1- Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Jilazimieni na ukweli. Kwani hakika ukweli unaongoza katika wema na wema unaongoza kwenda Pepo. Mtu hatoacha kuendelea kusema ukweli mpaka arekodiwe kwa Allaah kuwa ni mkweli. Tahadharini na uongo. Uongo unaelekeza katika dhambi na dhambi zinaelekeza kwenda Motoni. Mtu hatoacha kuendelea kusema uongo mpaka arekodiwe kwa Allaah ya kwamba ni mwongo.”

2- Allaah ameutukuza ulimi juu ya viungo vingine vyote, akainyanyua daraja yake na kubainisha fadhila zake kwa kuufanya ukatamka Tawhiyd tofauti na viungo vingine vyote. Kwa hiyo haifai kwa aliye na busara kutumia kifaa kilichoumbwa kwa ajili ya Tawhiyd katika uongo. Badala yake anatakiwa kuhakikisha daima anazungumza ukweli na kusema yale yenye kumnufaisha duniani na Aakhirah. Ulimi unapelekea katika yale imezowea. Ikiwa umezowea ukweli, utapelekea katika ukweli. Ikiwa umezowea uongo, utapelekea katika uongo.

3- Ismaa´iyl bin ´Ubaydillaah amesema:

“´Abdul-Malik bin Marwaan alinambia: “Wafunze watoto wangu ukweli kama unavyowafunza Qur-aan. Watenge mbali na uongo hata kama maisha yatatiwa khatarini.”

4- ´Aliy al-Bahdaliy amesema:

“Nilikuwa na Ibn ´Umar pindi mwiraki mmoja alipomwambia: “Wewe mtoto wa mnafiki!” Ibn ´Umar akasema: “Ole wako! Mnafiki ni yule ambaye anapozungumza anasema uong, anapoahidi anasema uongo na hatimizi kile alichoaminiwa.”

5- al-Fudhwayl bin ´Iyaadhw amesema:

“Hakuna kiungo kinachopendwa zaidi na Allaah kama ulimi mkweli. Hakuna kiungo kinachochukiwa zaidi na Allaah kama ulimi mwongo.”

6- Kila kitu anachotaka mtu kuazima ili kujipamba nacho ni sahali kukipata isipokuwa tu ulimi. Unasema yale imezowea. Ukweli unaokoa na uongo unaharibu. Mwenye kuudhibiti ulimi wake atazingatiwa kiongozi wa watu wake. Anayesema uongo sana hatojiachia kitu kukisadikisha. Hakuna anayesema uongo isipokuwa tu yule mwenye kujifanyia sahali.

7- Muhammad bin Ka´b al-Quradhiy amesema:

“Mwongo anasema uongo kwa sababu anajitweza mwenyewe.”

8- Uongo usingekuwa na ubaya wowote zaidi ya kwamba pindi mtu anaposema ukweli hasadikishwi ingelitosha kuwalazimu walimwengu wote daima kuzungumza ukweli. Moja ya maradhi ya uongo ni kuwa mwongo husahau. Mambo yakishakuwa namna hiyo anakuwa ni kama mtu ambaye siku zote anajitia utwevu.

9- Nasr al-Jahdhamiy amesema:

“Allaah ametusaidia dhidi ya waongo kwa kuwafanya kusahau.”

10- az-Zuhriy amesema:

“Lau ungelimwona Twaawuus basi ungelitambua kuwa hasemi uongo.”

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Hibbaan al-Bustiy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Rawdhat-ul-´Uqalaa’ wa Nuzhat-ul-Fudhwalaa’, uk. 51-53
  • Imechapishwa: 12/11/2016