12. Vipi inatakiwa kumuamini Allaah (´Azza wa Jall) kwa njia ya upambanuzi?

Swali 12: Vipi inatakiwa kumuamini Allaah (´Azza wa Jall) kwa njia ya upambanuzi?

Jibu: Tunathibitisha na kukiri kwa nyoyo na midomo yetu ya kwamba Allaah ni wajibu awepo. Ni mmoja pekee. Kila mmoja ni mwenye kumuhitajia Yeye na Yeye hamuhitajii yeyote. Amepwekeka kwa kuwa na ukamilifu, utukufu, ukubwa na ujalali wote. Ana ukamilifu wa kipindukia kiasi cha kwamba viumbe hawawezi kuzunguka kitu katika sifa Zake.

Yeye ni al-Awwaal ambaye hakuna kitu kabla Yake.

Yeye ni al-Aakhir ambaye hakuna kitu baada Yake.

Yeye ni adh-Dhwaahir ambaye hakuna kitu juu Yake.

Yeye ni al-Baatwin ambaye hafichikani na kitu.

Yeye ni al-´Aliyy na al-A´laa kwa dhati, ujuu wa hadhi na ujuu wa nguvu.

Yeye ni al-´Alim anayekijua kila kitu.

Yeye ni al-Qadiyr ambaye ni muweza juu ya kila kitu.

Yeye ni as-Samiy´ anayezisikia sauti zote pasi na kujali lugha na haja.

Yeye ni al-Baswir anayekiona kila kitu.

Yeye ni al-Hakiym anayehukumu viumbe Wake kwa hekima na kwa Shari´ah.

Yeye ni al-Hamiy anayehimidiwa kwa sifa na matendo Yake.

Yeye ni al-Majiyd aliye na enzi katika utukufu na ukubwa Wake.

Yeye ni ar-Rahmaan na ar-Rahiym ambaye huruma Wake umeenea kote na kukizunguka kila kilichopo.

Yeye ni al-Malik na al-Maalik anayekimiliki kila kitu. Mbingu na ardhi ni Vyake. Vyote hivyo ni waja Wake na wanaendeshwa na Allaah.

Yeye ni al-Hayy aliye na uhai mkamilifu uliokusanya sifa Zake zote za dhati.

Yeye ni al-Qayyuum aliye kivyake na vyengine viko kwa ajili Yake.

Ni Mwenye kusifika kwa matendo Yake yote. Anafanya kile Anachotaka. Anachotaka, huwa, na Asichotaka, hakiwi.

Tunashuhudia kuwa Yeye ndiye Mola wetu na mtengeneza sura aliyeumba viumbe kwa njia ya kihohadi.

Tunashuhudia ya kwamba hakuna mungu wa haki isipokuwa Allaah ambaye anastahiki kuabudiwa.

Hatunyenyekei kwa mwengine asiyekuwa Allaah. Haturejei wakati wa kutubia kwa mwengine asiyekuwa Allaah. Hatuelekei kwa mwengine asiyekuwa Allaah. Yeye ndiye tunayemwabudu na Yeye ndiye ambaye tunamtaka msaada. YTujeye ndiye ambaye tunamtarajia na kumcha.

Tunatarajia huruma Wake na tunachelea uadilifu na adhabu Yake. Hatuna Mola mwengine asiyekuwa Allaah. Tunamuuliza na kumuomba Yeye. Hatuna mungu mwengine wa kuabudu asiyekuwa Yeye. Tunamtarajia. Yeye ndiye Mola wetu anayeitengeneza dini yetu na dunia yetu. Yeye ndiye mbora kabisa wa kunusuru na kutulinda na kila chenye kudhuru na kibaya.

  • Mhusika: Imaam ´Abdur-Rahmaan bin Naaswir as-Sa´diy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Ahamm-ul-Muhimmaat, uk. 73
  • Imechapishwa: 25/03/2017