128. Ni ipi hukumu ya kuhamisha viungo vya maiti baada ya kufa kwake?

Swali 128: Ni ipi hukumu ya kuhamisha viungo vya maiti baada ya kufa kwake[1]?

Jibu: Muislamu ni mwenye kuheshimiwa akiwa hai na baada ya kufa. Kilicho cha wajibu ni kutofanya ukiukaji kwa yale yanayomuudhi au yanayofanya vibaya umbile lake kama vile kuvunja na kukata kiungo chake. Imepokelewa katika Hadiyth:

“Kuvunja mfupa wa maiti ni kama kuuvunja akiwa hai.”[2]

Hadiyth inajengewa hoja kutofaa kumkatakata kwa manufaa ya waliohai. Mfano wa hilo ni kama kuchukua moyo wake, figo lake na viungo vyenginevyo. Kwa sababu kufanya hivo ni kukubwa zaidi kuliko kuvunja mfupa wake.

Wanazuoni wamekinzana juu ya kufaa kujitolea viungo na baadhi yao kwamba jambo hilo lina manufaa kwa waliohai kutokana na wingi wa magknjwa ya figo. Maoni haya yanatakiwa kutazamwa vizuri. Maoni ya karibu zaidi kwangu ni kwamba haifai kutokana na Hadiyth iliyotajwa. Isitoshe kufanya hivo ni kucheza na viungo vya wafu na kuvitweza. Wakati mwingine warithi wanaweza kuwa na tamaa ya pesa na hawajali ile heshima ya maiti. Warithi hawarithi mwili wake na hakuna wanachorithi isipokuwa tu ni ile mali.

[1] Majmuu´-ul-Fataawaa (13/363).

[2] Ahmad (24218), Abu Daawuud (3207) na Ibn Maajah (1616).

  • Mhusika: Imaam ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah bin Baaz
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Ahkaam-ul-Janaa-iz, uk. 93-94
  • Imechapishwa: 16/01/2022