunywa kahawa, chai na vyenginevyo. Tukiongezea kumleta msomaji anayekuja kusoma Qur-aan kwa malipo. Isipowezekana basi hutumia kifaa cha rekodi kwa ajili ya kusikiliza Qur-aan. Katika usiku wa tatu jambo la kufanya chakula linakuwa lenye kutimia kwa wote. Ni yepi maelekezo yako? Je, inafaa kushiriki ndani yake[1]?

Jibu: Kufanya rambirambi kwa sura kama hii ni Bid´ah na haijuzu kuifanya wala kushiriki ndani yake. Imethibiti kutoka kwa Jariyr bin ´Abdillaah al-Bajaliy (Radhiya Allaahu ´anh) ambaye ameeleza:

“Tulikuwa tukizingatia kukusanyika nyumbani kwa maiti na kutengeneza chakula baada ya kuzika ni katika kuomboleza.”[2]

Ameipokea Imaam Ahmad kwa cheni ya wapokezi Swahiyh.

Sunnah ni kuwatengenezea chakula wafiwa wa maiti kitachotoka kwa jamaa na majirani zao. Hayo ni kutokana na yale yaliyothibiti kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kwamba aliwaambia familia yake wakati alipofikiwa na khabari za kufa kwa Ja´far bin Abiy Twaalib (Radhiya Allaahu ´anh):

“Watengenezeeni familia ya Ja´far chakula. Kwani hakika wamefikwa na kitu kinachowashughulisha.”[3]

Ameipokea Imaam Ahmad na watunzi wa as-Sunan kwa cheni ya wapokezi Swahiyh.

[1] Majmuu´-ul-Fataawaa (13/395-396).

[2] Ahmad (6866) na Ibn Maajah (1612).

[3] Ahmad (1754), Ibn Maajah (1610), at-Tirmidhiy (998) na Abu Daawuud (3132).

  • Mhusika: Imaam ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah bin Baaz
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Ahkaam-ul-Janaa-iz, uk. 111-112
  • Imechapishwa: 25/01/2022