15. Watu wote hawawezi kuwa wenye kupatia

Huenda mtu akasema kuwa maneno ya Imaam Maalik yanayosema kwamba haki ni moja pekee yanatofautiana na yale yaliyotajwa katika kitabu cha a-Razqaa “al-Madkhal al-Fiqhiy”. Imekuja ifuatavyo:

“Ja´far al-Mansuur na ar-Rashiyd walikuwa wakitamani kuyafanya madhehebu ya Imaam Maalik na kitabu chake “al-Muwattwa´” kuwa ni kanuni ya dola ya ´Abbaasiyyah. Lakini hata hivyo Maalik akawakataza na akasema: “Maswahabah wa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) walitofautiana katika mambo ya ki-Fiqh. Walikuwa ni wenye kufarikiana katika miji mbalimbali na wote walikuwa wamepatia.”[1]

Kisa hiki ni chenye kutambulika kwa Imaam Maalik (Rahimahu Allaah). Lakini hata hivyo nyongeza mwishoni inayosema “wote walikuwa ni wenye kupatia” sijui kuwa ina msingi wowote katika mapokezi na vyanzo nilivyosoma. Isipokuwa tu upokezi mmoja peke yake ambao kaupokea Abu Nu´aym katika “Hilyat-ul-Awliyaa”[2] ambao katika cheni ya upokezi wake yuko mtu anayeitwa al-Miqdaam bin Daawuud. adh-Dhahabiy amemtaja katika “ad-Dhwu´afaa´”. Pamoja na hivyo tamko lake linasema:

“… kila wamoja walikuwa wakiona kuwa wao ndio wamepatia.”

Ni dalili inayoonyesha kuwa upokezi unaosema “wote walikuwa wamepatia” katika “al-Madkhal” umezuliwa. Ni vipi mambo yatakuwa sivyo ilihali yanaenda kinyume na yale waliyopokea wapokezi waaminifu kutoka kwa Imaam Maalik juu ya kwamba haki ni moja pekee? Hivyo ndivyo walivyokuwa wakionelea maimamu wote katika Maswahabah, Taabi´uun, wale maimamu wane na wengineo. Ibn ´Abdil-Barr amesema:

“Lau usawa ungelikuwa katika pande mbili zinazopingana, basi Salaf baadhi wasingeliwaweka makosani wengine katika Ijtihaad, hukumu na fataawaa zao. Nadharia inakataa kitu na kinyume chake vyote viwili viwe sawa. Mshairi amepatia pale aliposema:

Kuthibitisha vinyume viwili wakati mmoja

ni jambo baya kabisa ambalo ni muhali”[3]

Ikishathibiti kuwa upokezi huu kutoka kwa imamu ni batili, mtu anaweza kujiuliza ni kwa nini imaam alimkatalia al-Mansuur kuwakusanya watu juu ya kitu kitabu “al-Muwattwaa´”. Jibu zuri nililopata ni ule upokezi uliotajwa na Haafidhw Ibn Kathiyr katika “Sharh Ikhtiswaar ´Uluum-il-Hadiyth”. Ndani yake Imaam Maalik mwenyewe amepambanua kwa kusema:

“Watu wamekusanya na wameyasoma mambo ambayo mimi sijayasoma.”[4]

Hayo ni kutokana na ukamilifu wa elimu na inswafu yake, kama alivosema Ibn Kathiyr (Rahimahu Allah).

Kwa msemo mwingine ni kwamba imethibiti kuwa tofauti zote ni shari na sio rehema. Zipo baadhi ya tofauti ambazo mtu atafanyiwa hesabu kwazo, kama zile tofauti za wale mashabiki wenye kufuata kichwa mchunga madhehebu, kinyume na tofauti zengine, kama mfano tofauti za Maswahabah na wale maimamu waliowafuata. Hivyo imedhihiri kuwa tofauti za Maswahabah sio kama tofauti za wale wenye kufuata kichwa mchunga.

[1] al-Madkhal al-Fiqhiy (1/89).

[2] Hilyat-ul-Awliyaa (6/332).

[3] Ibn ´Abdil-Barr katika ”al-Jaamiy´” (2/88).

[4] Sharh Ikhtiswaar ´Uluum-il-Hadiyth, uk. 31

  • Mhusika: Imaam Muhammad Naaswir-ud-Diyn al-Albaaniy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Swifatu Swalaat-in-Nabiy, uk. 56-57
  • Imechapishwa: 22/01/2019