150. Kufanya chakula kutoka katika pesa za maiti

Swali 150: Baadhi ya watu hufanya chakula na vichinjwa wakati anapofariki mmoja katika jamaa zao. Thamani ya chakula hichi inatolewa kutoka katika pesa za aliyekufa. Ni ipi hukumu ya hilo? Je, ni inawalazimu warithi kutekeleza wasia huu ikiwa maiti aliacha anausia kufanya mfano wa karamu kama hii baada ya kufa kwake[1]?

Jibu: Wasia wa kufanya chakula baada ya kufa ni Bid´ah na ni miongoni mwa matendo ya kipindi cha kikafiri. Vivyo hivyo ni jambo ovu na lisilojuzu kwa wafiwa wa maiti kufanya chakula kilichotajwa ijapo ni pasi na wasia. Imethibiti kutoka kwa Jariyr bin ´Abdillaah al-Bajaliy (Radhiya Allaahu ´anh) ambaye amesema:

“Tulikuwa tukizingatia kukusanyika nyumbani kwa maiti na kutengeneza chakula baada ya kuzika ni katika kuomboleza.”[2]

Ameipokea Imaam Ahmad kwa cheni ya wapokezi nzuri.

Isitoshe kufanya hivo ni kwenda kinyume na yale aliyoweka Allaah katika Shari´ah katika kuwasaidia wafiwa wa maiti kuwatengenezea chakula kwa sababu ni wenye kushughulishwa na msiba. Imethibiti kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kwamba alipofikiwa na khabari za kufa shahidi kwa Ja´far bin Abiy Twaalib katika vita vya Mu´tah alisema kuiambia familia yake:

“Watengenezeeni familia ya Ja´far chakula. Kwani hakika wamefikwa na kitu kinachowashughulisha.”[3]

[1] Majmuu´-ul-Fataawaa (13/390).

[2] Ahmad (6866) na Ibn Maajah (1612).

[3] Ahmad (1754), Ibn Maajah (1610), at-Tirmidhiy (998) na Abu Daawuud (3132).

  • Mhusika: Imaam ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah bin Baaz
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Ahkaam-ul-Janaa-iz, uk. 108-109
  • Imechapishwa: 24/01/2022