1- Ulimi ni mnyama mkali mwenye kuuma. Mwenye nao akiunyamazisha, anasalimika. Akiuacha, unamuuma. Uongo unafichuka kupitia mdomo. Aliye na busara haingilii kitu asichokijua asije kutuhumiwa kwa kitu asichokijua. Kiongozi cha madhambi ni uongo. Uongo unaonyesha mambo mabaya na unaficha mambo mazuri. Haifai kwa mtu kueneza kitu pale tu anapokisikia. Anayesimulia kila anachokisikia anatoa rai yake na anaharibu uaminifu wake.

2- Ibn Mas´uud amesema:

“Inatosha kwa muumini kuwa mwongo kuhadithia kila anachokisikia.”

3- ´Iysaa bin Maryam (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Pepo kwa yule anayeuchunga ulimi wake, ana nyumba pana na analia juu ya makosa yake.”

4- Ukweli unamnyanyua mtu duniani na Aakhirah na uongo unamshusha duniani na Aakhirah. Lau ukweli usingelikuwa na sifa nzuri yoyote zaidi ya kwamba uongo wa mtu unasadikishwa na kuonekana kuwa ni ukweli kwa wenye kuusikia, ingelitosha kwa mwenye akili kuufanyisha mazoezi ulimi wake juu ya kuzungumza ukweli na kujiepusha na uongo. Katika baadhi ya nyakati ni bora kunyamaza kuliko kuzungumza. Kila kunaposemwa makosa ni bora kunyamaza.

5- ´Umar bin al-Khattwaab amesema:

“Mja hatoonja uhakika wa imani mpaka aache mizozo hata kama amepatia na aache kusema uongo wakati anapotania pindi anapojua kuwa atawachekesha watu endapo atafanya hivo.”

6- ´Abdullaah bin ´Amr amesema:

“Achana na kisichokuhusu. Usizungumze juu ya kitu kisichokuhusu. Uchunge ulimi wako kama unavyozichunga pesa zako.”

7- Haifai kwa mwenye busara kupuuzisha ulimi. Anayezungumza sana hutumbukia katika makosa mengi. Makosa yanaweza kuwaathiri wengine na hatimaye mtu akamtumbukia katika kitu ambacho hawezi kuokoka nacho.

8- Donda la ulimi haliponi na kile inachokata hakirudi sehemu yake. Pindi neno linapoutia moyo jeraha haliponi isipokuwa baada ya muda mrefu na haliponi isipokuwa baada ya matibabu ya kisawa sawa.

9- Kuna watu wasiotukuzwa isipokuwa kwa ndimi zao na kuna watu wenye kutwezwa kwa ajili ya ndimi zao. Kwa hiyo ni wajibu kwa mwenye busara kutokuwa miongoni mwa wale wenye kutwezwa.

10- Ibn Siyriyn amesema:

“Uongo ni mkubwa zaidi kuliko tu ya kwamba ni mcheshi mwenye kudanganya.”

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Hibbaan al-Bustiy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Rawdhat-ul-´Uqalaa’ wa Nuzhat-ul-Fudhwalaa’, uk. 53-56
  • Imechapishwa: 12/11/2016