121. Nasaba ya Mtume ( صلى الله عليه وسلم) na aina mbili za waarabu

Kuhusu nasaba yake yeye ni Muhammad bin ´Abdillaah bin ´Abdil-Muttwalib bin Haashim bin ´Abdul-Manaaf bin Quswayy bin Kilaab. Anatokana na kabila la Quraysh ambalo ndio kabila bora. Quraysh wanatokana na kabila la Ismaa´iyl (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam).

Waarabu wamegawanyika aina mbili kwa yaliyotangaa:

1- Waarabu wa asili (al-´Arab al-´Aaribah). Nao ni wale Qahtwaaniyyah.

2- Waarabu waliojifunza uarabu na utamaduni wao kutoka kwa wale wa asili (al-´Arab al-Musta´ribah). Nao ni wale al-´Adnaaniyyah wanaotokana na kizazi cha Ismaa´iyl bin Ibraahiym (Swalla Allaahu ´alayhim wa sallam). Wameitwa al-Musta´ribah kwa sababu walijifunza kiarabu kutoka kwa wale waarabu wa asili wakati walipofika Jurhum na wakatua Makkah kwa Haajar, mama yake Ismaa´iyl, na kipndi hicho mwana wake Ismaa´iyl alikuwa mchanga. Walipopata maji ya zamzam ndipo wakatua hapo. Wakamuomba Haajar kushukia hapo na awaruhusu wateke maji. Ismaa´iyl (Swalla Allaahu ´alayhim wa sallam) alikuwa ni mwenye kunyonya katika kipindi hicho. Baadaye akakua na kulelewa na akajifunza kiarabu kutoka Jurhum ambao walikuwa al-´Arab al-´Aaribah na akaoa hapo kutoka Jurhum. Akapata watoto ambao walijifunza kiarabu na wakakua pamoja na waarabu. Wakawa ni al-´Arab al-´Aaribah ambao ni al-´Adnaaniyyah. Kuhusu al-´Arab al-´Aaribah ni Qahtwaaniyyah msingi wao ni kutoka Yemen.

Wapo wanachuoni wengine waliosema kuwa waarabu wa asili (al-´Arab al-´Aaribah) wamegaanyika sampuli mbili:

1- Waarabu wa kale (´Arab Baa-idah).

2- Waarabu waliobaki (´Arab Baaqiyah).

Waarabu wa kale ni wale walioangamia. Nao ni watu wa Nuuh, ´Aad na Shu´ayb.

Kuhusu waarabu waliobaki ni wale waliogawanyika katika al-´Arab al-´Aaribah na al-´Arab al-Musta´ribah. Hawa ndio wale waarabu waliobaki.

Haashim anatokana na kizazi cha Ismaa´iyl (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam).

Jina lake ni Muhammad bin ´Abdillaah bin ´Abdil-Muttwalib. ´Abdul-Muttwalib sio jina lake. Jina lake anaitwa Shaybah. Aliitwa hivo kwa sababu ami yake al-Muttwalib bin ´Abdil-Manaaf alikuja naye kutoka Madiynah akiwa ni mdogo kutoka kwa wajomba zake Banuu-un-Najjaar. Wakati watu walipomuona amepiga weusi kwa sababu ya safari wakafikiria kuwa ni mja na mtumwa wa al-Muttwalib na ndipo wakasema “´Abdul-Muttwalib bin Haashim bin ´Abdil-Manaaf. ´Abdul-Manaaf alikuwa na watoto wanne:

Wa kwanza: Haashim ambaye ni babu yake Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam).

Wa pili: al-Muttwalib.

Wa tatu: ´Abdush-Shams.

Wa tatu: Nawfal.

Kizazi cha Haashim wanaitwa “Haashimiyyuun”. Kizazi cha al-Muttwalib wanaitwa “Muttwalibuun”. Kuhusu ´Abdush-Shams katika wao anaingia pia ´Uthmaan (Radhiya Allaahu ´anh) na Banuu Umayyah. Watu hawa wanatokana na kizazi cha ´Abdush-Shams.

Nawfal ana watoto na miongoni mwao anaingia Zubayr bin Mutw´am, al-Hakiym bin Hizaam.

Ibraahiym (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alikuwa na mtoto ambaye ni Ismaa´iyl na yeye mkubwa. Yeye ndiye babu wa waarabu wa ´Adnaaniyyah. Ishaaq ndiye babu wa wana wa israaiyl. Mitume wote wanatokana na kizazi cha Ishaaq isipokuwa tu Mtume wetu (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam), Mtume wa mwisho, ambaye yeye anatokana na kizazi cha Ismaa´iyl.

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh Thalaathat-il-Usuwl, uk. 244-246
  • Imechapishwa: 04/02/2021