1- Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Miongoni mwa mambo ambayo watu waliyadiriki katika maneno ya utume wa kwanza: Ikiwa huna haya basi fanya utakalo.”

2- Ni wajibu kwa mwenye busara kuwa na haya. Haya ndio msingi wa akili na mti wa kheri. Kinyume chake ndio msingi wa ujinga na kuenea kwa shari. Haya inaashiria busara na kinyume chake kunaashiria ujinga.

3- Ibn Mas´uud amesema:

“Kitu chenye kutia uchungu zaidi kwa muumini ni uchafu.”

4- Haya ina maana ya kujiepusha na sifa zenye kuchukiwa.

5- Haya imegawanyika aina mbili:

Ya kwanza: Mtu kuona haya kwa Allaah wakati wa dhambi.

Ya pili: Mtu kuona haya kwa viumbe kwa maneno na matendo wanayoyachukia.

6- Haya yote ni yenye kusifiwa. Hata hivyo kuna haya ambayo ni ya wajibu na nyingine nzuri. Haya ya wajibu ni kuacha vile Allaah alivyoharamisha na haya nzuri ni kuacha vile watu wanavyochukia.

7- Haya ni katika imani na muumini ataingia Peponi. Uchafu ni katika utovu wa adabu na utovu wa adabu ni Motoni. Isipokuwa ikiwa kama Allaah atamfadhilisha na akamuokoa kutokamana na rehema Zake.

8- Mtu akiwa na haya sababu za kheri zinakuwa kwake. Kama ambavyo sababu za kheri zinapotea kwa mtu asiyekuwa na haya ilihali sababu za shari ndizo zinachukua nafasi. Haya ndio kizuizi kati ya mtu na dhambi zote. Pindi haya inakuwa na nguvu maasi yanadhoofika. Pindi haya inadhoofika maasi yanakuwa na nguvu.

9- Zayd bin Thaabit amesema:

“Mtu asiyestahi kwa watu hamstahi Allaah.”

10- Ni wajibu kwa aliye na busara kujizoeza kuwaoenea watu haya. Miongoni mwa baraka kubwa ni mtu kujizoeza kuwa na tabia njema na kujiepusha na sifa mbaya. Kama ambavyo miongoni mwa baraka kubwa za haya ni mtu kuuepuka Moto kwa kujiepusha na yale Allaah aliyoharamisha.

Haya ikiwa na nguvu heshima huhifadhika, yale mabaya hufichika na yale mazuri huonekana. Mwenye kupoteza haya yake hupoteza furaha yake. Mwenye kupoteza furaha yake hushuka machoni mwa watu na huchukiwa. Anayechukizwa huudhi. Mwenye kuudhi huhuzunisha. Ambaye anahuzunisha anapoteza akili yake. Mwenye kupoteza akili husema mabaya yake mengi kuliko mazuri yake. Hakuna dawa kwa asiyekuwa na haya. Asiyekuwa na uaminifu hana haya. Asiyekuwa na udugu hana haya. Aliye na haya ndogo hufanya na kusema atakacho.

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Hibbaan al-Bustiy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Rawdhat-ul-´Uqalaa’ wa Nuzhat-ul-Fudhwalaa’, uk. 56-59
  • Imechapishwa: 12/11/2016